Monday, March 19, 2018

Nimenunua CD za "Hamlet"

Leo niliingia katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf kununua vitabu ambavyo nilikuwa nimepangia tangu jana. Lakini wakati naangalia vitabu, niliona kifurushi cha CD za Hamlet, tamthilia ya Shakespeare.

Hiyo niliiona kama bahati ya pekee, kwa sababu siku chache zilizopita niliandika katika blogu hii kuwa tunasoma Hamlet. Ilikuwa ni wazi kuwa CD hizi nimeziona wakati muafaka. Nilichukua hicho kifurushi cha CD, nikakijumlisha na vitabu nilivyopangia kununua nikalipia vyote.

Jioni hii nimefungua kifurushi nikaona ziko CD tatu. Zimeandaliwa na Folger Theatre, ambacho ni kitengo cha Folger Shakespeare Library,  ambayo ndio makataba kubwa kuliko zote duniani za kazi za William Shakespeare na machapisho juu yake. Watafiti kutoka duniani kote wanafanya utafiti katika maktaba hii. Hamlet, kama ilivyo tamthilia zingine za Shakespeare, inapatikana katika matoleo mbali mbali. Folger Shakespeare Library ina toleo lake.

Kama nilivyosema, nimeanza kusikiliza jioni hii. Nimevutiwa sana na utambaji wa tamthilia. Wameonyesha uhodari mkubwa wa kuwasilisha sio tu maneno ya tamthilia bali pia vitu kama hisia na mazingira ya matukio. Kwa mfano, nimevutiwa sana na namna wanavyowasilisha tukio la kuonekana mzimu wa baba yake Hamlet. Mtu unasikiliza na unajhisi uko kwenye tukio unashuhudia.

Kusoma ni kutafsiri. Kusoma kwa sauti ni kutafsiri kwa namna ya pekee. Ni tabia ya tafsiri kwamba kila mtu anaibuka na yake. Ndio maana ninasema kuwa hizi CD zinagusa kwa namna ya pekee. Mimi mwenyewe, kwa kuzingatia ukweli huo, nilisoma kwa sauti shairi la W. B. Yeats, "The Second Coming," nikaweka katika blogu hii. Nilitaka niweke wazi kwa kutumia sauti uelewa wangu na hisia zangu juu shairi hili. Ni tafsiri yangu. Ukisikiliza usomaji wa wengine, ambazo zinapatikana mtandaoni, utajionea tafsiri tofauti za shairi hili hili.

Saturday, March 17, 2018

Tunasoma "Hamlet"

Muhula huu nina mwanafunzi mwingine aliyeamua kujitungia kozi yake mwenyewe na kuifanya chini ya usimamizi wangu. Utaratibu huu uko hapa chuoni St. Olaf, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii.

Kwa kushauriana nami, mwanafunzi alijitungia kozi juu ya "The Living and the Dead: Folklore and Tragedy." Tulikubaliana kusoma Agamemnon (Aeschylus), Beowulf (translated by Seamus Heaney), Inferno (Dante Alighieri), Hamlet (William Shakespeare), Othello (William Shakespeare), Love in the Time of Cholera (Gabriel Marcia Marquez), na As I Lay Dying (William Faulkner). Tumeshasoma Beowulf, na sasa tuna soma Hamlet.Napenda kusema neno kuhusu Hamlet katika mkabala wa kozi yetu hii.
Kwanza napenda kusema kuwa niliwahi kuongelea Hamlet katika blogu hii. Nilifanya hivyo kwa kujikumbusha tamthilia hii maarufu. Lakini sasa tunaisoma tukiwa na lengo la kuihusisha na mada ya kozi "The Living and the Dead: Folklore and Tragedy."

Hamlet ni tamthilia ya tanzia ("tragedy.") Hilo halina utata. Hamlet ana masononeko akikabiliwa na maamuzi magumu kufuatia kifo cha baba take katika mazingira ya kutatanisha. Katika tamthilia hii tunakutana na watu walio hai na pia mzimu wa baba yake Hamlet. Ujumbe wa mzimu ni kuwa aliuawa na mdogo wake, ambaye ni mfalme aliyeko madarakani. Baada ya mauaji hayo, mdogo huyu alimwoa mama yake Hamlet. Kuwepo kwa mzimu kunatupa fursa ya kujionea mfu aliye hai. Katika mazungumzo, wahusika wanaongelea masuala ya kifo na uhusiano wake na uhai. Mama yake anajaribu kumtuliza:

Good Hamlet, cast thy nighted color off,
And let thine eye look like a friend on Denmark.
Do not for ever with thy vailed lids
Seek for thy noble father in the dust.
Thou know't 'tis common, all that lives must die,
Passing through nature to eternity.
                                                       Act 1. Sc II

Hamlet mwenyewe anaonekana akijiuliza iwapo ni bora kuendelea kuishi na kukabiliana na magnum ya maisha au kujiua ili kuyamaliza. Tunamsikia akitafakari suala hilo katika hotuba yake maarufu "To be or not to be" ambayo ni moja kati ya hotuba maarufu kabisa katika tamthilia za Shakespeare:

Ham. To be, or not to be, that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them. To die--to sleep--
No more; and by a sleep to say we end
The heartache, and the thousand natural shocks
That flesh is heir to. 'Tis a consummation
Devoutly to be wished. To die--to sleep.
To sleep--perchance to dream: ay, there's the rub!
For in that sleep of death what dreams may come
When we have shuffled off this mortal coil,
Must give us pause.... 
                                              Act. III. Sc. I

Ninapenda kusema kuwa mwanafunzi wangu na mimi tumeanza vizuri kuiitafakari mada ya "The Living and the Dead.: Folklore and Tragedy." Kila kitabu kina mchango wake katika kuilezea mada hii. Haya tutayadhihirisha kadiri kozi inavyoendelea.

Thursday, March 8, 2018

Nimenunua Vitabu Vipya vya Mashairi

Katika siku chache zilizopita, nimenunua vitabu vipya viwili vya mashairi. Kimoja ni Collected Poems: 1974-2004  cha Rita Dove, ambacho nilikinunua mjini Moscow, Idaho. Kingine ni Diwani ya Tuzo ya Ushairi ya Ibrahim Hussein ambacho nilikinunua mtandaoni Amazon.

Nilipokuwa Moscow katika tamasha la Hemingway, niliingia katika duka la Book People of Moscow. Niliangalia, nikaona kitabu hiki Collected Poems, ambacho sikukifahamu kabla. Nilivutiwa kwa sababu nilifahamu habari za Rita Dove, kwamba ni mshairi maarufu sana, aliyepata tuzo kadhaa ikiwemo tuzo ya Pulitzer.

Zaidi ni kuwa niliwahi kusoma insha yake "Either I'm Nobody, or I'm a Nation," ambayo ni uchambuzi wa mashairi ya Derek Walcott. Nilikuwa ninafundisha tungo za Walcott, nikaitafuta makala hii na niliona ilivyojaa tafakari na ilivyoandikwa kwa ustadi. Makala hii ilinithibitishia kuwa Rita Dove ana akili sana. Hii ikawa sababu kubwa ya mimi kununua Collected Poems.

Diwani ya Tuzo ya Ushairi ya Ibrahim Hussein niliinunua baada ya kuiona imetajwa mtandaoni Amazon. Nilikuwa sifahamu kuwepo kwake, lakini kwa jinsi ninavyomwenzi Ebrahim Hussen ambaye nilimfahamu tulipokuwa wote katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, yeye akiwa mhadhiri wakati ninasoma, na hatimaye tukawa tunafundisha wote, niliona ninunue kitabu hiki. Mimi mwenyewe nimechapisha makala juu ya tungo za Ebrahim Hussein katika Encyclopedia of African Literature iliyohaririwa na profesa Simon Gikandi.

Nimeanza kuyasoma mashairi yaliyomo katika vitabu vyote viwili. Tayari nimeona kuwa Rita Dove anaandika kwa nidhamu ya hali ya juu, ya kutumia maneno yanayohitajika tu, na anatupeleka sehemu mbali mbali za dunia, tangu enzi za kale hadi leo, kama anavyofanya Derek Walcott katika tungo zake, iwe ni mashairi au tamthilia. Diwani ina washairi wengi chipukizi. Ni fursa yao kuonekana kwa wasomaji.

Tuesday, March 6, 2018

Mdau wa Kitabu Amekuja Tena

Hapa pichani ninaonekana na De'Vonna, mmoja wa waandaaji wa maonesho ya waandishi yaliyoitwa Minnesota Black Authors Expo, ambayo niliyaelezea katika blogu hii. Anaonekana ameshika kitabu changu, Africans and American:Embracing Cultural Differences. Picha tulipiga wakati wa maonesho. Amenilitea ujumbe kuwa anahitaji nakala nyingine ya hiki kitabu.

Kwa kuzingatia jinsi mama huyu alivyo na ushawishi katika jimbo hili la Minnesota, hasa miongoni mwa wenzake wa-Marekani Weusi, nimeguswa na ujumbe wake kwa namna ya pekee. Tangu nilipoandika kitabu hiki, nilikuwa na dukuduku ya kujua wa-Marekani Weusi watakuwa na maoni gani kuhusu yale ninayosema juu ya mahusiano yao na sisi wa-Afrika. Nilielezea dukuduku hiyo katika blogu ya ki-Ingereza.

Kama inavyoeleweka, mahusiano hayo yanawatatiza baadhi ya watu. Kwa hivyo ninapopata mrejesho kutoka kwa hao wenzetu, ninauchukulia kwa uzito wa pekee. Nimefarijika na kufurahi kwamba De'Vonna anataka nakala nyingine ya kitabu changu. Sijui anakipeleka wapi, au atakitumia vipi, lakini hii si hoja.

Tuesday, February 27, 2018

Freeman Mbowe: Kiongozi wa Mfano

Kwa miezi kadhaa nimekuwa nikiwazia kuandika ujumbe kuelezea kuwa ninamkubali Freeman Mbowe kuwa ndiye kiongozi wa kitaifa wa kupigiwa mfano. Nina sababu zangu, ambazo nitazieleza hapa.
Kabla sijafanya hivyo, nataka nifafanue kuwa mimi si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Baadhi ya watu wamekuwa wakinibambikiza uanachama wa CHADEMA. Ukweli ni kwamba sijawahi kukanyaga katika ofisi yoyote ya CHADEMA, wala sijawahi kuiona hata kadi ya CHADEMA, isipokuwa katika picha mitandaoni. Sijawahi kuhudhuria mkutano wa CHADEMA. 
Watu hao wanaonibambikiza chama sijui akili yao ikoje. Mimi ni mtu huru ninayetambua na kutumia haki yangu ya kutoa maoni na kujieleza kuhusu masuala yoyote, yakiwemo ya siasa. Nikisema jambo kuikosoa CCM, kwa mfano, sifanyi hivyo kwa sababu ya kuwa katika chama tofauti. Akili yangu haihitaji chama ili iweze kufikiri.
Baada ya ufafanuzi huo, napenda kurejea kwenye mada. Kwa nini ninamwenzi Freeman Mbowe kama kiongozi wa kupigiwa mfano? Si suala la mihemko au ushabiki. Ni suala la hoja.
Leo, katika taaluma ya saikolojia, tunaambiwa kuwa kuna aina nyingi za akili. Suala hilo kitaaluma linaongelewa chini ya kichwa cha "multiple intelligence" au "multiple intelligences."
Kufuatana na ufuatiliaji wangu wa mada hiyo, nimejifunza kwamba uongozi unahitaji aina ya akili iitwayo "emotional intelligence." Labda kwa ki-Swahili niseme akili hisia. Kwa maneno mengine, mtu mwenye akili hiyo ndiye anaumudu uongozi. Anakuwa kiongozi wa kweli.
Mtu huyo anakuwa mwenye kujitambua. Anatambua hisia zake na hisia za wengine. Kutokana na hilo, anazimudu hisia zake na hisia za wengine, kwa maana kwamba anajitawala vizuri, na anajali hisia za wenzake. Hana mihemko. Anakuwa msikivu. Watu wakitofautiana, yeye anakuwa msuluhishi. Anajenga umoja na maelewano. Anavutia watu. Watu wa kila aina wanamkubali kama kiongozi.
Mtu huyu anajiamini. Wale anaowaongoza wanakuwa huru kung'ara katika maeneo ya ujuzi wao. Yeye hawi mtu wa kutaka sifa, aonekane yeye ndio zaidi. Wenzake waking'ara kumzidi, kwake ni sawa. Vipaji vya kila moja anaviona ni mtaji wa manufaa kwa wote. Anachofanya si kuzuia vipaji hivyo visijitokeze, bali anaviratibisha kwa manufaa ya wote. Hii kwa ki-Ingereza huitwa "leveraging."
Nikirejea kwa Freeman Mbowe, ninaona anakidhi vigezo hivyo. Kuna watu wanambeza Mbowe, eti hana elimu ya kutosha. Wengine wanasema huyu ni DJ. Watu hao ni wajinga, kwa namna mbili. Kwanza hawaelewi kuwa elimu si ya shuleni na vyuoni tu. Inapatikana pia nje ya shule na vyuo. Pili hawaelewi hiyo dhana "emotional intelligence" kama kigezo na msingi wa uongozi.
Wangejua, wasingeshangaa kwa nini huyu Mbowe wanayemsema hana elimu ya kutosha, lakini ndiye kiongozi wa maprofesa, wanasheria maarufu, na kadhalika. Ni kwa sababu yeye hatingishiki na kung'ara kwa hao wenye kisomo zaidi yake. Hatingishiki na umaarufu wa wenzake, akina Tundu Lissu, Msigwa, Lema, au Halima Mdee. Wote wako naye, naye yuko nao. Hiyo ndio tabia ya mtu anayejiamini.
Kutokan na akili yake hiyo na busara zitokanazo, Mbowe amefanikiwa kuijenga CHADEMA mwaka hadi mwaka, hadi leo imekuwa ni chama kikuu cha upinzani, chenye kuongoza majimbo na miji mikubwa. Ingekuwa kuna fursa na uhuru sawa kwa kila chama kufanya shughuli zake kama inavyoelekezwa na katiba na sheria, nina hakika CHADEMA ingekuwa mbali zaidi.
Jambo jingine la muhimu sana linalonivutia kwa Freeman Mbowe ni uzalendo wake. Hata pamoja na magumu yote ambayo chama chake kinawekewa na utawala, daima anaongelea mustakabali wa Taifa. Hata mimi ambaye si mwana CHADEMA ninaguswa na hilo, kwamba anatuwazia wa-Tanzania, na nchi yetu sote, si wana CHADEMA pekee. Huyu ndiye Mbowe ninayemwona mimi.
Nimesema kuwa mimi si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Ila napenda kusema kuwa kutokana na kwamba mimi ni mwanataaluma na mwalimu, kama ingekuwa ni lazima kuwa na chama, ningekuwa CHADEMA. Ninaona jinsi CHADEMA inavyopigania uhuru na haki zilizomo katika katiba, ikiwemo uhuru na haki ya kutoa mawazo na kujieleza, na uhuru wa mikutano. 
Uhuru wa fikra ni msingi wa kustawi yale ninayofanya kama mwanataaluma na mwalimu. Elimu haistawi bila uhuru wa kutoa mawazo na kujieleza. Elimu inaihusu jamii nzima. Mikutano ni sehemu ya hiyo elimu ya jamii. Kwa hivyo, ni wazi kwangu kuwa kama ingekuwa lazima kuwemo katika chama, ningekuwa CHADEMA. Ningekuwa huko si kwa sababu CHADEMA inakidhi mategemeo yangu yote kuhusu masuala yote ya kitaifa, bali kwa sababu hii moja ambayo nimeelezea. Kama mwanataaluma ninayehitaji uhuru wa kufikiri na kutoa mawazo, na ninayetaka elimu ishamiri katika nchi yetu, ningejisikia huru kuwa na kiongozi Freeman Mbowe.

Wednesday, February 21, 2018

Maana ya Uzalendo

Kwa kuzingatia jinsi dhana ya uzalendo inavyovurugwa na watu mbali mbali, nimeona nilete tamko la Ilhan Omar, Msomali Mmarekani ambaye ameweka historia hapa Marekani kwa kuchaguliwa kuwa mwakilishi katika bunge la jimbo la Minnesota. Anafafanua kwa lugha rahisi maana ya uzalendo. Anachosema ni kuwa uzalendo si kutetea uongozi au kiongozi wa nchi, bali ni kutetea na kuzingatia maslahi ya nchi, katiba yake, na watu wake. Anasema ni kosa kufikiri kwamba mkuu wa nchi asikosolewe. Anasema kwamba katika nchi ya kidemokrasia, na katiba inayotambua uhuru wa watu kutoa mawazo na kujieleza, watu wana haki ya kumkosoa mkuu wa nchi, kumshinikiza afanye mambo ya manufaa, na kumwajibisha, bila wasi wasi au woga wa kueleweka kwamba si wazalendo.

Saturday, February 17, 2018

Ripoti ya Mhadhara wa Red Wing

Nashukuru nimeweza kwenda leo Red Wing na kutoa mhadhara juu ya "African Storytelling," kama ilivyotangazwa. Barabara zilikuwa na theluji, kwa hivyo ilibidi niendeshe gari kwa uangalifu. Lakini nilifika salama, saa tatu na dakika hamsini. Mhadhara ulipangiwa kuanza saa nne, na ndivyo ilivyokuwa.

Nilipokelewa vizuri na wahudumu wa maktaba ya Red Wing, hasa Lindsey Rindo ambaye ndiye aliyefanya mawasiliano nami tangu mwanzo, mwaka jana, kuniulizia kama ningeweza kwenda kutoa mhadhara, akafuatilia na kufanya mipango yote hadi kufanikisha shughuli ya leo.

Walikuwepo watu wa kila rika, kuanzia watoto wadogo hadi wazee. Nilianza kwa kuelezea umuhimu wa Afrika kama chimbuko la binadamu, tekinolojia, lugha, na usimuliaji wa hadithi. Nilielezea jinsi falsafa na maadili yalivyohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi hadi kizazi katika aina za fasihi simulizi kama vile methali. Nilitoa mifano ya methali.

Kisha nilisimulia hadithi ya "Spider and the Calabash of Knowledge," na "The Lion's Advice," kutoka katika kitabu cha West African Folktales cha Jack Berry, na hadithi ya "The Chief's Daughter," kutoka katika kitabu cha West African Folktales cha Steven H. Gale. Hizo hadithi mbili za mwanzo sikuzifahamu hadi jana. Ndipo nilizisoma, nikaamua kwenda kuzisimulia leo. Hiyo ya tatu niliifahamu, na niliwahi kuisimulia.

Dakika kumi za mwisho zilikuwa za masuali na majibu. Kwa tathmini yangu, mhadhara wa leo umekuwa moja wa mihadhara bora ambayo nimewahi kutoa. Nilivutiwa kuona wazazi wamekuja na watoto wao. Inapendeza kuona jinsi watoto wadogo wa Marekani wanavyozoeshwa kutumia muda maktabani.

Lindsey alikuwa ameniambia kuwa nilete vitabu vyangu, nikitaka, kwa ajili ya kuuza, nami nilifanya hivyo. Nilichukua nakala za kutosha za Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wakati wa kunua na kusainiwa vitabu, niliguswa kumwona mama moja alivyokuwa na ari ya kununua kitabu cha "Africans and Americans." aliniambia kuwa ni mfanya usafi katika maktaba hiyo. Kwa hapa Marekni, ni jambo la kawaida watu wa aina zote kupenda vitabu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...