Tuesday, November 9, 2010

Mdahalo wa Dr. Slaa, ITV, Utumike Mashuleni

Mimi ni mwalimu, mwenye uzoefu wa kufundisha tangu mwaka 1976, nilipoanza kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na hatimaye kutoa mihadhara katika vyuo vikuu sehemu mbali mbali duniani.

Kutokana na wadhifa wangu, napenda kusema kuwa ingekuwa bora iwapo mdahalo wa Dr. Slaa ITV ungesambazwa mashuleni, kwani una mambo muhimu ya kuwafundisha vijana wetu. Jambo la kwanza ni kuwa mdahalo ule unatoa changamoto kuhusu masuala ya nchi yetu, ni kichocheo cha fikra.

Jambo la pili ni kuwa vijana wetu wakiona jinsi Dr. Slaa anavyoyakabili masuali, kwa ufasaha, ufahamu, na kujiamini, wataona mfano wa kuiga na kigezo cha kujipima. Wataelewa kuwa wana wajibu wa kujielimisha sana.

Wengi tunafahamu jinsi kiwango cha elimu kilivyoporomoka nchini, kiasi kwamba hata kwenye mahojiano ya kutafuta ajira, wa-Tanzania wanapata taabu. Kwa mfano, taarifa zimezagaa kuwa wa-Tanzania wanaogopa kushindana na wa-Kenya.

Sisi miaka tulipokuwa tunasoma hatukuwa tunawaogopa wa-Kenya, wala wa-Ganda, wala wengine wowote. Tulisoma nao pale Chuo Kikuu Dar es Salaam, bila kuwaogopa kwa lolote. Kwa hali hii, ni muhimu vijana wetu wapewe kila aina ya msaada na changamoto ya kuwajengea mwamko mpya. Mdahalo wa Dr. Slaa una mchango kwa upande huo.

Vile vile, mdahalo huu wa Dr. Slaa unatoa mfano mzuri wa uwajibikaji katika kuitumia lugha ya ki-Swahili. Haipendezi kuona wale tunaowaita viongozi, kama vile wabunge, mawaziri, na wakurugenzi, wakishindwa kukitumia ki-Swahili ipasavyo, na badala yake wanachanganya lugha. Hii ni dalili ya kutoelimika vizuri, na kutoiheshimu lugha yetu ya ki-Swahili.

Nafahamu kuwa wa-Tanzania wengine wakisoma ujumbe kama huu wangu, watarukia mambo ya ushabiki wa vyama vya siasa. Mimi ni raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Kwa wadhifa wangu kama mwalimu, naangalia maslahi ya vijana wetu kielimu.

Wanaopenda kudhania kuwa mtu akitoa maoni kama yangu basi anahusika na chama fulani cha siasa nawaomba waelewe kuwa msimamo wangu kama mtu asiye mwanachama wa chama cha siasa ni kuwa mifumo ya siasa tunayoifuata Tanzania ni ya kikoloni mambo leo. Haijalishi kama ni chama kimoja au vyama vingi. Haitajenga demokrasia. Nimeelezea hayo katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

1 comment:

Masangu Matondo Nzuzullima (MMN) said...

Hili halitawezekana, na nadhani sababu ni wazi. Waliokimbia midahalo hawatakubali!

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...