Sunday, October 4, 2015

Uzushi wa Abdulrahman Kinana

Siku kadhaa zilizopita, niliiona mtandaoni makala iliyoandikwa na Abdulrahman Kinana, katibu mkuu wa CCM. Ilikuwa ni makala kali. Kinana anazitahadharisha nchi za magharibi kwamba mgombea urais Edward Lowassa na umoja wa vyama vya siasa ninavyomwunga mkono, yaani UKAWA, wakishinda uchaguzi, Tanzania itageuka kuwa ngome ya magaidi.

Makala yake imejibiwa na watu wengi, lakini nimeona nilete hapa uchambuzi wa Ahmed Rajab huu hapa. Ahmed Rajab amethibitisha vizuri uwongo na uzushi uliomo katika makala ya Kinana, nami sina sababu ya kurudia uchambuzi wake.

Ninapenda kuongezea mawili matatu. Kwanza, ni jambo la kushangaza kwamba Kinana anazielekea nchi za magharibi kama vile ni marafiki zetu wa kuaminiwa, au kama vile ni nchi zenye maslahi sawa na yetu. Ukweli ni kwamba nchi hizo zinafuata maslahi yao. Nchi kama Marekani imethibitisha katika historia yake kwamba haisiti kuwageuka wale waliojiaminisha kuwa ni marafiki wake. Mfano ni Saddam Hussein. Kinana angezingatia hilo.

Ni mradi gani huu anaofanya Kinana kwa kuziambia nchi za Magharibi kuhusu ugaidi Tanzania? Anadhani kwamba kwa kuongelea ugaidi Tanzania anajenga urafiki na hizo nchi za Magharibi?

Kinana anafanya mchezo wa hatari kwa usalama wetu. Hizi nchi za Magharibi, zikiongozwa na kinara wao Marekani, hazina mchezo wala subira na sehemu yoyote duniani ambayo inasemekana ina magaidi. Kwa mtu mwenye wadhifa mkubwa na nyeti kama Kinana kuwasema hao wa-Tanzania anaowasema kwamba ni magaidi ni kuyaweka maisha yao rehani.

Marekani imewakamata watu sehemu mbali mbali duniani ambao walisemw
a kuwa magaidi, hata kwa kusingiziwa, ikawapeleka Guantanamo na sehemu zingine. Wengine wamepoteza maisha kwa kushambuliwa na "drones" za Marekani. Hata hapa jirani Somalia imetokea hivyo. Na "drone" haina macho, inalipua hata wasiohusika, ambao huitwa "collateral damage." Tusipomdhibiti Kinana na uzushi wake, na CCM yake, tunaweza kuishia kuwa "collateral damage."

Kinana si wa kwanza katika CCM kuzua hii habari ya ugaidi. CCM ilishawazulia CUF kwamba wana ajenda ya ugaidi. Mwigulu Nchemba alishawazulia viongozi wa CHADEMA kwamba ni magaidi. Alishindwa kuthibitisha madai yake mahakamani
.

Kutokana na huu mchezo wa hatari anaofanya Kinana, endapo Marekani italeta "drone" kuwashambulia hao anaowaita magaidi, naombea ipotee njia, imlipue Kinana. Anayataka mwenyewe. Sisi wengine hatumo. Wakiturushia "drone" nyingine, naomba ipotee njia iilipue kamati au halmashauri kuu ya CCM. Wanajitakia wenyewe, kupitia kauli za katibu mkuu wao. Sisi wengine hatumo. Ikija "drone" nyingine, naomba ipotee njia iwalipue wana CCM. Wanajitakia wenyewe kwa kukishabikia chama hiki ambacho kinatishia usalama wetu raia tusio na hatia na ambao tunaitakia mema nchi yetu.

Jisomee makala ya Kinana hii hapa:

http://thehill.com/blogs/congress-blog/foreign-policy/253142-tanzania-cannot-be-allowed-to-be-the-new-front-for

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...