Friday, November 4, 2011

Nakunywa Chai na Kahawa ya Tanzania

Ujumbe wangu wa leo ni kuwa wa-Tanzania tunapaswa kutumia bidhaa zinazotengezwa nchini mwetu kila inapowezekana. Iwe tuko Tanzania au nje, tufanye hivyo, kwani manufaa yake ni makubwa.

Nimepata wazo la kuandika ujumbe huu kutokana na ukweli kwamba hapa ughaibuni ninakunywa chai na kahawa ya Tanzania. Sibadili.

Kila ninapokuwa Tanzania, wakati wa kuondoka nahakikisha kuwa nimenunua chai na kahawa ya kunitosha hadi nitakapokuja tena. Mwaka huu, kwa mfano, wakati naenda kupanda ndege uwanja wa Julius Nyerere Dar es Salaam, nilimwambia dreva wa teksi anipeleke kwanza sehemu wanapouza chai na kahawa ya Tanzania. Ndivyo alivyofanya




Faida za kutumia bidhaa za nchini mwetu ni nyingi. Kwanza, tunachangia ajira katika nchi yetu. Kama wa-Tanzania wote, walioko nchini na nje, tungekuwa tunanunua vitu vinavyotengenezwa nchini, kama vile nguo, sabuni, sukari, soda, na viberiti, ajira zingeongezeka mara dufu. Waziri wa mambo ya nchi za nje hivi karibuni aliripotiwa akisema kuwa kuna waTanzania zaidi ya milioni mbili katika nchi za nje. Ni wazi kuwa hili ni soko kubwa sana kwa bidhaa za Tanzania, lakini tumekosa upeo wa kujitambua.


Wa-Tanzania wengi, ndani na nje ya nchi, tuna tatizo la kasumba na elimu duni. Tunashabikia vitu vya nje, hata bila sababu ya maana. Ukiwa Dar es Salaam, nenda mahali kama Mlimani City, kwa mfano. Hapo utawaona wa-Tanzania wakihangaika kununua juisi ya vikopo kutoka nje ya nchi, wakati maeneo ya jirani, kama vile Mwenge, yanauzwa mananasi, machungwa, mapapai na maembe.




Wa-Tanzania wanashabikia vitu vinavyoitwa vya mamtoni, bila kutambua kuwa kwa kufanya hivyo, wanawapa ajira watu wa nchi za nje. Tukiorodhesha vitu hivi vinavyotoka nje, wakati sio lazima tuviagize, tutaona jinsi tunavyochangia ukosefu wa ajira katika nchi yetu. Sina nafasi ya kuelezea kirefu suala hili hapa. Nimelielezea katika kitabu cha CHANGAMOTO.




Nina hakika kuwa kwa kununua vikopo na vikasha vya chai na kahawa vinavyoonekana kwenye hizi picha, nimechangia uchumi wa Tanzania, na ajira kwa wa-Tanzania kadhaa.

2 comments:

Anonymous said...

Africafe?!? Mbinga Cafe hupendi au nini?

Mbele said...

Hii ya Mbinga nilinunua mwaka jana nikaja nayo hapa ughaibuni. Iliisha. Sasa mwaka huu, nilipokuwa Dar, sikufanikiwa kuipata kwenye hilo duka, na nilikuwa na haraka ya kwenda uwanja wa ndege. Lakini ni muhimu kuisaka hii ya Mbinga mwaka ujao.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...