Wednesday, December 23, 2015

Ninajivunia Binti Huyu: Bukola Oriola

Nimefurahi kupata taarifa kuwa Rais Obama amemteua Bukola Oriola, kuwa mjumbe katika tume ya kumshauri kuhusu masuala ya usafirishwaji wa ghilba na utumikishwaji wa binadamu, kama ilivyotangazwa katika taarifa hii. Bukola ni binti kutoka Nigeria anayeishi hapa Minnesota, Marekani. Nimemfahamu tangu mwaka 2009, kwa kusoma taarifa zake katika magazeti ya wa-Afrika hapa Minnesota.

Niliguswa kwa namna ya pekee niliposoma kauli yake kuwa alikuwa ameandika mswada wa kitabu bali hakujua auchapishe vipi. Kwa kuwa nilikuwa na uzoefu wa kujichapishia vitabu, dhamiri yangu ilinisukuma niwasiliane naye ili nimsaidie. Nilielezea kisa hicho katika blogu hii.

Baada ya kitabu chake, Imprisoned: The Travails of a Trafficked Victim kuchapishwa, niliendelea kumhamasisha. Kwa mfano, nilimwalika kwenye tamasha la vitabu mjini Minneapolis tarehe 10 Oktoba, 2009, ambalo nilikuwa nashiriki. Nilitaka yeye kama mwandishi chipukizi aone na kujifunza kazi inayomngoja mwandishi baada ya kuchapisha kitabu. Alikuja, tukapiga picha inayoonekana hapa kushoto tukiwa kwenye meza yangu.

Kitabu kilimfungulia milango. Alikuwa anazunguka sehemu mbali mbali kutoa mihadhara kuhusu utumwa na mateso wanayopata wanawake wanaorubuniwa, kutoroshwa, kutekwa, na kisha kutumikishwa na kunyanyaswa. Alianzisha kipindi cha televisheni na pia taasisi aliyoiita The Enitan Story. Yote hayo ni kwa ajili ya kuwasaidia waathirika na kuielimisha jamii kuhusu tatizo hili ambalo limeota mizizi duniani.

Ninafurahi kwa mafanikio ya binti huyu. Naye, kwa kukumbuka nilivyomsaidia, aliandika ifuatavyo katika utangulizi wa kitabu chake:

     I would also like to thank those who worked with me to get this book published. My profound gratitude goes to Prof. Joseph Mbele of St. Olaf College, Northfield, Minnesota, who showed me how to get my book published, otherwise it would have been another Word Document on my computer. It would have not been able to give the message of hope to the hopeless. God bless you sir.

Kitendo cha Rais Obama kumteua Bukola kwenye tume hiyo ni heshima kubwa kwake. Hapa Minnesota na Marekani kwa ujumla watu wamezipokea taarifa hizi kwa furaha. Nchini kwake Nigeria taarifa hii imekuwa kishindo katika vyombo vya habari. Kwa upande wangu, naona fahari kuwa niliitikia wito wa dhamiri yangu nikamwelekeza namna ya kuchapisha kitabu ambacho kilichangia na bado kinachangia mafanikio yake. Mungu ni mkubwa.

Bukola mwenyewe anatambua kuwa kuna mkono wa Mungu katika mambo anayopitia na kuyashuhudia maishani. Anaamini kuwa ana wajibu mbele ya Mungu wa kuwasaidia wanyonge, na kuwa mtetezi wa wanaonyanyaswa na kudhulumiwa. Msikilize anavyojieleza:

1 comment:

Mbele said...

Taarifa za binti huyu zinaendelea kushamiri. Ni nyingi, bali leo nimeona nilete hii hapa. Wakati huu ninapoandika ujumbe huu, Bukola yuko Washington DC kujumuika na wanatume wenzake katika mkutano Ikulu ya Marekani, White House.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...