Showing posts with label Ajira. Show all posts
Showing posts with label Ajira. Show all posts

Saturday, April 13, 2013

Maonesho ya Elimu na Huduma za Jamii, Brooklyn Park

Leo nimeshiriki maonesho ya elimu na huduma za jamii yaliyoandaliwa na African Career, Education & Resource, Inc (ACER). Maonesho haya yalifanyika katika shule ya Park Center, Brooklyn Park, Minnesota. Wadau wa huduma kama afya, ajira, elimu, na malezi ya vijana, walikuwepo, kutoa elimu na ushauri, na hasa kuifahamisha jamii kuhusu huduma wanazotoa.
Nilipata fursa ya kukutana na watu ambao tunafahamiana, na wengine ambao hatukuwa tunafahamiana.








Huyu dada anayeonekana kwenye picha ya juu kabisa na hapa kushoto alikuwa mwanafunzi wangu hapa Chuoni St. Olaf, miaka 13 iliyopita. Asili yake ni Ethiopia. Ni shabiki mkubwa wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences




Kati ya hao tunaofahamiana, ambao tumekutana leo, ni Dr. Alvine Siaka kutoka Cameroon, ambaye ni mratibu wa African Health Action. Mwingine ni Rita Apaloo, kutoka Liberia, ambaye ni mratibu wa jumuia iitwayo African Women Connect. Rita naye ni shabiki wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences

Kati ya watu ambao tumefahamiana leo ni dada Iqbal Duale, m-Somali, ambaye ni mtaalam wa elimu ya jamii.  Tulielezana shughuli zetu kwa jamii, tukaona zinahusiana. Taasisi anayofanyia kazi inaitwa Planned Parenthood.  Tutawasiliana zaidi, Insh' Allah.

 Kama kawaida, kwenye mikusanyiko kama hii, tulipata fursa ya kubadilishana mawazo. Tuliongelea shughuli tunazofanya, changamoto zake na malengo yake, na umuhimu wake kwa jamii. Kitu kimoja cha kuvutia na kutia moyo ni kuwa pamoja na changamoto zote na magumu, kila moja wetu ana msimamo thabiti kuwa hakuna kulegea, kurudi nyuma, wala kukata tamaa. Changamoto hizi ni kama chachu kwetu.

Taasisi iliyoandaa maonesho ya leo, yaani ACER, niliitaja siku chache zilizopita, katika ujumbe wangu kuhusu mkutano wa bodi ya taasisi ya Afrifest. ACER na Afrifest tumeamua kushirikiana, nami niliamua kuhudhuria maonesho ya leo kama njia ya kujenga uhusiano huo.

Mimi ni mwenyekiti wa bodi ya taasisi ya Afrifest. Papo hapo, nilienda nikiwa nimejisajili kwa jina la kampuni ya Africonexion. Nilikuwa na meza, kama inavyoonekana hapa kushoto, ambapo niliweka vitabu na machapisho yangu mengine, nikapata fursa ya kuongea na wadau waliofika hapo. Wengine wana wadhifa katika taasisi zinazoshughulikia masuala ninayoshughulikia, yaani ya elimu kuhusu tofauti za tamaduni. Uzuri wa kukutana namna hiyo ni kuwa tunajenga msingi wa kushirikiana siku zijazo.

Thursday, June 3, 2010

Umuhimu wa Warsha Zangu

Sijui kama kuna jambo ninaloongelea mara nyingi zaidi katika blogu hii kuliko suala la tofauti za tamaduni duniani, athari zake, na umuhimu wa kuzielewa. Ni suala muhimu sana, hasa katika dunia hii ya utandawazi.

Nimekuwa nikiendesha warsha kuhusu masuala haya huku Marekani, na miaka ya karibuni nimeanza kufanya hivyo Tanzania. Masuala haya yanaendelea kufahamika vizuri katika makampuni, mashirika,taasisi, vyuo na jumuia mbali mbali huku Marekani na sehemu zingine za ughaibuni.

Lakini haya si mambo ya ughaibuni tu, na wala pasiwe na mtu akadhani ni mambo ya ughaibuni tu. Ndio maana naendesha warsha Tanzania. Kama kuna asiyeamini hayo, napenda kuleta tangazo la ajira lilitolewa na World Food Program la Umoja wa Mataifa hapa Tanzania, kama lilivyoripotiwa katika blogu ya Michuzi. Bofya hapa.

Kigezo cha ufahamu wa tamaduni tofauti, ufahamu wa namna ya kushughulika na watu wa tamaduni mbali mbali, kimesisitizwa kama sifa mojawapo ambayo mwomba ajira anatakiwa awe nayo. Watu waliohudhuria warsha zangu wanafahamu kuwa hapo ndipo kwenye msisitizo wa warsha zangu. Warsha zangu hazina mbwembwe wala madoido. Ni darasa, kama inavyoonekana hapa, hapa, na hapa.

Nimefurahi kuona tangazo hili la World Food Program, hasa kwa kuwa zimebaki siku chache tu kabla sijasafiri kuelekea Tanzania, ambako nitaendesha tena warsha. Kitu kimoja kinachotajirisha warsha hizi na kuzipa umuhimu wa pekee ni kuwa washiriki wanachangia uzoefu wao katika kuhusiana na watu wa tamaduni mbali mbali, sehemu zao za kazi au katika shughuli zingine. Hapo najifunza mengi, na natambua umuhimu wake. Warsha yangu ya kwanza ni tarehe 12 Juni, mjini Tanga, kama nilivyoeleza hapa.

Kwa taarifa zaidi, wasiliana nami: info@africonexion.com

Thursday, April 22, 2010

Kenya Yaondoa Vibali vya Kazi

Kuna taarifa kuwa Kenya inaondoa vibali vya kazi kwa raia wa Afrika Mashariki wanaotaka kufanya kazi Kenya. Bofya hapa. Sijui wa-Tanzania wanaipokeaje habari hii, lakini binafsi sishangai, kwani naifahamu Kenya kiasi fulani, na nafahamu kuwa wa-Kenya sio tu wamejiandaa kwa ushindani bali wanajiamini.

Tatizo liko upande wa wa-Tanzania. Kwa miaka mingi sana, labda kuanzia miaka ya themanini na kitu, wa-Tanzania wamekuwa na tabia ya kupuuzia elimu. Shuleni wanatafuta njia za mkato badala ya kusoma sana, ndani na nje ya yale yanafundishwa.

Wakishamaliza shule (ambayo ni dhana ya kipuuzi, kwani shule haimaliziki), wanaona kusoma ni kero. Sijui kuna wa-Tanzania wangapi wanaonunua vitabu na kuvisoma, au wanaoenda maktaba na kujisomea tu, au wana vitabu majumbani na wanavisoma, au wanashirikiana na watoto wao katika kusoma vitabu.

Binafsi, nimeandika kwa miaka mingi nikiwalalamikia wa-Tanzania kwa tabia hizo, na nimeelezea sana nilivyoona tofauti baina ya Tanzania na Kenya, tangu nilipoanza kutembelea Kenya, mwaka 1989.

Nimeelezea mara kwa mara kuwa hata huku ughaibuni, wa-Tanzania hawafanani na wenzetu wa nchi zingine za Afrika. Siwaoni wa-Tanzania kwenye tamasha za vitabu au kwenye maduka ya vitabu. Siwaoni wa-Tanzania wanaomiliki maduka ya vitabu au magazeti. Lakini wenzetu, kama vile wa-Kenya au Wanigeria, wamo katika shughuli hizi.

Watanzania ni wapenda ulabu na starehe, wawe Tanzania au ughaibuni. Hayo nimesema sana kwenye kumbi mbali mbali, na kwenye blogu zangu, na hata kwenye kitabu ambacho nimechapisha mwaka jana, kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii

Sasa basi, katika huu utandawazi, ni wazi wa-Kenya wanajiamini zaidi na hawatishiki kama wanavyotishika wa-Tanzania. Wa-Kenya wamejiandaa zaidi kielimu na wanaweza kujieleza. Watanzania wengi wanawapeleka watoto wao kusoma Kenya, na wa-Kenya wanazidi kuchukua ajira hata nchini Tanzania. Kwa hali ilivyo, wataendelea kuchukua ajira, iwe ni kwao au kwetu, au sehemu nyingine duniani. Wa-Kenya wamejiandaa kiasi kwamba hata fursa za kufundisha ki-Swahili huku ughaibuni wanazichukua zaidi wao.

Wahenga walisema kuwa asiyefunzwa na mama yake, hufunzwa na ulimwengu. Ndio yatakayowapata wa-Tanzania, katika ulimwengu huu wa utandawazi.

Siku za karibuni nitakuwa Tanzania nikiendesha warsha kuhusu masuala ya aina hiyo. Warsha mbili nitafanyia Arusha, tarehe 3 Julai, na nyingine tarehe 10 Julai. Nilishawahi kutangaza katika blogu hii. Lakini, sina hakika kama ni wa-Tanzania wangapi watakaohudhuria. Ila nina hakika wageni watahudhuria, ili mradi wapate taarifa.

Mimi kama mwalimu, siwezi kumezea au kuendekeza uzembe kama huu walio nao wa-Tanzania, ambao wanatumia pesa nyingi sana kwenye sherehe na bia, lakini kununua kitabu cha shilingi elfu saba hawakubali, wala kutumia saa mbili kwa wiki wakisoma maktabani hawawazii, uzembe ambao unawafanya wawe wanatoa visingizio kila siku, au lawama kwa wengine, hasa serikali, wakati wao wenyewe hawawajibiki.

Kama nilivyogusia, hakuna jipya ambalo nimesema hapa juu, bali ni marudio ya yale ambaye nimekuwa nasema kwa muda mrefu, katika blogu hii na kwingineko.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...