Saturday, August 3, 2013

Tundu Lissu: Pigeni Kelele Kuokoa Watanzania

Lissu: Pigeni kelele kuokoa Watanzania
Penulis : mtandao-net on Saturday, August 3, 2013 | 10:09 PM

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimeutaka umoja wa vijana wa Vyama vya Kidemokrasia Duniani (IYDU) kupiga kelele kote duniani ili kuwanusuru Watanzania wanaouawa hovyo kwa sababu za tofauti za siasa hapa nchini.

Akizungumza na uongozi wa umoja huo (IYDU) jijini Dar es Salaam wiki hii, Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni Tundu Lissu alisema ni wakati wa vijana kuwaokoa wenzao wa Tanzania ambao kujiunga kwao na siasa kumesababisha wachukiwe na watawala.

“Watu wanauawa hadharani na hakuna hatua zinazochukuliwa…nendeni katika nchi zenu katika mabunge yenu mkapige kelele katika haya yanayotokea Tanzania; inaweza kusaidia na mkawa mmewasaidia Watanzania,” alisema Lissu. Tundu Lissu alisema viongozi wengi wamekamatwa na kufunguliwa kesi nyingi mahakamani, na hivyo kuifanya CHADEMA kuwa katika wakati mgumu kuliko mwingine wowote katika uendeshaji wa siasa za vyama vingi hapa nchini.

Chama hicho kimedai kuwa hali ya kisiasa hususan kwao na baadhi ya wapinzani nchini ni ngumu, kutokana na ukandamizaji mkubwa unaofanywa na serikali kwa kutumia vyombo vya dola.

Lissu alisema viongozi wa upinzani wamefunguliwa kesi za ugaidi kwa lengo la kuwafanya watumie muda mwingi katika kesi hizo, badala ya kuishughulikia serikali pale inaposhindwa kutimiza wajibu wake.

Mbali na kesi hizo, kumekuwa na matukio ya kikatili ya kuteka, kutesa na hata mauaji dhidi ya watu wanaoshabikia upinzani na wale wanaoikosoa serikali katika mambo ya msingi na yenye maslahi ya nchi.

Lissu amesema wabunge wa CHADEMA licha ya uchache wao, wakiwemo baadhi wa vyama vingine vya upinzani, wamejitahidi kupambana bila woga bungeni kutetea wananchi lakini wamekuwa wakizidiwa na wingi wa wenzao wa CCM, ambao wamekuwa wakipitisha maamuzi mengi ya hovyo na yasiyo na manufaa kwa nchi.

Mapema akiwaaga vijana hao, Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe, amewataka vijana kutokata tamaa kutokana na mambo yanayotokea nchini.

Mbowe alisema CHADEMA haitarudi nyuma katika harakati za kutwaa madaraka ya dola hata kama watawala waliopo madarakani hawapendelei nafasi zao kuwaponyoka.

“Tunafahamu katika siasa kuna magumu mengi lakini niwahakikishieni kuwa ninyi mna nafasi kubwa ya kuleta mageuzi sehemu yoyote kama mtakuwa na dhamira na kuvishinda vitisho mbali mbali dhidi yenu,” alisema Mbowe.

Katika ziara yao hapa nchini vijana hao wa IYDU walitembelea ofisi mbali mbali ikiwamo Wizara ya Mambo ya Nje na ubalozi wa nchi za Ulaya nchini (EU).

Mkurugenzi wa masuala ya Mashariki ya Mbali, Wizara ya Mambo ya Nje, Balozi Simba Yahya, alikiri kuwa watumishi wa umma wanashindwa kutofautisha utendaji wa serikali na chama kilichoko madarakani.

“Itachukua muda kwa wafanyakazi kutenganisha hali hii….. kiuhalisi wanatakiwa wawe watendaji kwani wapinzani wa leo wa serikali ndio wanaweza kuwa mabosi wao wa kesho,” alisema Yahya.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...