Thursday, February 11, 2010

Mwaliko wa Mhadhara: Kampuni ya RBC Wealth Management

Nimealikwa na kampuni ya RBC Wealth Management mjini Minneapolis, kwenda kutoa mhadhara tarehe 19 Februari. Kampuni hii ambayo shina lake ni nchini Canada, inafanya shughuli zake sehemu mbali mbali duniani, ikiwa na wafanyakazi wanaozidi 80,000.

Kama ninavyosema mara kwa mara katika blogu zangu na maandishi mengine, dunia ya leo inavyozidi kuwa kijiji, na watu wa mataifa na tamaduni mbali mbali kujikuta wakifanya kazi pamoja maofisini, vyuoni, katika biashara, na kadhalika, ni muhimu kujielimisha na masuala ya tofauti za tamaduni. Kujielimisha huko ni msingi mojawapo wa mafanikio.

Kampuni ya RBC Wealth Management imenialika makusudi ili kuongelea suala la mahusiano baina ya watu wa tamaduni mbali mbali wanaofanya kazi katika kampuni hiyo, kwani wafanyakazi hao wanatoka sehemu mbali mbali za dunia. Kampuni hii ilishanialika miaka michache iliyopita, kuongea na viongozi na maofisa wa kampuni kuhusu masuala haya haya. Walitaka kupata mawaidha kuhusu namna ya kushughulika na wafanyakazi wao kwa jinsi ya kujenga na kuimarisha mahusiano mema. Hii ni njia ya kuboresha ufanisi na kujiimarisha kibiashara.

Katika mwaliko wa awali, na katika mwaliko wa sasa, nimeombwa nikaongelee masuala yaliyomo katika kitabu changu cha Africans and Americans na yatokanayo. Wameagiza nakala za kuwatosha watakaohudhuria. Naafiki wazo hilo, kwani mtu anaweza kusahau yasemwayo katika mhadhara, lakini kitabu ni kitu cha kudumu, nyenzo ya elimu endelezi.

Kuanzia mwaka juzi nimeenda Tanzania na kuendesha warsha kuhusu utamaduni na utandawazi. Niliamua kufanya hivyo kwa kutambua umuhimu wa suala hili la kujiandaa. Nimeona jinsi taasisi, makampuni na jumuia za huku Marekani zinavyojiandaa. Na kwa vile ninashuhudia mwenyewe, nina uhakika na ninachosema. Ili wa-Tanzania waweze kushindana vizuri na kupata mafanikio katika dunia hii inayozidi kuwa kijiji, ni muhimu wajiandae pia. Huu ndio ujumbe wangu.

Mihadhara ninayotoa huku Marekani, ambayo naiongelea kwenye blogu zangu, inanijengea ujuzi na uzoefu. Si tu kwamba nawafundisha wale ninaoongea nao, bali nami naelimika. Ninapoenda kwenye sehemu kama hii kampuni ya RBC Wealth Management, ninasikiliza masuali kwa makini na kuelewa hali halisi ya sehemu hii. Ni uzoefu ambao naamini utawafaidia wa-Tanzania, wa-Afrika, na wengine hapa duniani. Huwa daima napenda kukutana na watu wenye ari ya kujielimisha, kwani mimi mwenyewe sichoki kutafuta elimu na kuwapa wengine. Ni mzunguko ambao naamini unainufaisha dunia.

Ratiba ya warsha zangu Tanzania mwaka huu inaandaliwa. Warsha ya kwanza, "Culture and Globalization," itafanyika Arusha Community Church, tarehe 3 Julai, kuanzia saa 4 hadi saa 7. Itafanyika kwa lugha ya ki-Ingereza kwani wahudhuriaji huwa ni wa mataifa mbali mbali. Karibuni.

Saturday, February 6, 2010

Wamarekani Safarini Malawi

Leo nilikwenda mjini Chippewa Falls, katika jimbo la Wisconsin, umbali wa maili 123 kutoka Northfield, ambapo naishi. Nilienda kuongea na kikundi cha wa-Marekani wanaojiandaa kwenda Malawi kwa shughuli za kujitolea. Nilialikwa na Mama Diane Kaufmann, ambaye anaonekana kushoto kwangu, katika picha hapa juu. Yeye ameenda Malawi mara kadhaa, katika wadhifa wake kama mratibu wa mpango wa ushirikiano baina ya dayosisi ya Kanisa la kiLuteri Kaskazini Magharibi ya Wisconsin na Malawi. Ana uzoefu wa kupeleka vikundi vya wanadayosisi Malawi katika mpango huo. Vile vile tumeshirikiana kwa miaka kadhaa katika kuendesha mafunzo kwenye kituo cha Luther Point.
Kikundi nilichoenda kukutana nacho leo kinaenda Malawi kuwashughulikia watu wenye matatizo ya macho, na kuwagawia miwani. Wanatarajia kufanya shughuli hizo Karonga na Chitipa.
Baadhi yao wameshaenda Malawi, na kwa wengine hii itakuwa ni mara yao ya kwanza. Mama Kaufmann aliniita niongee nao kuhusu masuala ninayoongelea katika kitabu changu cha Africans and Americans. Alinieleza kabla kuwa washiriki wote watakuwa wamekisoma kitabu hiki kabla ya ujio wangu. Kama kawaida, mazungumzo na watu waliojiandaa namna hii yanakuwa ya kina, kwani yanalenga katika kufuatilia yale ambayo wamesoma.
Walifurahi kuwa nami, kwani walijisikia kama vile wameshanifahamu, kutokana na ninavyojieleza kitabuni. Nami nilifurahi kuwa nao na kuwasisitizia mambo ya msingi kuhusu kuishi au kushughulika na watu wa utamaduni tofauti na wetu. Kwa vile hao wanaenda kwa shughuli za matibabu, mazungumzo yetu yalilenga zaidi kwenye hali halisi ya kushughulika na watu katika hospitali. Tofauti za tamaduni zinajitokezaje katika mazingira ya hospitali.
Kwa bahati nzuri haya ni mambo ambayo nimeyawazia kwa muda mrefu, na katika kitabu changu nimeyagusia. Vile vile, nimekuwa nikijipatia uzoefu katika mazungumzo na wanafunzi wa masomo ya uuguzi wanapojiandaa kwenda Tanzania kimasomo.

Baadhi ya wasafiri hao walisoma katika chuo cha St. Olaf, na tulipata fursa ya kuongelea na kupiga soga kuhusu maisha chuoni hapa. Baadhi wamesoma maandishi yangu mengine, kama vile Matengo Folktales na Notes on Achebe's Things Apart. Niliona wazi kuwa hao ni watu makini ambao wanajishughulisha kufahamu habari za huko waendako.

Thursday, February 4, 2010

Kioo cha Lugha: Jarida la Kiswahili la Isimu na Fasihi

Leo nilienda posta nikakuta bahasha yenye vitabu ikiwa imetumwa Dar es Salaam. Sikujua ni vitabu gani. Nilipofungua nikakuta ni nakala za jarida la Kioo cha Lugha.
Nimefurahi kupata hazina hii nikiwa huku ughaibuni ambako natumia ki-Ingereza karibu muda wote. Sasa, kwa kusoma makala maridhawa zilizoandikwa na watafiti na walimu mahiri wa Tanzania, Kenya, na kwingineko, nitajiongezea ujuzi wa kutumia ki-Swahili katika taaluma, hasa isimu na fasihi.

Miaka ya karibuni nimepata msisimko wa kuandika kwa ki-Swahili, ili kujitoa katika giza la ujinga linalotukabili wasomi wengi. Ujinga huu ni pamoja na kutoelewa namna ya kutumia ki-Swahili ipasavyo, na pia kudhani kuwa ki-Swahili hakina uwezo sawa na lugha zingine katika kuelezea mambo, hasa taaluma.

Ninajitahidi kujikomboa. Mwaka jana, kwa mfano, niliandika makala nyingi kwa ki-Swahili, hadi nikachapisha kitabu. Wakati wa kuandika nilisoma kazi kadhaa za Shaaban Robert ili kujijengea uwezo na kujiamini katika kutumia lugha ya ki-Swahili. Ni kama muujiza kuwa leo nimeletewa majarida haya, kwani kiu yangu ya kujielimisha bado na itaendelea kuwa kubwa.

Natoa shukrani tele kwa Idara ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kunikumbuka hivyo.

Sunday, January 31, 2010

Nimefika Chuoni Augustana

Jana nilifika chuoni Augustana, Illinois, kutoa mihadhara. Jana jioni niliongea na walimu wachache kuhusu masuala ya utamaduni na utandawazi katika dunia ya leo na umuhimu wa kuwaandaa wanafunzi wetu ipasavyo. Leo nimepata fursa ya kuongea na wanafunzi wapatao 40, ambao wanaenda Ghana na Senegal kwa masomo.Nimekuja hapa chuoni Augustana kusaidia kukuza mpango wa masomo kuhusu Afrika. Profesa John Tawiah Boateng, kutoka Ghana, aliyesimama nami hapa juu, kulia, ni mmoja wa wahusika wa mpango huu, chini ya mratibu wa masomo yahusuyo nchi za nje katika chuo cha Augustana, Dr. Kim Tunicliff. Hapa chini wanaonekana wote wawili, Dr. Tawiah Boateng akiwa katika kunitambulisha kwa waliohudhuria.
Dr Tunicliff tulifahamiana miaka iliyopita, alipokuwa makamu rais wa jumuia ya vyuo vinavyoshirikiana katika eneo la Marekani ya Kati, Associated Colleges of the Midwest (ACM). Nilikuwa mwanabodi katika bodi ya uongozi wa jumuia ya vyuo hivi, nikiwa mshauri wa mipango ihusuyo ushirikiano kati ya vyuo hivi na Zimbabwe na Tanzania. Ingawa yeye alishaondoka ACM, mimi bado ni mwanabodi. Ni wakati huo wa uongozi wa Dr. Tunicliff ndipo nilipohamasika kuandika kitabu cha Africans and Americans, ili kuchangia suala la kuwaandaa wanafunzi waendao Afrika. Hayo nimetaja katika utangulizi wa kitabu.. Katika kunitambulisha, Dr. Tawiah Boateng aliongelea mengi kuhusu shughuli zangu za utafiti na ufundishaji na pia shughuli za kuendeleza mipango ya kuwapeleka wanafunzi Afrika. Yeye, sawa na Dr. Tunicliff wanakipenda kitabu changu na wanakitumia katika matayarisho ya wanafunzi waendao Afrika. Nilitumia muda wa saa moja na nusu kuongelea masuala mbali mbali ya kuwatayarisha wanafunzi hao kwa safari yao ya Ghana na Senegal. Nilisema kuwa kuishi katika utamaduni tofauti na wetu ni changamoto inayotuelimisha kuhusu mapungufu yetu na pia kutupa fursa ya kuwaelimisha wengine. Mapungufu hayo ni pamoja na tabia ya kudhani kuwa tunavyofanya katika utamaduni wetu ni sahihi, na watu wa utamaduni tofauti wanahitaji kurekebishwa. Huo ni mtego unaotukabili sote. Katika kuandika kuhusu utamaduni wa wengine kazi kubwa ni ya kujisafisha roho ili tuweze kuandika kwa kutumia misingi ya kila utamaduni, badala ya kutumia misingi ya utamaduni wetu kama kigezo cha ubora. Baada ya mhadhara wangu na masuali, tulitawanyika, tukaenda kupata chakula cha jioni.

Kwa mwandishi yeyote ni faraja kuona maandishi yake yanasomwa kwa makini. Nami nilifurahi kuona kuwa wote waliohudhuria walikuwa wamesoma kitabu changu. Masuali waliyouliza yalionyesha kuwa wamefuatilia kwa makini yale niliyoandika. Baada ya yote, baadhi ya wanafunzi waliendelea kuongea nami, na niliombwa kuweka sahihi kwenye nakala za vitabu vyao, kisha tukapiga hii picha ya mwisho.

Monday, January 25, 2010

Kiapo cha Uraia wa Marekani

Mtu anapoomba uraia wa Marekani, anakula kiapo, wakati wa kupewa uraia huo, na katika kiapo hiki anatamka kuwa hatambui mamlaka ya kiongozi wa nchi anakotoka juu yake, wala hatambui mamlaka ya serikali ya nchi anakotoka juu yake. Anaukana kabisa utii na uaminifu kwa kiongozi, serikali au himaya ya nchi alikotoka. Kiapo ni hiki hapa:

I hereby declare, on oath, that I absolutely and entirely renounce and abjure all allegiance and fidelity to any foreign prince, potentate, state, or sovereignty of whom or which I have heretofore been a subject or citizen; that I will support and defend the Constitution and laws of the United States of America against all enemies, foreign and domestic; that I will bear true faith and allegiance to the same; that I will bear arms on behalf of the United States when required by the law; that I will perform noncombatant service in the Armed Forces of the United States when required by the law; that I will perform work of national importance under civilian direction when required by the law; and that I take this obligation freely without any mental reservation or purpose of evasion; so help me God.

Friday, January 15, 2010

Kitabu Kuhusu Mlima Kilimanjaro

Asubuhi ya leo, nikiwa nazunguka katika duka la vitabu hapa chuoni St. Olaf, niliona kitabu kipya kuhusu Mlima Kilimanjaro. Nilikichukua na kuanza kukisoma. Ni kitabu chenye maelezo yalioyoandikwa na Michael Moushabeck na picha zilizopigwa na Hiltrud Schulz.

Mwanzoni mwa kitabu, Moushabeck anasema kuwa wazo la kitabu hiki alilipata wakati anahudhuria tamasha la vitabu London. Pale alikutana na mwandishi ambaye alikuwa ana mswada wa kitabu kuhusu Kilimanjaro. Waliongea, na Moushabeck akaamua kusafiri kuja Tanzania.

Kitabu hiki ni rekodi ya safari hiyo, kwa maneno na picha. Moushabeck anasema kuwa alijiandaa kwa kusoma sana kuhusu Mlima Kilimanjaro na mambo mengine, kabla na wakati wa safari ya kuja Tanzania. Na katika kitabu hiki anatumegea mawili matatu aliyoyapata katika kusoma huko. Kwa mfano, amemnukuu Ernest Hemingway, yule mwandishi maarufu, alivyouelezea Mlima Kilimanjaro. Amewanukuu waandishi maarufu kama T.S. Eliot, Marianne Moore, na kadhalika. Kitabu hiki kinavutia, kwa maelezo yake mazuri na picha.

Kama ilivyo kawaida yangu, nilipokuwa nakisoma, nilishindwa kujizuia kuwazia uzembe wa wa-Tanzania. Jambo hili nimelilalamikia na nitaendelea kulilalamikia. Wa-Tanzania hawaonekani kwenye matamasha ya vitabu. Sasa je, akili wanayoipata wenzetu kwenye shughuli kama hizi wa-Tanzania wataipata? Wa-Tanzania hawana utamaduni wa kusoma vitabu. Je, wataweza kuitangaza nchi yao kwa ufanisi? Hazina kama Mlima Kilimanjaro imo nchini mwetu. Lakini wanaoitangaza na kufaidika zaidi na hazina hii ni wageni, wakati sisi tunashinda vijiweni tukiilalamikia serikali kwa kukosa sera.

Je, tunahitaji sera ili tununue kitabu na kukisoma? Tutajuaje dunia inavyokwenda? Ni wazi kuwa, katika mchakato wa maendeleo ya dunia, wa-Tanzania watakuwa wasindikizaji. Ni wazi kuwa wameamua hivyo, na wameridhika. Nimeelezea sana matatizo ya wa-Tanzania katika kitabu changu kipya, CHANGAMOTO.

Saturday, January 9, 2010

Arusha na Kansas City: Miji Rafiki

Kama ilivyo kwa miji mingi hapa Marekani na duniani kwa ujumla, mji wa Kansas una utaratibu wa kujenga urafiki na miji mingine duniani. Arusha ni mji moja ambao tayari una urafiki huo na mji wa Kansas, kama inavyoonekana kwenye tovuti hii.

Nilifahamu habari ya uhusiano huu baina ya mji wa Kansas na Arusha tangu miaka kadhaa iliyopita, kwa kusoma taarifa mtandaoni. Kuna taarifa nyingi, lakini iliyonivutia zaidi ni ile ya harakati za Pete O'Neal, mwenyeji wa mji wa Kansas, ambaye aliikimbia nchi yake akahamia Arusha. Shughuli zake hapo Arusha ni pamoja na kuwa kiungo baina ya wa-Marekani na wa-Tanzania, kama inavyoelezwa hapa. Habari za mwanaharakati huyu zinaelezwa vizuri katika filamu iitwayo A Panther in Africa.

Katika kufuatilia habari hizi, nilianza kupata wazo la kuwasiliana na watu wa mji wa Kansas wanaoshughulika na mpango huu wa urafiki baina yao na Arusha. Nilishatembelea mji wa Kansas, kwa utafiti kuhusu mwandishi Ernest Hemingway, lakini si kuwa kufuatilia uhusiano baina ya mji huu na Arusha.

Mwaka huu, nilialikwa Kansas. Fursa hii ilitokana na Dr. Mbaari Kinya, mwanasayansi Mkenya, ambaye tulionana kwenye mkutano katika Chuo cha Principia, Illinois, ambapo nilikuwa mtoa mada mwalikwa. Dr. Kinya anaendesha taasisi inayoshughulikia nishati, mazingira, tekinolojia na maendeleo ya wanawake. Taarifa zake hizi hapa. Nilipoelezwa kuwa Dr. Kinya anaishi mjini Kansas, nilimweleza kwamba nafuatilia masuala ya uhusiano baina ya mji wa Kansas na Arusha, naye alisema anafahamiana na mratibu wa mpango huu. Aliporejea Kansas, alimpa taarifa zangu Eslun Tucker, na huo ukawa mwanzo wa mawasiliano baina ya Eslun nami. Kwa bahati nzuri, Eslun ni rafiki ya baadhi ya wa-Kenya waishio Kansas. Nao waliniulizia iwapo ningeweza kuhudhuria kumbukumbu ya Jamhuri ya Kenya, tarehe 12 Desemba. Elsun Tucker ni mama mmoja mwenye mawazo mapana kuhusu ulimwengu. Tofauti na wengi wetu ambao ni wa-Afrika au wenye asili ya ki-Afrika na tumejikita upande wetu tu, yeye ana uzoefu wa watu weusi wa kuanzia Marekani, hadi Caribbean, Afrika Mashariki na Afrika Magharibi.
Nilienda Kansas terehe 12 Desemba, kukutana na wahusika wa mpango huu wa urafiki baina ya Kansas na Arusha na pia kushiriki sherehe za kuazimisha kumbukumbu ya Jamhuri ya Kenya.
Katika kikao chetu alihudhuria pia Harvey Marken. Huyu ni mwalimu na mshiriki katika mpango wa ushirikiano baina ya Kansas na Arusha. Harvey Marken alitembelea Tanzania mara moja, ziara ambayo ilimgusa akaamua kujishughulisha na maendeleo ya shule ya Shangarao.

Alikuwepo pia Deo Rutabana, mwenyekiti wa jumuia ya wa-Tanzania wa mjini Kansas. Yeye ni mdau wa shughuli za maendeleo Tanzania. Nilivutiwa na ajenda za timu hii ya Kansas na ari yao ya kujenga na kuboresha mahusiano baina ya watu wa Marekani na Tanzania na Afrika kwa ujumla
Kati ya shughuli wanazofanya ni kuwawezesha watu kutoka miji hiyo miwili kutembeleana. Safari hizi zinahusisha watu wazima, vijana na watoto wa shule pia. Lengo moja kubwa ni kukuza maelewano baina ya watu wa Tanzania na Marekani.
Watu walioanzisha wazo hili la kujenga uhusiano baina ya mji wa Kansas na Arusha huenda walikuwa na ajenda fulani maalum, kwa mujibu wa taratibu za mipango ya aina hii. Lakini ukweli ni kuwa mbegu iliyooteshwa imekua na kueneza matunda sehemu nyingi. Imezaa mipango mingi yenye wahusika wa sehemu mbali mbali, Marekani na Tanzania. Mtandao huu utaendelea kupanuka.
Lengo langu kubwa ni kutafakari namna mahusiano ya aina yoyote baina ya watu wa tamaduni mbali mbali yanavyoathiriwa na tofauti za tamaduni.
Ni wazi kuwa, katika suala kama hili la uhusiano baina ya Arusha na Kansas, masuala ya tofauti baina ya utamaduni wa m-Tanzania na ule wa m-Marekani yatajitokeza. Ni lazima yashughulikiwe, sambamba na masuala mengine yote.
Katika mazungumzo ya aina hii tuliyofanya, mambo mengi yalijitokeza, mawazo na ushauri. Ni namna nzuri ya kuboresha mipango ilikwisha anza, na pia kuandaa mipango mingine.


Kamati ya Kansas inafahamu umuhimu wa kushughulikia suala la utamaduni. Kwa mfano, imeandaa kijitabu cha kufundishia ki-Swahili. Kuna wazo pia la kuandaa kijitabu kuhusu mapishi na vyakula. Zote hizi ni juhudi za kuuleta utamaduni wa ki-Tanzania katika mawazo na maisha ya watu wa Marekani. Ni muhimu vile vile wa-Tanzania nao tufanye juhudi kuwaelewa wa-Marekani, ili tunapokuwa pamoja tusiwe tunakutana kama wageni daima. Tunayo fursa ya kupunguza ugeni na kujenga maelewano ya karibu zaidi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...