Wednesday, July 4, 2012

Tanga, Mji wa Baiskeli Nyingi

Kitu kimoja kilichovuta hisia yangu, tangu nilipofika Tanga mara ya kwanza, miaka yapata kumi iliyopita, ni jinsi watu wengi wanavyotembelea baiskeli. Mji huu una baiskeli nyingi sana. Hali ni hiyo hadi sasa.

Jambo moja linalonishangaza ni jinsi baiskeli nyingi zinavyopita mitaani usiku bila taa. Sijui watu wa hapa wanawezaje kuimudu hali hiyo, bila wasi wasi. Wanaume kwa wanawake wanatembelea baiskeli mjini hapa.  Jana, tukiwa kwenye Barabara ya Nne, nilimwona mama mmoja amevaa ile aina ya hijab ambayo inafunika hadi uso, kasoro macho. Alikuwa akipita mtaani akiwa amepanda baiskeli.

Hali hiyo ya mji wa Tanga kuwa ni mji wa baiskeli inanipa mawazo kadhaa. Kwanza, kupanda baiskeli namna hiyo, badala ya magari, ni mazoezi bora kwa mwili na afya. Pili, kutumia baiskeli ni jambo jema kwa mazingira, tofauti na utitiri wa magari ambao huchafua hewa ya miji kama Dar es Salaam.

Huu utumiaji wa baiskeli kiasi hicho unanikumbusha mji wa Lamu, kule Kenya. Kule watu wengi hutumia usafiri wa punda. Sijawahi kuona mji wenye punda wengi kama Lamu, na ni usafiri ambao nadiriki kusema una mantiki nzuri kuliko utitiri wa magari kama ilivyo Dar es Salaam.

1 comment:

Anonymous said...

Ni Kweli Punda wengi Lamu, ila Kumbuka Mwalimu alisema Dar-es-salaam Punda wengi watolewe sasa wamekuja waendesha mikokoteni badala ya Magari ya Punda.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...