Monday, February 14, 2011

Mwanafunzi Wangu Kaniacha Hoi

Leo kaja ofisini mwanafunzi wangu ambaye amerejea siku chache zilizopita kutoka Tanzania, ambako alikuwa ameenda kujifunza masuala ya huduma za hospitali. Alikuwepo kule kwa mwezi moja.

Kabla ya kwenda Tanzania, alikuwa amechukua somo langu moja. Halafu, alipokuwa anaandaa safari ya Tanzania, tulikutana nikamweleza yale ninayowaelezea wa-Marekani kabla hawajaenda Afrika, kuhusu hali ya Tanzania, na hasa kuhusu tofauti za tamaduni kama nilivyozielezea katika kitabu cha Africans and Americans.

Alivyokuwa Tanzania, alikuwa akiangalia shughuli za madaktari katika hospitali moja mkoa wa Arusha. Kutokana na lengo lake la kuwa daktari, amejifunza mengi. Siku za mapumziko alisafiri hadi Dar es Salaam na Zanzibar, hifadhi za Ngorongoro, Serengeti na Lake Manyara. Pia alipanda Mlima Kilimanjaro.

Tulipomaliza maongezi, alinipa picha, bila mimi kutegemea, aliyopiga akiwa kileleni Mlima Kilimanjaro. Nimeguswa sana na zawadi hii. Raha moja kubwa ya ualimu ni kugusa mioyo, akili, na maisha ya wanafunzi. Nimevutiwa na ubunifu wa mwanafunzi huyu. Sikutegemea kuona jina langu linapepea juu ya Mlima Kilimanjaro. Labda ni changamoto, nijikongoje ili nami siku moja nikafike pale.

11 comments:

Christian Sikapundwa said...

Hongera Profesa,kuwa na mwanafunzi mahili na mbunifu wa hali ya juu kiasi hicho.

Christian Sikapundwa said...

Si kitu cha ajabu,kwa professional ya ualimu kupata kitu kama hicho,mie pia imenigusa sana kwani kisa kama hicho kilinikuta mwaka 1990 nikiwa Mjini Arusha ni kiwa mgeni kabisa.

Nikasikia mtu akiniita wenzangu walinishagaa,kuona mtu ananifahamu,kumbe alikuwa mwalimu ambaye nilimfundisha chuo cha ualimu Songea Matogoro Songea amabeye alipangwa wilaya ya Ngorongoro.

Nina maana mwalimu ni mtu wa pekee kabisa katika jamii,isitoshe ni wito,mtu anafanya kazi ambayo haina kipato cha maana ukilinganisha na kazi anayoifanya.Hongera sana kwa kazi yako inayoonekana kitaifa na kimataifa.

Masangu Matondo Nzuzullima (MMN) said...

Japo si kazi ya kutajirikia, ualimu ni kazi mojawapo ambayo inaleta ridhiko la kweli kwa waifanyayo kwa moyo.

Fikiria huyu mwanafunzi. Mbali na misukosuko na mahangaiko yote ya kupanda Mlima Kilimanjaro bado alikuwa amefumbata upendo na kumbukumbu ya Mwalimu wake moyoni.

Inafurahisha na kutia moyo sana. Hongera mwalimu kwa jina lako kupepea katika mlima Kilimanjaro kwa njia ya aina yake na ya kuheshimika sana. Mimi napendekeza picha hii iwe hapo juu kwenye blogu iwe inatukaribisha!!!

Mbele said...

Mwalimu Sikapundwa na Mwalimu Matondo, shukrani kwa mchango wenu. Sina cha kuongeza, maana nakubaliana nanyi kabisa. Wazo la kuiweka hii picha mahali pa wazi katika blogu hii ni wazo murua. Sina ujuzi sana wa tekinolojia hizi za mtandao, lakini kuna watu hapa nilipo nitawaulizia.

Inafurahisha kwa walimu kukaa na kuongelea masuala yetu namna hiyo. Kitu kimoja kinachokera ni kuwa wako watu wengi katika jamii yetu wanaodhani kuwa kila mtu anahangaika na pesa. Wanasahau kuwa walimu ni wito, na wale walimu wanaovunja maadili haya na kufanya ualimu kama biashara wanatuaibisha sisi wengine. Kadhalika wanaofanya ufisadi kwa kutumia wadhifa wa ualimu.

Upepo Mwanana said...

Hata na mimi imenigusa. Inaonekana huyo mwanafunzi alithamini sana mchango wako katika kumueleza uhalisia wa Tanzania, labda ilikuwa ni kinyume kabisa na alivyokuwa anafikiri kabla ya kwenda Tanzania

Mbele said...

Dada Upepo Mwanana, kwanza shukrani kwa kutembelea hiki kijiwe changu. Hao wanafunzi wangu wanavutiwa na yale ninayowaambia kuhusu Tanzania. Hata leo asubuhi, mwanafunzi mwingine ambaye yuko darasani kwangu ameniandikia barua pepe akisema kuwa katika darasa lake la Uchumi, wameambiwa wachague nchi ya kuitafiti na kuandika habari zake kwa muhula huu wote. Naye amesema amevutiwa na yale ninayosema kuhusu Tanzania, na kwa hivi amechagua Tanzania.

Katika hiki chuo ninapofundisha, kuna msisitizo wa kuwafanya wanafunzi waifahamu dunia kwa ujumla, na ni chuo kinachosifika kwa kuwa asilimia zaidi ya 70 ya wanafunzi wanaenda nchi za nje kusoma kwa muda fulani, kama vile mwezi, miezi sita, au mwaka. Kwa hivi, kuna huo msisimko katika fikra za watu hapa chuoni.

Cha zaidi ni kuwa tuko waTanzania kadhaa katika vyuo vya Marekani ambao tunajihusisha na kuandaa na kupeleka wanafunzi Tanzania. Kila mwaka tunapeleka wanafunzi wengi sana, ambao utawakuta sehemu kama Zanzibar, Bagamoyo, Arusha, Moshi, Tanga, na vyuoni kama Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Ni kazi ya kujitolea, yenye manufaa makubwa kwa hao wanafunzi kielimu, na manufaa makubwa kwa nchi yetu kwa upande wa pato la fedha za kigeni, na kwa ujumla katika kujenga maelewano baina ya waTanzania na waMarekani.

Wakati nchi yetu inapotangaza idadi ya watalii wanaoingia nchini, huwa haielezwi kuwa mamia ya hao "watalii" ni wanafunzi.

Narudia kushukuru kwa kutembelea kijiwe changu, na kwa changamoto yako.

Sophie B. said...

Hongera Prof. yaani hapa ndipo Mswahili hakukosea aliposema tenda wema uende zako.Huyo mwanafunzi wako naamini mwongozo wako umemsaidia sana akaona hiyo ndiyo zawadi unayostahili ama kweli ni zawadi kwelikweli ambayo siku zote itakudhihirishia kazi nzuri unayoifanya.

Simon Kitururu said...

Hili bonge la zawadi Prof. Mbele!Na ni zaidi ya pesa!

Unknown said...

Hii ni zawadi ya thamani sana, hongera Prof.Mbele

Emmanuel said...

Hongera sana Prof Mbelle. Katika zawadi zote ulizowahi kupewa nadhani hii ina maana sana. Sina maana ya kudharau mengine maana ni makubwa zaidi. Lakini huyu mwanafunzi kakupenda sana kutokana na yale uliyomwelezea kuhusu Tanzania na Africa na ujumla. Ndio maana kaamua kupanda na jina lako juu ya mlima wetu. Huu ni mchango mkubwa kwa Tanzania umeutoa. Mungu akubariki. Mungu aibariki Tanzania

Mbele said...

Wadau asanteni kwa maoni yenu. Ni kweli hii ni zawadi kubwa kuliko maelezo na haisahauliki.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...