Sunday, November 5, 2017

Hadithi Zetu za Jadi

Hadithi zetu za jadi ni hazina kubwa ya utamaduni wetu. Kila kabila lilikuwa na hadithi nyingi, pamoja na aina nyingine za fasihi simulizi, kama vile nyimbo, na methali. Hadithi zina tafakari juu ya maisha na tabia za binadamu ingawa mara nyingi wahusika wana taswira za wanyama, ndege au viumbe vingine. Zinaelezea masuala ya familia, malezi ya watoto, wajibu wa wazazi na watoto. Zinatoa tahadhari kuhusu tabia mbaya na maelekezo juu tabia njema. Zinafundisha huruma, maelewano, ushiriano na kusaidiana.

Hadith zinaelezea mahangaiko, mategemeo, mafanikio, ubora na udhaifu wa binadamu, Kuna hadithi za kusisimua hisia na fikra, zenye kuibua masuali kuhusu maana ya maisha, kama walivyoibua wanafalsafa wa mkondo uitwao "existentialism," kama nilivyogusia katika kitabu cha Matengo Folktales.

Kitabu hiki ni mkusanyo wa hadithi kumi za ki-Matengo, ambazo nilizitafsiri kwa ki-Ingereza. Niliandika uchambuzi wa kila hadithi na nikaandika pia insha ya jumla kuhusu hadithi, ili kuwapa wasomaji kianzio cha kuzichambua.

Nilipokuwa ninaandaa kitabu hiki, nilikuwa mhadhiri katika Chuo kikuu cha Dar es Salaam. Somo mojawapo nililokuwa ninafundisha ni "Oral Literature" (fasihi simulizi). Hapakuwa na kitabu cha kufaa kufundishia somo hilo kwa wanafunzi wa chuo kikuu. Hapakuwa na kitabu cha kufundishia hadithi za jadi, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Kwa hivyo, lengo langu lilikuwa ni kuziba pengo, kwa kuandika kitabu ambacho nilitaka kiwepo. Hii ni falsafa ambayo imekaa kichwani mwangu: kama hakuna kitabu ambacho ungetaka kiwepo, andika hicho kitabu. Au kama kitabu unachosoma hakikuridhishi, andika hicho ambacho kitakuridhisha.

Ingawa kitabu changu si kikamilifu, angalau kinakidhi mahitaji yangu ya kufundisha somo la hadith i za jadi kwa wanafunzi wa chuo kikuu. Ni faraja kwangu kuwa si mimi peke yangu mwenye wazo hilo. Kuna wengine ambao wanakitumia kama ilivyokuwa katika chuo kikuu cha Montana na chuo cha St. Benedict/St. John's.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...