Sunday, April 15, 2018

Mialiko kwa Mwandishi wa Kitabu

Kutokana na mawasiliano kutoka kwa waandishi chipukizi Tanzania ninafahamu kuwa hao ni miongoni mwa wasomaji wa blogu yangu hii ambamo ninaandika mara kwa mara kuhusu vitabu. Mbali na kuviongelea vitabu, nimekuwa nikiandika kuhusu uandishi, uchapishaji, na uuzaji wa vitabu kutokana na uzoefu wangu.

Leo ninapenda kuongelea kipengele cha mialiko kwa mwandishi wa kitabu, jadi ninayoiona hapa Marekani, mwandishi kualikwa kuzungumza sehemu mbali mbali baada ya kuchapisha kitabu. Mada hii nimeigusia kwa kiasi fulani katika blogu hii Hata hivyo, nimeona niongezee neno.

Kama wewe ni mfuatiliaji wa blogu yangu hii, utakuwa unafahamu kuwa ninapata mialiko mara kwa mara kuongelea mada zinazohusiana na vitabu vyangu: Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Suali ni je, kwa nini watu wanialike badala ya wao kusoma tu nilichoandika? Wananialika nikawasomee?

Jibu ni hapana. Kinachowafanya wanialike ni kutambua kwao, baada ya kusoma kitabu, kwamba wana mambo yatokanayo na yale yaliyomo kitabuni ambayo wangetaka kuyafahamu zaidi. Kitabu changu si kwamba kinajitosheleza, bali kina madokezo muhimu. Ni chachu ya dukuduku kwa wasomaji. Hata kama hakijitoshelezi, wanavutiwa na mwelekeo wa fikra. Hiyo ni sababu muhimu ya kunialika nikazungumze nao.

Wengine wakishasoma kitabu, wanakuwa na imani kwamba ninaweza kuwasaidia mawazo juu ya mipango wanayotaka kutekeleza au mambo yanayowakabili. Kwa mfano, viongozi wa kampuni au taasisi wanaona kwamba ninaweza kuwasaidia katika kuzielewa na kuzitatua changamoto zitokanazo na kuwa na timu ya watu wa tamaduni mbali mbali. Mfano ni nilivyoalikwa RBC Wealth Management.

Kuhusu kitabu cha Matengo Folktales, watu wanataka kufahamu zaidi juu ya utamaduni wa kusimulia hadithi ulivyo Afrika na pia wanataka kusikiliza hadithi zinavyosimuliwa. Ndivyo ilivyokuwa nilipoalikwa chuo kikuu cha St. Benedict/St. John's na pia maktaba ya Redwing.

Kwa upande wa Tanzania, jadi hii ya kuwaalika waandishi kuzungumzia uandishi na vitabu ingekuwa na manufaa kama ilivyo Marekani. Waandishi wangekuwa wanaielimisha jamii uzoefu wao katika vipengele mbali mbali, kama vile jinsi walivyopata wazo la kuandika au walivyoanza kuandika, mchakato wa uandishi, ugumu au urahisi wake, vipingamizi, uchapishaji, uhusiano na wachapishaji, wasomaji, wahakiki, na wauzaji wa vitabu. Waandishi wangetumia fursa hizi kutoa ushauri kwa waandishi chipukizi.

Katika mkutano na mwandishi, vitabu vya mwandishi vinaweza kuwepo, ili wahudhuriaji wanunue. Huu ni utaratibu unaofanyika sana hapa Marekani. Ni njia nzuri ya vitabu kuifikia jamii. Vile vile, kwa uzoefu wangu hapa Marekani, uwepo wa mwandishi na jinsi anavyojieleza, kunawavutia watu kununua kitabu. Kitu kingine kinachovutia ni kusainiwa kitabu na mwandishi, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii, katika kubadilishana mawazo na mwanablogu Christian Bwaya.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...