
Nilisikia juu ya Popol Vuh kwa mara ya kwanza mnamo mwaka 1982 kutoka kwa Profesa Harold Scheub, nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu Cha Wisconsin-Madison. Hata hivi hatukusoma kitabu hiki. Sasa nimefurahi kuwa katika darasa langu tumefanikiwa kukisoma na kukijadili, ingawa mambo yake mengi si rahisi kueleweka kwetu watu wa leo, wa tamaduni tofauti kabisa na ule utamaduni wa wa-Maya wa zamani.
Popol Vuh ni masimulizi kuhusu mambo mengi yahusuyo jinsi dunia ilivyoumbwa, na matukio mbali mbali yaliyofuatia, yakiwahusisha miungu na mashujaa wa aina aina. Ni masimulizi yenye uzito, kwani yanabeba mambo ya imani, maadili, utabiri na falsafa. Baadhi ya masimulizi ya Popol Vuh yanatukumbusha masimulizi ya vitabu vya dini kama Biblia au Quran, na pia masimulizi mengine kama Gilgamesh, au hata masimulizi maarufu ya wa-Kerewe, alivyoyaandika Mzee Kitereza katika kitabu chake cha Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka na Ntulanalwo na Buliwhali.
Kusoma vitabu vya aina hii ni jambo jema sana, kwani linatupa mwanga kuhusu hali halisi ya yale waliyopitia na kuwazia wanadamu sehemu mbali mbali za dunia.
No comments:
Post a Comment