Tuesday, March 29, 2011

Mkutano wa Peace Corps, Madison, Ulifana

Machi 24-27 nilikuwa Madison, Wisconsin, kuhudhuria mkutano wa Peace Corps, uliojumuisha waMarekani walioenda kujitolea Afrika chini ya mpango wa shirika la Peace Corps. Mwaka huu ni mwaka wa maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Peace Corps, na maadhimisho hayo yanafanyika sehemu mbali mbali hapa Marekani.

Mkutano huu wa Madison ulikuwa na mengi ya kuelimisha na kusisimua kuanzia historia ya kuanzishwa kwa Peace Corps hadi masimulizi na kumbukumbu za watu walioenda katika nchi mbali mbali za Afrika kujitolea katika nyanja mbali mbali.

Kulikuwa na masumulizi kuhusu Rais Kennedy ambaye alichangia kuotesha mbegu ya Peace Corps kwa mtazamo wake wa kuwahamasisha raia wake wawe na moyo wa kujitolea, si kwa nchi yao tu, bali kwa ulimwengu. Rais Kennedy aliweka sahihi ya kuzindua Peace Corps tarehe 1 Machi, 1961.

Kulikuwa na masimulizi kuhusu Sargent Shriver, ambaye ndiye alikuwa mwanzilishi wa Peace Corps, akiwa na moyo na ari isiyomithilika iliyowasha moto mioyoni mwa wana Peace Corps, moto ambao bado unaendelea kuwaka, ukiwahamasisha kwenda kujitolea sehemu mbali mbali za dunia, na kuishi katika mazingira yoyote.

Kulikuwa na masimulizi kuhusu Kwame Nkrumah alivyojenga shule sehemu mbali mbali za nchi yake, akakuta hana walimu. Ndipo alipomwambia Scriver kuwa wanahitajika walimu. Na Peace Corps ikafanya hima kuandaa watu wakaenda Ghana mwaka 1961. Jina la Julius Nyerere pia lilitajwa, kwani naye aliwakaribisha Peace Corps mapema hivyo hivyo.

Watu mbali mbali, kama vile mabalozi, wasomi, walimu, wajasiriamali na waandishi walikuwepo kuelezea kumbukumbu zao za Peace Corps na mtazamo wao kuhusu umuhimu wa Peace Corps katika maisha yao na ya wanadamu kwa ujumla.

Nilipata fursa ya kukutana na watu waliojitolea Tanzania, kama vile Mzee Ernie Zaremba, ambaye tulipiga hii picha. Tulipiga stori siku zote tatu kuhusu Tanzania. Yeye alijitolea miaka ya 1964-66 Mwanza, Misungwi. Mzee huyu sasa anajishughulisha na kurekodi habari za wana Peace Corps, na kuwaunganisha. Huwa anatembelea Tanzania kukutana na watu waliofahamiana na wana Peace Corps au waliofaidika kutokana na Peace Corps kwa namna moja au nyingine.

Nilipiga stori na Mark Green, ambaye alikuwa balozi wa Marekani Tanzania, 2007-2009. Nilianza kufuatilia habari za Mark Green alipokuwa balozi. Niligundua kuwa maskani yake ni Wisconsin, na kuwa aliwahi kufundisha katika kijiji fulani Kenya. Nilivutiwa na shughuli zake nchini mwetu, nikagundua kuwa tulisoma wote katika chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, ingawa hatukufahamiana. Mimi nilimaliza shahada ya uzamifu mwaka 1986 na yeye 1987. Sote tulifurahi kufahamiana.

Kitu kimoja kilichonifurahisha zaidi katika mkutano huu ni kukutana na rafiki yangu Mwalimu Wade DallaGranna, ambaye tulifahamiana mwaka 1980, nilipofika Madison kusoma. Yeye alikuwa amerejea kutoka Lesotho, ambako alikuwa mwana Peace Corps.

Tangu nilipomaliza masomo Madison na kurudi Tanzania katikati ya mwaka 1986, hatukuwahi kukutana tena, hadi hiyo juzi. Tulifurahi sana, tukawaambia wengine pia.

Nina mengi ya kuelezea kuhusu mkutano huu, na natengemea kuendelea kuandika. Inatia moyo na hamasa kubwa kuwemo katika jumuia kubwa namna ile ya watu ambao fikra na mazungumzo yao ni juu ya kujitolea na kuwasaidia binadamu wengine, kujenga mahusiano mema duniani, na kuwaletea wengine maisha bora na mafanikio.

3 comments:

Simon Kitururu said...

Asante kwa kutuwakilisha Prof. M!

Mbele said...

Shukrani kwa ujumbe. Kwa kweli, nilifurahi kuwa katika mkutano ule. Unajua, unapokuwa na watu maarufu, nawe unajisikiasikia umo :-)

Simon Kitururu said...

@Prof: :-)

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...