Saturday, June 27, 2009

Makala ya "Kwanza Jamii" Yachapishwa Marekani

Wiki kadhaa zilizopita, nilipata mwaliko kutoka kwa Ndugu Maggid Mjengwa, kuwa niandike makala katika gazeti lake jipya la Kwanza Jamii. Nilikubali, na niliandika makala ya kwanza yenye kichwa "Maendeleo ni Nini?." Makala hii ilichapishwa mwezi Aprili, 2009.

Siku moja, katika maongezi na Mmarekani Mweusi mmoja katika mji wa Minneapolis, nilimwambia kuwa nimeanza kuandika makala za kiSwahili katika gazeti moja la nyumbani Tanzania. Kwa vile alikuwa na duku duku ya kujua zaidi kuhusu makala hizo, nilimweleza kuhusu makala yangu hiyo ya kwanza. Huyu Mmarekani tulikuwa tumefahamiana kwa wiki kadhaa, tukiwa katika shughuli za kuandaa tamasha la utamaduni wa kiAfrika, liitwalo Afrifest.

Alivutiwa na mada na mtazamo wa makala, akasema ingefaa kuchapishwa katika gazeti la mtandaoni ambalo yeye na watu wengine walikuwa wanaliandaa. Alisema kuwa mawazo niliyoandika kuhusu maendeleo yatawafaa watu wa Marekani pia, kama vile waMarekani Weusi, ambao nao wamepitia msukosuko wa kutawaliwa kimawazo, kama waAfrika.

Tulikubaliana niitafsiri, na kisha imechapishwa katika gazeti hilo liitwalo TheUrbanFly.

Tuesday, June 23, 2009

Dala dala: Katuni ya Fadhili

Sijawahi kuwa na gari wala kuendesha gari Tanzania, ingawa mara kwa mara ninakuwa hapo. Nikiwa mahali kama Dar es Salaam, usafiri wangu ni kwa mguu au dala dala. Mara moja moja natumia teksi. Katuni hii, ambayo imetoka kwa Michuzi, imenigusa kwa ujumbe wake na namna yake ya kuyaelezea matatizo halisi kwa namna ya mchapo. Hii ni staili ambayo naipenda katika baadhi ya maandishi yangu.

Nategemea sana kuwa msanii huyu atakusanya katuni zake na kuchapisha kitabu au vitabu, aweze kuvuna matunda ya kazi yake ambayo ni ngumu. Wasanii wetu wanafanya kazi kubwa sana kwa manufaa ya jamii, lakini wanahujumiwa haki zao na jamii. Nikiwa mwandishi, mwenye haki juu ya kazi zangu sawa na hao wasanii wetu, nawapigia debe ili wafaidike na kazi zao.

Saturday, June 20, 2009

Nauza Vitabu Vyangu

Leo nimeona niandike kuhusu jinsi nilivyoanza kuuza vitabu vyangu. Naamini habari yangu itawasaidia waandishi wengine.

Mimi ni mwalimu, mtafiti, na mwandishi. Nimeshachapisha vitabu kadhaa. Lakini napenda niongelee vitabu viwili: Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nilichapisha Matengo Folktales mwaka 1999 hapa Marekani. Lazima nikiri kuwa mara baada ya kitabu kutoka, sikuwa na furaha sana. Ingawa nilikuwa nimetumia yapata miaka 23 kukiandaa kitabu hiki, na ingawa kutokana na ujuzi wangu wa taaluma hii nilijua kuwa ni kitabu muhimu, sikuwa na raha kilipotoka mtamboni. Kwa namna isiyoelezeka, nilijiuliza kama watu watakionaje. Vile vile nilifahamu kuwa, ingawa nilikuwa nimechoka kabisa kukiboresha kitabu hiki, kama ningeendelea kukishughulikia, ningeweza kukiboresha zaidi. Uandishi ndivyo ulivyo. Huwezi ukafikia hatua ya kusema kitabu chako kimekamilika, hakina upungufu wowote, na hakiwezi kuboreshwa zaidi.

Hata hivi, wasomaji walipoanza kunieleza kuhusu kitabu hiki, nilianza kupata hisia tofauti, kwani walikipenda kwa namna moja au nyingine. Basi nilianza kutulia, na kukiacha kitabu kiendelee kuwepo na kusambaa duniani. Mwaka 2005 nilichapisha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitabu hiki kinapigiwa debe na watu wengi, taasisi, vyuo, ma mashirika kama vile Global Service Corps, shirika la kiMarekani linalowaleta watu wa kujitolea huko Tanzania.

Nilianza kujifunza zaidi habari za uuzaji wa vitabu. Kama waandishi wengine, nilikuwa nadhani kuwa maadam kitabu kimetoka, kazi ya kukitangaza na kukiuza ni ya mchapishaji, na mimi naendelea na shughuli zangu zingine.

Lakini kujitafutia elimu katika vitabu na makala mbali mbali kulinisaidia kufahamu kuwa ukweli ni tofauti. Mwajibikaji mkuu wa kutangaza na kuuza vitabu ni mwandishi mwenyewe. Wachapishaji hawana uwezo wa kukitangaza kila kitabu kwa namna inayotakiwa. Kama mwandishi ni maarufu sana, wanakuwa na motisha ya kufanya hivyo. Na hata hivyo, umaarufu wa mtu kama huyu ni motisha ya kutosha kwa wasomaji kukitafuta kitabu chake wao wenyewe. Mtu kama Bill Gates au Osama bin Laden akiandika kitabu, wengi duniani watataka kukisoma, bila hata mchapishaji kukipigia debe.

Sasa, baada ya
kutambua kuwa jukumu la kuvitangaza vitabu vyangu ni langu, nilipata tatizo jingine. Mimi nafundisha chuo kikuu. Je, nina ubavu wa kukaa gengeni au kijiweni na kuuza vitabu? Watu watanionaje? Hii ilikuwa pingamizi kubwa. Ilikuwa ni kasumba ya usomi, ambayo baadaye niligundua haina mantiki nzuri.

Lakini, nilianza kujitafakari zaidi, kama ifuatavyo. Mimi ni mwalimu. Kazi yangu muda wote ni kuwaeleza watu fikra na mitazamo yangu. Katika taaluma yangu, hakuna ninachowaficha wanafunzi na watu wengine. Sasa iweje nisite kuvitngaza au kuviuza vitabu vyangu, wakati vitabu hivi ni sehemu ya yale yale ninayowaeleza watu siku zote? Je, kuwaonyesha watu vitabu vyangu kuna ubaya gani wakati lengo langu siku zote ni kuwagawia ujuzi wangu? Yaliyomo vitabuni ni yale yaliyomo kichwani mwangu, na ni sehemu ya nafsi yangu. Ninapoongea na watu, najitoa nafsi yangu. Kwa nini vitabu vyangu nivitenge kama vile si sehemu ya nafsi yangu?

Baada ya kupata utambuzi huo, nilianza kupata ujasiri wa kuviongelea vitabu vyangu kwa watu, sawa na ninavyoongelea masuala mengine yaliyomo katika uzoefu na ujuzi wangu. Nilianza kuhudhuria tamasha za vitabu nikiwa na meza ya vitabu vyangu. Nilianza kuona umuhimu wa shughuli hii. Watu wanakuja pale mezani na wanataka kusikia habari za shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, na uandishi. Na huwa sikosi kuwaelezea furaha ninayopata katika utafiti vijijini Tanzania na sehemu zingine, ingawa utafiti ni mgumu. Nawaeleza pia shughuli ninazofanya katika kuendeleza programu za kuwapeleka wanafunzi wa kiMarekani Afrika.

Jambo la msingi si kuuza vitabu; ni kukutana na watu, kuongea nao. Suala la vitabu linajitokeza lenyewe, bila hata juhudi ya pekee kwa upande wangu, kwani wakati wa mazungumo, watu hupenda kuangalia pia vitabu. Wanavyoridhishwa au kufurahishwa na taarifa za shughuli zangu, wanapata msukumo wa kujipatia kitabu. Cha muhimu ni kuwa na mazungumzo ya maana na ya kuvutia, na ni hayo ndio yanayowafanya watu wavutiwe na wazo la kununua vitabu.

Wengine, kwa hakika, wanatafuta vitabu, na wanavinunua hata bila maongezi. Wakishaona tu kitabu na kukiangalia kidogo, wanataka kukinunua. Na pengine wanaondoka bila hata mazungumzo, mbali ya kusalimiana tu na kuagana. Hao nao nawaheshimu, kama wale wanaopenda sana mazungumzo.

Naiona shughuli ya kuviongelea na kuvitangaza vitabu kama sehemu ya shughuli yangu ya ufundishaji. Ukweli ni kuwa mtu anayetaka kujifunza kutoka kwangu, atafanya vizuri akivisoma vitabu hivi na maandishi yangu mengine. Sioni sababu ya kuiona shughuli ya kuviongelea vitabu kwa namna nyingine. Naifurahia kama ninavyofurahia kufundisha darasani. Nakutana na watu wa kila aina, wenye taarifa na uzoefu wa namna mbali mbali. Kukaa kwenye meza na vitabu vyangu ni kivutio, na watu wanakuja wenyewe. Nafaidika sana na mazungumzo yangu na watu hao.

Kwa kumalizia, napenda nitaje jambo kuhusu waTanzania ambao wanapenda sana kulalamika kwamba watu kama mimi tunatumia nguvu zetu kuwafundisha watu wa nje badala ya kufundisha nchini. Lalamiko hili halina msingi madhubuti katika dunia ya leo yenye tekinolojia zinazowezesha mawasiliano kirahisi sana. Vitabu vyangu vinapatikana mtandaoni, kama nilivyoonyesha hapo juu. Hata kama mtu yuko Arusha, Mbeya, au Mtwara, anaweza kuviagiza akaletewa.

Lakini, kwa kuwa waTanzania wengi hawana uwezo wa kuagiza kwa njia hiyo, nimehakikisha kuwa vitabu hivi vinapatikana Tanzania, kama vile Dar es Salaam, simu namba 0717 413 073 au 0754 888 647. Kama kweli mtu ana nia ya kujifunza kutoka kwangu, anachoweza kufanya ni kuvitafuta vitabu hivi na kuvisoma, na baada ya hapo tunaweza kuendeleza mjadala kwa njia ya barua pepe. Watu huku Marekani, Ulaya, na sehemu zingine duniani tunawasiliana hivyo, bila kuonana uso kwa uso. Kwa jinsi mawasiliano yalivyo leo, mwalimu anaweza kukaa ofisini kwake Tanga na akafundisha darasa lenye watu walioko Morogoro, London, Pretoria, Kinshasa, na New Delhi. Watu waache kutoa visingizio, na badala yake wawajibike.

Sunday, June 14, 2009

Binadamu Amnyonyesha Mnyama


















Picha hii, iliyotokea tarehe 8 Juni, 2009, kwa Mjengwa, ya mama anayemnyonyesha mwanawe upande mmoja na mnyama yatima upande mwingine imenivutia na inanifikirisha.

Wengi wetu labda tutashangaa na kujiuliza kama huyu mama ana akili timamu. Lakini nadhani huyu mama anatufundisha au kutukumbusha mengi. Ni mama mwenye upendo na huruma. Habari hiyo hapa juu inasema kuwa huyu mama alikuwa anawalea watoto wake sambamba na huyu mnyama. Watoto na mnyama walikuwa wanacheza pamoja bila shida, na wakati wa kunyonyesha, mama anawanyonyesha wote kama inavyoonekana katika picha. Laiti nasi tungevipenda viumbe vyote namna hiyo hiyo. Lakini kwa wengi wetu, hata kuwapenda binadamu wenzetu tu ni shida. Uhasama, vita na magomvi hayaishi.

Huko tulikotoka, binadamu na wanyama tulikuwa pamoja, bila utengano. Pole pole kiumbe kinachoitwa binadamu kilibadilika na kuwa hivyo kilivyo leo. Lakini msingi wa maumbile yetu na wanyama wengine ni ule ule. Kama sisi wanadamu tunaweza kunywa maziwa ya ng'ombe na kustawi, kwa nini wanyama nao wasinyonye maziwa ya binadamu kama inavyoonekana katika picha hii? Huyu mama anathibitisha kuwa inawezekana, na hakuna madhara. Badala yake, anathibitisha kuwa ni faida pande zote.

Kuna hadithi nyingi na masimulizi mengine kuhusu binadamu waliolelewa na wanyama, labda kwa sababu ya kupotelea porini walipozaliwa, au kutelekezwa huko. Hadithi za aina hii zimekuwepo tangu zamani sana, sehemu mbali mbali za dunia. Warumi wa kale, kwa mfano, walikuwa na masimulizi kuwa waasisi wa mji wa Roma walikuwa Remus na Romulus, mapacha ambao walilelewa na wanyama porini. Hata miaka ya karibuni, zimeshatokea habari Uganda na sehemu zingine za kugunduliwa kwa binadamu ambao walilelewa na nyani porini.

Katika fasihi, tangu zamani za kale, habari hizi zimekuwepo. Katika hadithi ya Gilgamesh, iliyoanzia miaka elfu nyingi zilizopita katika nchi iitwayo Iraq leo, kulikuwa na mhusika aitwaye Enkiddu, ambaye aliishi porini na wanyama, kama ndugu wa damu. Ingawa kimwili alikuwa ni binadamu, hakuwa na tabia wala silika ya binadamu. Naye David Maluf, mwandishi maarufu wa Australia, ameelezea katika riwaya yake, Remembering Babylon, habari ya mtu aliyeanza kupoteza tabia na vipawa vya binadamu, kama vile lugha, kwa kuishi sana na wanyama.

Pamoja na mambo mengine, hadithi hizi zinatupa chemshabongo ya kutafakari nini maana ya kuwa binadamu.

Nafurahi jinsi huyu mtoto katika picha anavyomchungulia huyu mnyama. Haogopi. Na mnyama nae hawaogopi wanadamu. Laiti tungeendeleza jadi hii ya binadamu na wanyama kuishi pamoja bila uhasama. Leo hii, tuna uhasama mkubwa baina yetu na wanyama wa porini. Wakristu wanasimulia habari za Mtakatifu Francis wa Assisi, kwamba alikuwa anawapenda sana wanyama na ndege, nao walimpenda, wala hawakumwogopa, na walikuwa wanamkimbilia wakati wa shida. Ndege wa angani walikuwa wanakuja na kutua mikononi mwake, naye akiwalisha. Mtakatifu huyu aliwaita hao wanyama ndugu zake, kaka na dada.

Huyu mama katika picha anafanya vizuri kumlea mwanae katika tabia ya kuwa karibu na wanyama na kuwapenda na kuwajali. Tabia hii ingetufaidia wanadamu katika maisha yetu.

Mwandishi wetu maaarufu, Shaaban Robert, ni mmoja kati ya watu waliotuhamasisha kuwaheshimu na kuwapenda wanyama, ndege, na viumbe vingine. Katika maandishi yake alisisitiza muungano uliopo baina ya viumbe mbali mbali. Laiti kama tungezingatia mafunzo na falsafa yake; labda leo tungekuwa watunzaji wazuri wa wanyama na mazingira kwa ujumla.

Tuesday, June 9, 2009

Sunday, June 7, 2009

Viumbe "Anonymous" Katika Blogu

Kila anayepitia blogu mbali mbali atakuwa anaona maandishi yaliyoandikwa na viumbe viitwavyo "Anonymous." Mwanzoni, nilikuwa sioni ajabu wala kufikiria suala la viumbe hivi. Lakini, siku za karibuni, nimeanza kuvifikiria.

Ninapoona ujumbe umeandikwa na "Anonymous" huwa sioni sababu ya kujibu, kwani sielewi ni kiumbe gani kilichoandika, kama ni binadamu au mzimu. Na hata kama ni binadamu, sielewi kama ni jirani yangu au rafiki, ni mtu anayenifahamu au hanifahamu, na kadhalika.

Halafu, nikiviwazia hivi viumbe, suala zima la mijadala linakuwa kama sinema au hadithi ya ajabu ya Ughaibuni, ilivyoandikwa na Shaaban Robert katika kitabu chake cha Adili na Nduguze.

Ninapoona mlolongo wa maandishi kutoka kwa "Anonymous," nitajuaje kama ni "Anonymous" tofauti, au ni yule yule mmoja anatuchezea akili? Ni mambo ya Ughaibuni kabisa. Ni rahisi sana kwa "Anonymous" yule yule kuandika tena na tena, akitoa hoja mbali mbali, na sisi wasomaji tusigundue kuwa tunachezewa akili. Ndio maana huwa sitaki kujibizana na "Anonymous."

Juzi hapo nimerushiwa makombora na viumbe hivi kule kwa Michuzi , nami nikaogopa kujibu mapigo.

Kama viumbe hivi ni wanadamu wenzetu, kwa nini wasijitambulishe? Mimi ninapoandika kwenye hizi blogu, naweka jina langu. Ninafahamu kuwa mbele ya Mungu hakuna anayeweza kujificha. Kwa sisi Wakristu, dini inatufundisha kuwa siku ya kiyama, kila kilichofichika kitafichuliwa. Hii inanipa faraja moyoni, kwani kama hao "Anonymous" ni wanadamu wenzetu, nao tutawafahamu siku hiyo. Na hata kama ni mizimu, itafahamika pia.

Wednesday, June 3, 2009

Safari za JK Nje ya Nchi

Makala hii imechapishwa katika Kwanza Jamii.

Profesa Joseph L. Mbele

Leo nimeamua kuongelea safari za Rais Kikwete, maarufu kama JK, katika nchi za nje. Suala hili linazungumzwa sana na waTanzania. Wako wanaodai kuwa JK anatumia muda mwingi mno nje ya nchi badala ya kubaki nchini na kushughulikia masuala ya nchi. Wako wanaodai kuwa JK anaenda kuomba omba misaada. Wengine wanasema kazi ya kuzunguka nje ni ya waziri wa mambo ya nchi za nje, na kwamba kwa vile JK alizoea kuwa waziri wa mambo ya nchi za nje, bado hajabadilika, hata baada ya kuwa rais. Basi, kila mtu anasema yake, nami nimeona nichangie.

Naanza kwa kukiri kuwa nchi ya nje ninayoifahamu kuliko zote ni Marekani. Nimeishi na waMarekani katika nchi yao kwa miaka mingi, nikiwafundisha na kujumuika nao kwa namna mbali mbali. Naweza kusema nawafahamu, na suala la safari za JK katika nchi za nje, naweza kuliongelea kwa kutumia mfano wa Marekani.

Rais Kikwete ameshatembelea Marekani mara kadhaa, tangu awe rais. Binafsi, naona safari zake ni za manufaa. Kwanza, waMarekani kwa ujumla hawazijui nchi za Afrika kwa majina. Sana sana wanajua tu Afrika. Kuja kwa JK daima imekuwa ni fursa nzuri ya waMarekani kuijua na kuikumbuka nchi inayoitwa Tanzania. Kwa vile JK ni mtu mkubwa, ujio wake unatangazwa vilivyo, na hivi wahudhuriaji wanakuwa wengi. Fursa ya kuitangaza Tanzania inakuwa kubwa zaidi kuliko kama angekuja mbunge au waziri kama wanavyotaka baadhi ya Watanzania. Sio rahisi mbunge au waziri aje Marekani aweze kuwavuta watu kama anavyowavuta JK.

Watanzania wanaoishi Marekani wanayo fursa ya kuitangaza Tanzania, na wako wanaofanya hivyo, kwa kadiri ya uwezo wao. Lakini mtu kama Rais Kikwete anapokuja, suala hili linakuwa na mafanikio mara dufu. Kinachosaidia zaidi ni kuwa JK ana mvuto wa pekee kwa watu. Wamarekani walishangaa kuona alivyokuwa na uhusiano wa karibu na Rais Mstaafu Bush. Na hilo niliwahi kuelezwa pia na mzee mmoja Mmarekani, ambaye ni balozi mstaafu na mtu mashuhuri. Tayari, dalili zinaonekana kuwa JK na Rais Obama wataelewana vizuri. Kwa mtazamo wangu, ziara za JK zinatuweka waTanzania kwenye chati inayohitajika vichwani mwa watu wa huku nje.

Suala la uwezo wa JK kuitangaza Tanzania nililishuhudia alipofika katika jimbo la Minnesota, Septemba 26, 2006. JK alitunukiwa shahada ya heshima ya udaktari na Chuo Kikuu cha Mtakatifu Thomas, mjini Minneapolis. Baada ya Chuo kutoa wasifu wa JK na msingi wa kumpa tuzo hiyo, JK alitoa hotuba ambamo aliwaelimisha watu wa Minnesota kuhusu hali halisi, uwezo, malengo na mahitaji ya Tanzania na Afrika. Alielezea utajiri na fursa zilizomo katika nchi yetu na bara letu. Katika kuiongelea Tanzania, alitaja rasilimali tulizo nazo, kama vile madini, ardhi ya kilimo, vivutio vya utalii, na taratibu muafaka za kuwezesha uwekezaji. Aliongelea pia hali ya kijamii na kisiasa, kuwa ni nchi ya amani, ukifananisha na nchi zingine. Alisisitiza kuwa mazingira ya uwekezaji na ubia ni mazuri katika Tanzania na kuwa yanazidi kuboreshwa.

Hakuishia hapo, bali aliezea pia matatizo na mahitaji. Alisema kuwa pamoja na rasilimali zake, Tanzania haina uwezo wa kuziendeleza ipasavyo bila ushiriki wa wengine. Alisema kuwa Tanzania inahitaji mitaji na wawekezaji. Alisisitiza kuwa Tanzania si maskini anayehitaji kuhurumiwa na kutupiwa misaada. Inachohitaji ni washiriki katika kuufanyia kazi huu utajiri na kuleta faida kwa pande zote.

Kwa namna hii, JK alituweka Watanzania na Waafrika katika akili za WaMarekani, kwa namna tofauti na walivyozoea. Wao wamezoea kuisikia Afrika, na wengi wanadhani Afrika ni nchi ndogo, ambayo ni hoe hae kwa dhiki, njaa, maradhi na vita. JK alijenga picha tofauti miongoni mwa wali0hudhuria. Kwa yeyote anayewafahamu waMarekani, huu ni mchango mkubwa wa fikra, hasa tukizingatia kuwa vyombo vya habari viliripoti vizuri ujio wake.

Rais Kikwete alikuja na ujumbe mkubwa kutoka Tanzania, hasa wafanyabiashara. Kuja kwake na ujumbe wa wafanyabishara kulimaanisha kuwa Tanzania inataka kufanya biashara, si kuomba misaada. Ilifanyika semina kuhusu masuala ya biashara na uwekezaji Tanzania. WaTanzania wengi wanaoishi huku Minnesota walihudhuria, na walikiri kuwa semina hii ilikuwa muhimu sana. Kwa maoni yangu, JK alitekeleza vizuri jukumu lake.

Kilichobaki ni upande wetu waTanzania. Ingekuwea bora kama waTanzania waliohudhuria wangefanya utaratibu wa kuwaelezea wenzao ambao hawakupata fursa ya kuhudhuria, ili kuyatafakari na kuyafanyia kazi yale ambayo yalitokana na ujio wa JK. Ulihitajika utaratibu wa sisi waTanzania kuendeleza mawasiliano na waMarekani, baada ya JK kuwahamasisha. Sisi tungepaswa tuikuze ile mbegu ambayo JK alikuwa ameipanda.

Lakini waTanzania hatukujizatiti kufanya hayo. Inawezekana wako wanaoendeleza masuala aliyoanzisha Rais Kikwete, lakini sio kama jumuia. Labda wako ambao wanafuatilia, lakini hakuna taarifa. Hatuna vikao ambapo tunaelimishana na kuhamasishana. Tunakutana tu kwenye misiba au sherehe. Kama vile ilivyo Tanzania, kwenye sherehe waTanzania tunajitokeza kwa wingi. Lakini kwenye masuala ya kushirikiana katika maendeleo, ni wazi tunahitaji kujirekebisha.

Ziara ya JK ilileta msisimko miongoni mwa watu wa Minnesota, na iliripotiwa vizuri katika vyombo vya habari. Ilikuwa ni juu yetu waTanzania kutumia fursa hii iliyotengenezwa na JK ili kuendelea kuwa karibu na watu wa Minnesota, na kuwa nao bega kwa bega, kupanga mipango na mikakati ya uwekezaji, ubia, biashara, na kadhalika.

Kwa maoni yangu, wale wanaosema JK anazunguka nchi za nje kuomba omba misaada hawasemi ukweli. Kuhusu hoja kuwa kazi ya kuzunguka nje JK awaachie wengine, sina hakika kama tutapata mafanikio kama anayoyapata yeye. Ikiwa tutamleta mbunge au waziri, sina hakika ni waMarekani wangapi watavutiwa kuja kumsikiliza. Wanaosema JK akae nchini ashughulikie matatizo ya ndani, huenda wana hoja, lakini, kwa mtazamo wangu, si rahisi kutenganisha mambo ya ndani na ya nje. Pengine kwa kujishughulisha na mambo ya nje Rais Kikwete anajenga mazingira mazuri ya kutusaidia kwa mambo ya ndani. Vile vile Tanzania ina viongozi wengi au watu wengi ambao tunawaita viongozi. Hao wanafanya kazi gani? Kwani ni lazima awepo JK kuwaelekeza watu wa wilayani au mkoani wajibu wao? Je tunamhitaji rais aje kuwahamasisha watu wazoe taka taka mitaani, au waendeshe magari kwa uangalifu? Tunao viongozi wengi, kuanzia mtaani hadi kwenye ngazi ya Taifa. Wanafanya nini, na wanashindwa nini mpaka awepo rais?

Watanzania tumezoea kukaa vijiweni na kutoa lawama kwa wengine. Nayachukulia malamiko kuhusu safari za nje za JK kwa msingi huo. Kama kila mwananchi na kiongozi angewajibika pale alipo, nchi yetu ingekuwa mbali. Lakini hii tabia ya kumlaumu rais na kumtaka awepo nchini kutuelekeza namna ya kusafisha mitaro iliyoziba ni visingizio vya waTanzania ambao wanapenda zaidi kukaa vijiweni na kukosoa kuliko kuwajibika.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...