Saturday, November 12, 2011

Mbeya Nchi, Raisi Sugu

Kabla ya yote, sherti niseme kuwa nasikitishwa na mambo yaliyotokea Mbeya siku mbili tatu hizi zilizopita na kusababisha uvunjifu wa amani. Natoa pole kwa waathirika. Kwa kuangalia habari zilizopatikana, tatizo limesababishwa na ukosefu wa busara za kiuongozi.

Kati ya taswira zilizotolewa kutokana na matukio haya ya Mbeya ni hili bango lisemalo Mbeya Nchi Raisi Sugu. Picha nimeipata kutoka blogu ya Francis Godwin. Bango hili naona lina ujumbe wa kufikirisha. Kwa upande mmoja, mtu anaweza kusema kuiita Mbeya nchi ni makosa na dharau kwa nchi ya Tanzania.

Lakini kwa upande mwingine, inakuwa vigumu kuthibitisha kosa liko wapi. Neno nchi limekuwa likitumika kwa namna nyingi katika maisha yetu. Miaka ya zamani na hadi leo, tunaposema u-Gogoni, au u-Sukumani, tunamaanisha nchi ya wa-Gogo na nchi ya wa-Sukuma. Hakuna ubaya wowote hapa. Katika hali hii, inakuwa vigumu kuwakosoa wenye hili bango lisemalo Mbeya Nchi.

Kuna wakati tulikuwa na nchi ya Tanganyika. Nchi hiyo ilipata Uhuru mwaka 1961 na mwaka 1964 ikatoweka. Pamoja na kuwa nchi ya Tanganyika haipo, mwaka huu kuna shughuli za kukumbuka uhuru wa nchi hiyo ambayo imetoweka.

Leo kuna nchi iitwayo Tanzania. Kesho na keshokutwa, watu wanaweza kuamua kuififisha nchi hiyo pia, kama walivyoififisha Tanganyika. Kwa mfano, wanaweza kuiunganisha hii Tanzania na nchi jirani, wakatunga nchi tofauti kabisa, na Tanzania ikafa kama ilivyokufa Tanganyika. Labda wenzetu wa Mbeya wanakazana kuhakikisha kuwa nchi yao haipotei kienyeji namna hiyo.

Kuhusu Mheshimiwa Mbunge wa Mbeya, maarufu kama Sugu, jambo moja lililojitokeza ni jinsi anavyokubalika na wananchi, hususan walalahoi. Nimeguswa na jinsi alivyokuja Mbeya wakati wa vurugu, na wakati viongozi wa serikali na polisi wakiwa wameshindwa kuzidhibiti, akaweza kuwahutubia wananchi na kuwatuliza. Napata picha kuwa ana akili na busara ya kiuongozi. Niliwahi kushiriki mjadala kuhusu Sugu hapa. Picha nimeitoa kwenye blogu ya mbeyayetu.

Taarifa tulizozipata ni kuwa wananchi wa Mbeya walikuwa hawataki kumsikiliza kiongozi yeyote isipokuwa Sugu. Hapo ikabidi Sugu aondoke kwenye vikao vya Bunge Dodoma na kuwahi Mbeya. Umati aliohutubia unaonekana kwenye hizi picha, ambazo nimeziona kwenye blogu ya mbeyayetu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...