Wednesday, March 17, 2010

Naishangilia Zanzibar

Siku kadhaa zilizopita nilipata fursa ya kusikiliza hotuba aliyotoa Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Shariff, kule Uingereza, akielezea makubaliano yaliyofikiwa baina yake na Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Amani Karume. Bofya hapa.

Nimeipenda sana hotuba ile, kwa jinsi ilivyojaa kumbukumbu, mawazo, tathmini na mawaidha kuhusu siasa Zanzibar. Nimevutiwa na jinsi Zanzibar ilivyofikia hatua ya kutathmini maana ya mfumo wa siasa ambao umetumika kwa yapata nusu karne na wakauona kuwa una dosari na ni chanzo cha matatizo. Mfumo huo ni wa vyama vya siasa.

Mimi mwenyewe nimehoji sana mantiki ya dhana nzima ya chama au vyama vya siasa. Mwaka jana niliandika makala nikihoji kama chama cha siasa au vyama vya siasa ni kitu cha lazima katika kujenga demokrasia. Nilisema kuwa tumeiga hii dhana kikasuku, na tunashinikizwa na mataifa mengine. Nilitamka kuwa labda kuna umuhimu wa kuangalia uwezekano wa kujenga demokrasia bila chama au bila vyama. Bofya hapa. Mawazo yangu, ambayo yanahoji mambo tuliyozoea, katika siasa, uchumi, utamaduni, elimu na kadhalika, yamo katika kitabu cha Changamoto.

Nimefurahi kusikia maelezo ya Maalim Seif kuhusu tathmini waliyoifanya Zanzibar, hadi wakafikia hatua ya kujenga ushirikiano baina ya CUF na CCM, na kuondokana na historia ya uhasama, kwa ajili ya maslahi ya Zanzibar. Wamefanya uamuzi wa maana, na nimefurahi kuona jinsi wanavyojipanga kuunganisha nguvu za wa-Zanzibar wote, walioko nchini na nje ya nchi, ili wajenge Zanzibar, ambayo zamani ilikuwa na historia na heshima kubwa duniani.

Naamini kuwa kwa Zanzibar kuchukua uamuzi huu, sote tutafaidika. Kuimarika kwa Zanzibar ni neema kwa Muungano. Wale waliokuwa wanaitumia Zanzibar kwa manufaa yao, wakawa wanaendekeza siasa za mfarakano, ndio pekee watakaoambulia patupu. Wale waliokuwa wanaendekeza ubabe wa kutumia nguvu ya chama au vyama, wamepewa somo kubwa. Nategemea watajifunza.

Hotuba hii ya Maalim Seif nimeona ni muhimu kuliko zote ambazo nimewahi kuzisikia kutoka kwa wanasiasa wetu tangu aondoke Mwalimu Nyerere.

Wednesday, March 10, 2010

Mteja Anapofurahi

Leo mama moja Mmarekani ameniandikia ujumbe kwenye ukurasa wangu wa Facebook. Anaelezea kuhusu kitabu changu cha Africans and Americans, na jinsi kilivyomsaidia alipokuwa Afrika Mashariki:

I remember being glad I had read it. Observations from someone who has lived in both Minnesota and East Africa, and a scholar no less, were a lot more insightful than my Lonely Planet.

Ni faraja kwangu kupata maoni ya wasomaji. Ni furaha kuwasikia kuwa wameridhika. Niliandika kitabu kwa sababu niliona kuna tatizo duniani lililohitaji ufumbuzi, tatizo la maelewano baina ya watu wa tamaduni mbali mbali. Lengo langu halikuwa kujipatia pesa. Hii Lonely Planet anayoitaja ni kampuni maarufu inayochapisha vitabu kwa ajili ya wasafiri. Vitabu hivi vinaelezea taarifa za nchi mbali mbali. Basi, nimetabasamu kusoma kauli ya huyu mama, kuwa kitabu changu ni tishio kwa Lonely Planet. Wakae chonjo.

Ni kweli kuwa watu wananunua kitabu hiki. Na mimi nazingatia hilo. Lakini jambo la msingi zaidi kwangu ni kuwa mteja aridhike. Asione kuwa alipoteza hela zake au kitu alichonunua hakikumridhisha. Mteja anapofurahi kama huyu wa leo, nami nafurahi.

Mara kwa mara, huwa naalikwa kwenda kutoa mihadhara kuhusiana na kitabu hiki au maandishi yangu mengine. Kama ilivyo kawaida hapa Marekani, wanaonialika wananiuliza gharama ya mihadhara yangu ni kiasi gani.

Ningekuwa mtu ninayeweka pesa mbele, ningesema hii ni fursa yangu ya kuwakomoa na kutajirika. Lakini mimi, pamoja na mahitaji mengi ya pesa ambayo sote tunayo, siwezi kufanya hivyo. Kwa nini nifanye jambo ambalo haliendani na dhamiri yangu? Sipendi makuu, na sikulelewa katika mkondo wa kujilimbikizia utajiri.

Ninaridhika na malipo ya wastani. Vile vile, hata kama taasisi au jumuia inayonialika haina pesa, mimi huwa naenda kuwapa mhadhara. Akili niliyo nayo nilipewa na Mungu, haikuwa haki yangu, wala siwezi kujivunia. Nina wajibu wa kuitumia kwa manufaa ya wanadamu, si kwa manufaa yangu binafsi. Ninaamini kuwa nikifanya ubinafsi, Mungu anaweza kuninyang'anya.

Furaha ya mteja ni malipo tosha kwa juhudi zangu, na ni njia ya kumtukuza Mungu aliyenipa uwezo.

Wednesday, March 3, 2010

Mfinyanzi Aingia Kasri: Siti Binti Saad

Mwaka jana, nilipokuwa Dar es Salaam, niliingia katika duka la vitabu, Dar es Salaam Bookshop, nikanunua vitabu kadhaa vya ki-Swahili. Vitatu vilikuwa vya Shaaban Robert, na kingine ambacho sikuwa nimewahi kusikia habari zake, kilikuwa juu ya Siti Binti Saad.
Kitabu hiki Mfinyanzi Aingia Kasri: Siti Binti Saad Malkia wa Taarab, kimeandikwa na Nasra Mohamed Hilal wa Malindi, Zanzibar, ambaye alikuwa mtangazaji wa Radio Tanzania Zanzibar kwa miaka 27. Kimechapishwa na Mkuki na Nyota Publishers, 2007.

Kwa mujibu wa taarifa iliyo ukurasa wa nyuma ya kitabu, Bibi Nasra "(a)mefanya utafiti wa historia ya wanawake wa makabila mbali mbali walioishi mjini Zanzibar na kuacha nyayo zao juu ya mila, utamaduni na sanaa. Hivi sasa anakamilisha vitabu vingine viwili. Zaidi ya uandishi Bibi Nasra ni mtengenezaji wa filamu wa kujitegemea na amekwishatoa filamu tano fupi, zote katika Kiswahili."

Natoa pongezi na shukrani kwa juhudi za mama huyu. Kitabu chake hiki kinathibitisha juhudi yake katika utafiti, kwani amekusanya habari na kumbukumbu nyingi kutoka kwa watu mbali mbali waliomfahamu Siti Binti Saad, wakiwemo ndugu zake.

Amekusanya nyimbo mbali mbali za Siti Binti Saad, nyingine zikiwa mpya kwetu ambao ufahamu wetu wa Siti Binti Saad unatokana na maandishi. Tuna bahati ya kuzipata taarifa na nyimbo nyingi namna hii katika kitabu kimoja.

Kuna mengi ya kujifunza kutokana na maisha na tungo za Siti Binti Saad, ambaye alipambana na matatizo mengi katika maisha yake, lakini akawa shujaa mwenye kujiamini muda wote. Alituachia mafundisho mengi murua. Kwa mfano, katika wimbo wake moja alisema

Ukicha kutajwa
Hutotenda jambo....

Alimaanisha kuwa kama unaogopa maneno ya watu, hutafanya kitu cha maana maishani.

Kama tunavyofahamu, msingi wa utafiti juu ya Siti Binti Saad uliwekwa na Shaaban Robert, katika kitabu chake cha Wasifu wa Siti Binti Saad. Katika kufuatilia habari za Shaaban Robert, nimeshangazwa na vipaji vyake. Kwa mfano, ingawa hakuwa na elimu kubwa ya shuleni, ikiwemo elimu ya utafiti wa masuala ya aina hii, Shaaban Robert alifanya kazi nzuri, akizingatia maadili ambayo leo tunafundisha vyuoni. Bibi Nasra ameutaja vizuri mchango wa Shaaban Robert na amemtolea sifa na shukrani ipasavyo.

Nategemea kupata wasaa wa kukichambua kitabu hiki cha Mfinyanzi Aingia Kasri siku zijazo na kuelezea maoni yangu vizuri. Kwa leo nimeona nikitaje tu, ili walimwengu wapate kufahamu uwepo wake.


















Tuesday, February 23, 2010

Nimejiunga "twitter"

Napenda kuwafahamisha wasomaji wa blogu hii na maandishi yangu mbali mbali kuwa nimejiunga "twitter," mtandao wa mawasiliano ya haraka haraka. Bofya hapa.

Shukrani kwa kuwa pamoja nami katika blogu hii. Nawakaribisha kujumuika nami "twitter" vile vile na kufuatilia shughuli zangu kwa karibu zaidi.

Saturday, February 20, 2010

Maandalizi ya "Afrifest 2010"

Leo nilienda Minneapolis kwenye mkutano wa maandalizi ya Afrifest, tamasha la utamaduni linalofanyika hapa Minnesota kila mwaka, kama kielelezo cha historia na mchango wa wa-Afrika katika ulimwengu.
Tulikutana katika mgahawa uitwao 1st Cup Cafe. Ni sehemu ambapo wa-Afrika hupenda kukutana na shughuli nyingi hufanyika hapo, kama vile mihadhara, uzinduzi wa vitabu, na burudani.

Mwanzilishi wa Afrifest ni Nathan White, ambaye anaonekana katika picha hapa juu, wa pili kutoka kulia. Mimi ninayeonekana kulia kabisa nimekuwa mwanachama wa kamati hii tangu mwanzo. Mchango wangu umekuwa zaidi katika kuelezea historia ya watu wenye asili ya Afrika, tangu chimbuko la binadamu katika Afrika hadi kuenea kwa wa-Afrika hao sehemu mbali mbali za dunia. Hilo ndilo somo ninalotoa siku ya tamasha, nikiwa na vielelezo kadha wa kadha vya kimaandishi.
Shughuli zote tunazofanya kama wanakamati ni za kujitolea, lakini tunazifanya kwa moyo mmoja kwa vile tunaamini umuhimu wa kuwakutanisha watu wenye asili ya Afrika kwa kufuata nyayo za wale waliotutangulia, kama vile Marcus Garvey, Kwame Nkrumah, W.B. Dubois, Gamal Abdel Nasser, Jomo Kenyatta, Julius Nyerere, Malcolm X, Bob Marley na Walter Rodney. Ni fursa ya kujielimisha sisi wenyewe, kujikumbusha tulikotoka katika historia yetu na harakati tulizopitia, mafanikio na matatizo, na pia ni fursa ya kuwaelimisha wa-Marekani na wengine.
Kwenye mkutano wetu huu tulishughulikia zaidi masuala ya kuandaa katiba ya "Afrifest Foundation." Tulianza shughuli za Afrifest tukiwa na mfumo tofauti, ila sasa tunataka kujiimarisha zaidi kwa muundo wa "Foundation."

Kwa mwaka huu, tumepangia kufanya tamasha la Afrifest tarehe 7 Agosti. Wanakamati tutakuwa na mikutano mingi hadi kufikia siku ya tamasha. Wajumbe wawili watatu hawaonekani kwenye taarifa hii, kwa vile walikuwa na udhuru siku hiyo.

Wednesday, February 17, 2010

Maongezi Mjini Faribault, Minnesota

Asubuhi leo nilikwenda mji wa Faribault, mwendo wa nusu saa. Nilikuwa nimealikwa na Mama Delane James, mkuu wa maktaba ya Faribault, kwenda kuongea na wafanyakazi wa maktaba kuhusu masuala ya utamaduni wa wa-Afrika.

Mji wa Faribault unazidi kuwa na watu kutoka pande mbali mbali za dunia, wengine wakiwa wakimbizi au wahamiaji wa kawaida au watafuta ajira. Miji mingi hapa Marekani inajikuta katika hali hiyo. Matokeo yake ni kuwa wenyeji wa miji hiyo na hao wageni wanakumbana na masuala yatokanayo na tofauti za tamaduni. Wahudumu wa maktaba wanakumbana na masuala hayo pia, kwani wageni hao nao ni wateja wa maktaba, ambapo wanatafuta ujuzi wa aina mbali mbali, kama vile lugha, ili kuweza kuyafahamu mazingira na maisha katika nchi ya Marekani.

Ingawa nilishafika katika maktaba ya Faribault mara kadhaa, sikutambua kuwa ina wafanykazi wengi kama niliowaona kwenye mkutano wa leo. Nilipata fursa ya kutoa mawaidha ya msingi kuhusu umuhimu wa kujifunza suala la tofauti za tamaduni, ili kuepusha matatizo. Nilizingatia uzoefu wangu na juhudi ninazofanya katika kujielimisha kuhusu tofauti hizo na kuwaelimisha wengine, iwe ni hapa Marekani au Tanzania.

Mji wa Faribault umewapokea watu wengi kutoka Afrika, hasa Somalia na Sudan. Kwa hivi, suala muhimu lililomfanya mkuu wa maktaba anialike ni kuelezea utamaduni wa watu hao. Mkuu wa maktaba na baadhi ya waliohudhuria walikuwa wameshasoma kitabu changu cha Africans and Americans, na waliuliza masuali kutokana na yaliyomo kitabuni. Pia waliwahamasisha wengine wote wakisome.

Mkutano ulikuwa wenye manufaa, na wahudhuriaji walisisitiza kuwa mazungumzo ya aina hii yanapaswa yafanyike sehemu zingine pia, kama vile shuleni na katika taasisi mbali mbali. Wanafanya mpango niende tena Faribault kutoa mhadhara kwa jamii na kusaini vitabu. Hayo nitaelezea yatakapotokea, panapo majaliwa.

Sunday, February 14, 2010

Fursa za Kuwatoa Upepo wa-Tanzania

Pamoja na kuwa kazi yangu ya msingi huku Marekani ni kufundisha, ninajishughulisha pia na mipango ya uhusiano baina ya vyuo vya Marekani na Tanzania na nchi zingine za Afrika. Mipango hii ni ile ya kupeleka wanafunzi Afrika. Kwa upande wa Tanzania, napata pia fursa ya kufanya mahojiano (intavyuu) na wasomi wanaotafuta nafasi ya kuja Marekani kwa masomo zaidi au utafiti.

Hizi ni kazi za kujitolea, lakini nazifanya kwa moyo moja, nikizingatia umuhimu wake kwa upande wa Marekani na nchi zetu, kwani, pamoja na kutoa fursa mbali mbali kwa wahusika, zinakuza maelewano duniani.

Mtu unapokuwa na fursa au wadhifa kama wangu, wa-Tanzania wanasema umeula. Wanaamini unalipwa hela nyingi sana, tena dola, si madafu. Pili, wanategemea kuwa unatumia fursa hizi kujitajirisha sana kifedha kwa msingi wa "akili mkichwa." Zaidi ya yote, wa-Tanzania wanataka wakuone unaishi maisha ya hali ya juu, si uwe unakula pilau au chapati kwenye vihoteli vya Ubungo au Kinondoni.

Siku moja, miaka ya tisini na kitu mwishoni, nikiwa Chuo Kikuu Dar es Salaam kwenye shughuli hizi za intavyuu, nilipanda dala dala pale Mwenge kuelekea Tegeta. Niliposhuka kituoni Tegeta, nilikutana na wa-Tanzania wanaonifahamu. Walishangaa kuniona nimepanda dala dala, wakaanza kunisema kwa nini ninahangaika na dala dala, wakati ningeweza kujipatia gari kutokana na hizi hizi intavyuu ninazowafanyia wasomi.

Mmoja wao aliniambia: "Sisi hapa Bongo, intavyuu ya kufagia ofisi za kampuni tunatoa laki tatu kwa bosi. Sasa je intavyuu za kwenda Marekani? Mbona mtu atakupa milioni, tena kwa hiari yake! Profesa Mbele unajitakia mwenyewe matatizo ya dala dala."

Sikujua namna ya kujitetea, nao waliendelea kunipa vidonge vyangu. Nategemea kwenda tena Tanzania, miezi ya usoni, kwenye shughuli nilizoongelea, na nafahamu kuwa vidonge zaidi vinaningoja.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...