Thursday, October 1, 2015

Kwa Wanadiaspora: Fursa ya Kuitangaza Tanzania

Naandika ujumbe huu kwako mwanadiaspora mwenzangu, kuelezea mradi ambao nimehusika nao, wa kitaaluma na wenye fursa ya kuitangaza Tanzania. Mradi huo ni filamu juu ya mwandishi maarufu Ernest Hemingway, ambaye aliwahi kutembelea nchi yetu na Afrika Mashariki kwa ujumla mwaka 1933-34 na 1953-54.

Kutokana na safari hizo, Hemingway aliandika vitabu, hadithi, insha, na barua. Maandishi hayo ni hazina, kwa jinsi yanavyoitangaza nchi yetu, iwapo tutaamua kuwa makini katika kuyatumia. Mfano ni hadithi ambayo wengi wamesikia angalau jina lake, "The Snows of Kilimanjaro."

Nilifanya utafiti wa miaka kadhaa juu ya mwandishi huyu, hatimaye nikatunga kozi, Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi wa ki-Marekani kwenda Tanzania, tukatembea katika baadhi ya maeneo alimopita Hemingway, huku tukisoma maandishi yake.

Kozi hii imemhamasisha Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi hao, kutengeneza filamu, Papa's Shadow. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye hai. Tunaongelea umuhimu wa Afrika katika maisha, safari, uandishi, na fikra za Ernest Hemingway. Filamu inaonyesha sehemu mbali mbali alimopita Hemingway, kama vile Longido, Arusha, Mto wa Mbu, Karatu, na Babati, na hifadhi kama Serengeti na Ngorongoro. Inaonyesha pia wanafamilia wa mtengeneza filamu wakipanda Mlima Kilimanjaro.

Filamu imekamilika, na mimi nimeiangalia, nikaipenda sana. Lakini, kwa mujibu wa taratibu na sheria, inatakiwa kulipia gharama kadhaa kabla haijaonyeshwa au kusambazwa. Kuna kampeni ya kuchangisha fedha, na mimi ni mchangiaji mojawapo. Zinahitajika dola 10,000, kama inavyoelezwa hapa.

Tofauti na miaka iliyopita, wanadiaspora tunatajwa na serikali ya Tanzania siku hizi kwa sababu tunapeleka fedha ("remittances"). Ni mchango muhimu kwa uchumi wa nchi yetu. Lakini huu mradi ninaoelezea hapa ni njia nyingine ya kuifaidia Tanzania. Filamu hii, mbali ya kuelimisha juu ya Hemingway, ni kivutio kwa watalii. Nasema hivi kwa kuwa najua namna jina la Hemingway na maandishi yake yanavyotumiwa na wenzetu sehemu zingine za dunia ambako Hemingway alipita au kuishi. Mifano ni miji kama vile Paris (Ufaransa) na Pamplona (Hispania), na nchi ya Cuba. Wanapata watalii wengi sana.

Hiyo ninayoelezea hapa ni fursa kwetu wanadiaspora wa Tanzania. Tukishikamana na kuchangia filamu hii hata hela kidogo tu kila mmoja wetu, tutasaidia kumalizia kiasi kinachobaki. Imebaki wiki moja tu na kidogo. Ukitaka, tafadhali tembelea na toa mchango wako hapa katika tovuti ya Kickstarter.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...