Sunday, February 25, 2024

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano.

Kati ya matangazo hayo, tangazo la mkutano wangu wa tarehe 15 Februari mjini Faribault, Minnesota, lilitia fora.
 

Monday, February 19, 2024

MPIGA DEBE WANGU MPYA MAREKANI

Katika shughuli zangu za uandishi na kutoa ushauri kwa waMarekani na waAfrika kuepusha migogoro na matatizo mengine yatokanayo na tofauti za tamaduni, nina bahati ya kuwa na wapiga debe wa mataifa mbali mbali, wanawake kwa wanaume.

Mmoja ambaye amejitokeza miaka ya karibuni kama mpiga debe wangu ni Audrey Kletscher Helbling, mwanablogu maarufu wa hapa jimboni Minnesota. Alianza kunifahamu miaka michache iliyopita katika ushiriki wangu kwenye International Festival Faribault.

Wiki za karibuni amepata kusoma vitabu vyangu. Alianzia na Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences, ambacho alikiongelea katika blogu yake. Kwenye andiko lake hilo, alikuwa ananadi mhadhara wangu uliopangiwa kufanyika tarehe 15 Februari, 2024, mjini Faribault, jimbo la Minnesota.

Mdau huyu alihudhuria mhadhara ule na aliongelea vizuri sana katika blogu yake. Katika ujumbe wake huo, alinipigia debe, akahitimisha kwa kuwahimiza watu wasome vitabu vyangu, iwe ni kimoja au vyote.  Aliviorodhesha: Africans and Americans: Embracing Cultural DifferencesChickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences, na Matengo Folktales.

Inaniletea faraja na furaha kuwa na watu wa aina hiyo, wanaoona thamani ya kazi yangu kama ninavyoona mimi mwenyewe. Sifanyi kwa sababu yao, bali ni kwa maamuzi na mapenzi yangu mwenyewe, kama nilivyotamka katika video hii.

Video: Kipande cha Hotuba Yangu Books on Central


 Februari 15, 2024, nilitoa mhadhara mjini Faribault, jimbo la Minnesota, kuhusu tofauti za tamaduni baina ya waAfrika na waMarekani. Mhadhara ulifanyika katika duka la vitabu la Books on Central, na hapa naleta video ya kipande cha mhadhara, nikiwa nasoma paragrafu ya kwanza ya kitabu changu kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences

Sunday, February 18, 2024

Mwanablogu Marekani Akichambua Kitabu cha "Chickens in the Bus"

Mwanablogu na mwandishi Audrey Kletscher Helbing wa Minnesota, Marekani, ambaye ni mfuatiliaji wa shughuli zangu za kuelimisha katika jamii, amechapisha uchambuzi wa kitabu changu Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences.  Soma hapa.

Saturday, February 10, 2024

Taarifa fupi ya Mhadhara Mjini Owatonna.

Tarehe 8 Februari, nilikwenda mjini Owatonna, hapa katika jimbo la Minnesota. Nilikuwa nimelikwa na mkurugenzi wa Owatonna Public Library kutoa mhadhara juu ya changamoto za tofauti za tamaduni baina ya waAfrika na waMarekani.

Mahudhurio yalikuwa makubwa, kwa mujibu wa mkurugenzi. Miongoni mwa wahudhuriaji alikuwa bwana Tim Penny ambaye aliwa kuwa mjumbe katika bunge la wawakilishi hapa nchini Marekani.

Mhadhara ulikwenda vizuri, na wahudhuriaji walikuwa na masuali ya kusisimua. Kikao kilipoisha, watu walinunua vitabu, na mmoja wao alikuwa bwana Tim Penny aonekanaye pichani. Aliwahi kuwa mjumbe katika Baraza la Wawakilishi la Marekani.

Sunday, January 14, 2024

Vitabu Vinaenda Iran

 Tarehe 12 Januari, 2024, nilisafirisha vitabu vyangu viwili, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences, kwenda Tehran, Iran, kwa mwendesha kipindi cha televisheni kiitwacho THE ENLIGHTENMENT SHOW. Hii ilikuwa ni baada ya yeye kufanya mahojiano nami, akiwa amelenga zaidi kwenye mada ya fasihi ya Afrika na ukoloni, na pia mitazamo ya waMarekani kuhusu Afrika.

Mahojiano tulifanya kwa Zoom, na hii ilikuwa mara yangu ya kwanza kufanyiwa mahojiano Iran. Ninasubiri kwa hamu kupata mrejesho kutoka kwa watu wa kule, hasa baada ya vitabu vyangu kuwafikia.


Sunday, January 7, 2024

NIMEKABIDHI “CHICKENS IN THE BUS”

Januari 4, 2024, nilikwenda Maple Grove, kukabidhi nakala 20 za Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences kwa mama wa Cameroon ambaye alikuwa ameziagiza kwa ajili ya shule fulani nchini Cameroon.

Katika maongezi, mama huyu alinieleza habari za shule yenyewe, ambayo iko kaskazini magharibi mwa Cameroon, uliko mji wa Bamenda. Alinieleza kwamba lengo lake ni kuwa hivi vitabu visomwe na wanafunzi wa darasa la sita kwenda juu. 

Tuliongelea umuhimu wa kuwafundisha watoto wa kiAfrika juu ya utamaduni wetu, na kuwajenga katika kuuheshimu. Huyu mama alisisitiza kuwa yaliyomo katika Chickens in the Bus yanakidhi malengo hayo.

Mimi kama mwandishi nafurahi sana kujua kuwa watoto wa kiAfrika watakuwa wanasoma na kutafakari kitabu changu 
 

Thursday, December 21, 2023

"Chickens in the Bus" Kusomwa Shuleni Cameroon

Leo, tarehe 21 Desemba, 2023, nimepata habari ya pekee kuhusu kitabu cha Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences. Mama mmoja kutoka Cameroon aishiye hapa Minnesota, na ni mmoja wa wale ambao wamafahamu kazi zangu miezi ya karibuni, ameniambia kuwa anahitaji nakala za Chickens in the Bus kwa ajili ya kuzipeleka kwenye shule Cameroon, ambayo yeye mi mmoja wa wahusika. Amesema wanahitaji nakala 20 ili kila darasa liwe na angalau nakala tatu. 

Taarifa hii imenifanya nirudie kukipitia kwa uangalifu kitabu hiki, nijiridhishe hakina kosa lolote. Naogopa kuwapa watoto wa shule kitabu chenye kosa. Kwa mtazamo wangu, kusambaza kitabu chenye makosa ni uhalifu. Kuwapa watoto kitabu cha namna hiyo ni kosa la jinai.

Saturday, October 7, 2023

KIKAO MJINI MAPLE GROVE, MINNESOTA


Tarehe 30 Septemba, 2023, nilikwenda Maple Grove, Minnesota, kuongelea kitabu changu cha Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences. Kikao kilifanyika katika maktaba ya Maple Grove. Tulitambulishana na wale ambao hatukufahamiana. Tulibadilishana uzoefu na mawazo. 

Aliyeandaa na kuendesha kikako ni Samba Fall wa Senegal aonekanaye kulia kabisa kwenye hii picha. Yeye ni mratibu wa Multicultural Kids Network pia mjumbe katika Hennepin County Race Equity Advisory Council. Yeye na mimi tumefahaiana kwa miaka kadhaa.

Wadau walipata fursa ya kununua vitabu vyangu. Hii itachangia tafakari na maongezi yetu kuwa endelevu. Papo hapa, ndugu Samba Fall anataka vikao vya aina hii vifanyika katika maktaba zote za Hennepin County. Tumekubaliana hivyo.




Saturday, May 27, 2023

Kijitabu Hiki Kiuzwe Angalau Shilingi Milioni Moja

WaTanzania wenzangu, nimechapisha kijitabu, "Notes on 'Song of Lawino'" na sasa naleta hoja kuhusu bei yake.
Kijitabu hiki nimekiandika kutokana na jinsi ninavyoipenda fasihi. Nilipenda kuandika uchambuzi wa "Song of Lawino." Nimetumia miaka mingi kutafakari na kuandika. Ingekuwa ninalipwa kwa kila saa na siku niliyofanya hiyo kazi, ningekuwa tajiri.
Kwa maneno mengine, ingekuwa masaa yale yote na siku zile zote nimetumia kutengeneza na kuuza mkaa au kwenye ajira katika ofisi fulani, ukizingatia elimu yangu, ningekuwa nimeingiza mfukoni mamilioni ya shilingi.
Sasa kumbe matokeo ya shughuli yote hii ni kijitabu cha kurasa 70 tu. Watu watauliza bei yake ni shilingi ngapi. Ni dola 12, ambayo ni karibu shilingi 28,000. Najua kuwa wako watakaoshangaa bei hiyo kwa kijitabu cha kurasa chache.
Je, bei ya kitabu inawakilisha nini? Ndio thamani ya kitabu? Yaani tafakari yote na mawazo yote yaliyomo humu thamani yake ni hii shilingi 28,000? MTanzania akienda baa na hizi hela, atakunywa bia ngapi? Je kitabu hiki thamani yake ni sawa na hizi bia chache?
Binafsi, nakataa. Inatakiwa kitabu hiki kiuzwe angalau shilingi milioni moja. Angalau milioni moja, ukizingatia jasho nililotoa, na mikwamo niliyopitia. Niliyoandika humu nayaona kuwa ya thamani kubwa. Angalau kiuzwe milioni moja. Shilingi 28,000 ni dhuluma tupu, mchana kweupe.
Halafu, hiki ni kitabu ambacho hakitanunuliwa, labda na watu wachache sana. Huenda zisiuzwe nakala 10. Kingekuwa kitabu cha udaku, kingeuzika kwa kiasi fulani. Lakini hiki ni kitabu kikavu cha kitaaluma. Kitasota bila wateja. Hakitaniletea hela, labda visenti vichache. Ni kazi isiyo na ujira.
Mimi siandiki vitabu kwa ajili ya kupata hela. Nilitumia muda wangu wote huu kuandika hiki kitabu nikijua kuwa hakitauzika, labda nakala chache sana. Kinachonifanya niandike si pesa bali kuipenda kwangu fasihi. Nitaendelea kuandika.

 

Sunday, February 26, 2023

Mdau Kajipatia Vitabu

Jana ndugu aitwaye John Oketch kaweka picha katika ukurasa wa Facebook uitwao Africans in the United States, akiwa ameshika kitabu changu Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences. Ameambatanisha ujumbe akiwahimiza watu wajipatie nakala ya kitabu hiki. Picha hii imenivutia sana. Naona imepigwa kwa ustadi mkubwa.

>

Baadaye, ndugu Oketch aliweka hii picha nyingine, na ujumbe huu: thank you professor. I am grateful for your writing especially for my 4 kids who are born and raised in America. I have added your books to our African collection. Would you be kind to please share the link again in the reply just incase someone would like a copy.

Tafsiri: asante profesa. Nashukuru kwa uandishi wako hasa kwa ajili ya watoto wangu wanne ambao wamezaliwa na kulelewa hapa Marekani. Nimeviweka vitabu vyako katika maktaba yetu ya vitabu kuhusu Afrika. Je, unaweza, tafadhali, kuweka tena linki ya vitabu endapo kuna atakayehitaji nakala?

Nami nimeweka linki hii kwenye ukurasa ule wa Facebook.

Saturday, December 17, 2022

Cross Cultural Conversation With an American Student

Sophia ni mwanafunzi wangu hapa katika Chuo cha St. Olaf. Ni mfuatiliaji wa maandishi na maongezi yangu YouTube kuhusu tofauti za tamaduni. Siku chache zilizopita, aliniambia kuwa amepata kitabu changu, Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences. Aliniambia kuwa angependa tufanye mahojiano. Leo, tarehe 17 Desemba, tumekutana ofisini mwangu tukaongelea mengi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...