Friday, January 15, 2016

Vitabu vya Kozi: Waandishi Wanawake wa ki-Islam

Jana, kama ninavyofanya kila siku, niliingia katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf, kuona kama vitabu vya kozi zangu za muhula ujao vimefika. Ni utaratibu wetu kwamba miezi au wiki kadhaa kabla ya kuanza masomo, tunapeleka dukani orodha ya vitabu tunavyotaka kutumia, na idadi yake, ili wanafunzi wavinunue.

Lengo langu hasa lilikuwa kuona kama vitabu vya kozi yangu mpya, "Muslim Women Writers," vimefika. Nimeona kuwa vyote vimefika, na hapa naleta orodha ya waandishi na vitabu, na majina ya wachapishaji:

1. Aboulela, Leila. Minaret. Grove. 
2. Ali, Monica. Brick Lane. Scribner.
3. Ba, Mariama. So Long a Letter. Waveland Press, Inc.
4. el Saadawi, Nawal. The Fall of the Imam. Telegram Books.
5. Hossein, Rokeya S. Sultana's Dream. Feminist Press.
6. Mattu, Ayesha. & Nura Maznavi. Love, InshAllah. Soft Skull Press.
7. Nafisi, Azar. Reading Lolita in Tehran. Random.

Nimekuwa nikiandika kuhusu kozi hii mpya katika blogu hii, kuelezea ninavyojiandaa kuifundisha. Nina hamasa juu ya kozi hii kwa sababu ya umuhimu wake, sio tu kwa maana ya kuelimisha jamii juu ya u-Islam, bali juu ya uwepo wa fasihi inayoandikwa na wanawake wa ki-Islam. Upekee wa kozi hii ni kwamba inahoji dhana iliyoenea miongoni mwa wengi kwamba wanawake wa ki-Islam hawana sauti au hawapaswi kuwa na sauti katika jamii.

Kama ilivyo kawaida yangu ninapofundisha fasihi yoyote, huwa napenda kufundisha vitabu nilivyowahi kusoma na vingine ambavyo sijavisoma. Wakati mwingine naweka zaidi vile ambavyo sijavisoma. Ninafanya hivyo kwa sababu fasihi ni bahari kubwa inayoendelea kujaa. Kuna waandishi wa zamani ambao wamefariki na kuna walio hai, na wengine watajitokeza baadaye. Haiwezekani kusoma kila kilichoandikwa. Fasihi ni bahari inayoendelea kujaa.

Katika orodha niliyoweka hapa juu, nimefundisha kazi za waandishi watatu. Wa kwanza ni Mariama Ba wa Senegal. Nilishafundisha riwaya zake mbili: So Long a Letter na Scarlet Song. Halafu nilifundisha riwaya mbili za Nawal el Saadawi: wa Misri: Woman at Point Zero na The Fall of the Imam. Mwaka juzi nilifundisha Minaret, riwaya ya Leila Aboulela wa Sudan Nitakuwa na urahisi fulani katika kufundisha maandishi yao katika kozi ya "Muslim Women Writers."

Hao wengine ni wapya kwangu. Nimewahi kusikia majina yao tu, na sijawahi hata kuwa na vitabu vyao, isipokuwa kimoja cha Monica Ali, ambacho pamoja kuwa nilikinunua miaka michache iliyopita, sijawahi kukisoma, hata ukurasa moja. Kwa hali hiyo, kuwasoma waandishi hao itakuwa ni kupanua na kutajirisha akili yangu.


Nina dukuduku zaidi kusoma Love, InshAllah, kitabu ambacho ni mkusanyo wa maandishi ya waandishi wengi, wanawake wa ki-Islam, waishio hapa Marekani. Baada ya kufundisha kozi hii kwa mara ya kwanza, nitaifundisha tena muhula utakaofuata, na wakati ule nitaweza kuingiza riwaya za waandishi wengine, kama vile Assia Djebar wa Algeria, na Alifa Rifaat wa Misri, ambaye kitabu cha hadithi zake, Distant View of a Minaret nimewahi kufundisha.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...