Sunday, November 25, 2012

Rais Obama Anunua Vitabu

Jana Rais Obama aliripotiwa akinunua vitabu kwenye duka dogo, kwa lengo la kuchangia mapato ya wafanya biashara wadogo. Alitanguzana na binti zake, akanunua vitabu 15 vya watoto, kwa ajili ya kuwagawia ndugu. Picha ionekanayo hapa ni ya J. Scott Applewhite, Associated Press.

Niliposoma taarifa hii, nilijiuliza je, ni lini tumewahi kuwaona vigogo wa Bongo wakinunua vitabu? Ni lini umewahi kumwona kigogo wa Bongo akiwa na wanawe katika duka la vitabu? Pia nilikumbuka kuwa niliwahi kuuliza katika blogu hii kama unaweza kumpa m-Tanzania kitabu kama zawadi ya Krismasi au Idd el Fitri. Soma hapa.

 Kama vigogo wa Bongo wangekuwa na utamaduni wa kuvithamini vitabu, wangeweza kuleta mabadiliko makubwa nchini. Wangeweza kuanzisha maktaba vijijini. Wangeweza kuanzisha klabu za usomaji wa vitabu.

Vigogo hao husafiri sana nje ya nchi. Kwenye viwanja vya ndege, iwe ni O'Hare, Schippol, Heathrow, Johannesburg, au Istanbul, kuna maduka ya vitabu. Vigogo hao wangeweza kununua vitabu kila wanaposafiri na kuvipeleka kwenye maktaba za mkoa, shule na vyuo. Hebu fikiria, ukimpelekea hata tu kamusi ya ki-Ingereza mwalimu wa shule kule Lindi au Kalenga, unakuwa umeleta mapinduzi fulani katika ufundishaji kwenye shule hiyo.

Sisemi tu kwa kujifurahisha au kuwalaumu wengine. Mimi mwenyewe nanunua sana vitabu, na hadi sasa ninavyo zaidi ya elfu tatu. Niliposoma Marekani, 1980-86 nilinunua vitabu vingi sana, nikarejea navyo Tanzania. Ingawa watu walinishangaa kwa kuleta vitabu badala ya gari, vitabu hivyo vimewafaidia wanafunzi na wasomi wengi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Baada ya kuja kufundisha Marekani, 1991, nimenunua vitabu vingi zaidi. Nikifanikiwa kuvisafirisha nitakaporudi Tanzania, itakuwa ni hazina kubwa kwa wapenda elimu. Ila sina hakika kama nitaweza kuvisafirisha, kwani ni vingi mno. Itabidi wa-Tanzania wafanye mchango waniletee hela za kusafirishia vitabu hivyo. Uwezo wanao sana, kama inavyothibitika katika michango ya sherehe mbali mbali. Vinginevyo huenda nikaamua kuviuza hapa hapa Marekani nipate hela za kununulia angalau bajaji. Itanisaidia baada ya kustaafu Tanzania.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...