Friday, February 16, 2018

Mrejesho Kuhusu Kitabu

Ni furaha na faraja kwangu kama mwandishi kupata mrejesho kutoka kwa wasomaji. Leo asubuhi, nilipoamka, niliona ujumbe kutoka kwa mwalimu wa chuo cha St. Lawrence. Ameandika:

Mimi ni ndugu Kitito. Tulikuwa wageni wako katika kongamano la African network. Mimi na Robin tunashukuru mno kwa kitabu chako "Africans and Americans." Tunakitumia darasani mwetu. Wanafunzi wamefaidika mno...

Huyu mwalimu Robin anayetajwa nilishaandika habari zake katika blogu hii. Baada ya mimi kusoma ujumbe wake, mwalimu Kitito amenipigia simu, akanielezea zaidi kuhusu kitabu kinavyotumiwa. Nami nilimwelezea nilivyokiandika, baada ya miaka mingi ya kukabiliana na maisha ya Marekani. Nilimweleza kwa nini nilitumia mtindo ambao si kawaida kwa wanataaluma.

Nimefarijika kupata mrejesho kutoka kwa waalimu hao ambao wanatumia kitabu changu, nami nimeona niweke kumbukumbu hii hapa, kama ilivyo kawaida yangu.

Monday, February 12, 2018

Nasubiri Mhadhara wa Red Wing

Tarehe 17 mwezi huu, nitakwenda Red Wing kutoa mhadhara, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Mada itakuwa "African Storytelling" yaani jadi ya hadithi za Afrika. Maandalizi yamefanyika kikamilifu, kama inavyoonekana katika tangazo la mhadhara.

Hii si shughuli ya kwenda kusimulia hadithi tu. Ni kuelimisha kuhusu misingi, maana, na dhima ya hadithi za jadi katika utamaduni wa Afrika. Jadi ya kusimulia hadithi ni sanaa yenye kugusa vionjo na hisia za binadamu, pia ni nia ya kuhifadhi elimu na kuelimisha. Hadithi zinayotafakari maisha, tabia na mahusiano ya binadamu, na masuala ya maadili.

Hadithi zimefungamana na aina zingine za sanaa ya maneno kama vile methali na nyimbo. pia zimefungamana na mila, desturĂ­, na imani. Ni kioo cha jamii, lakini pia ni kichocheo cha mwenendo wa jamii. Upana huo wa mtazamo kuhusu hadithi nimeubainisha katika kitabu changu, Matengo Folktales ambacho kina hadithi kumi, pamoja na uchambuzi wangu wa kila hadithi. Pia kina insha juu ya padithi kwa mtazamo wa kitaaluma, lakini kwa lugha rahisi.

Mhadhara wangu wa Red Wing utaelimisha kuhusu mchango wa wa-Afrika katika utamaduni wa ulimwengu. Nitaelezea kuwa sanaa ya usimuliaji hadithi ilianzia Afrika, sambamba na kutokea kwa binadamu na lugha. Nitaelezea kuwa falsafa haikuanzia Ulaya, kwa akina Socrates na Plato, bali ilikuwepo Afrika, katika hadithi na aina nyingine za fasihi simulizi. Mafundisho ya hadithi na fasihi simulizi kwa ujumla kuhusu maisha na mahusiano ya binadamu bado yana maana na umuhimu
katika ulimwengu wa leo na kesho.

Ninatoa shukrani kwa uongozi wa Red Wing Public Library na Goodhue County Historical Society kwa kunialika kwenda kutoa mhadhara huu. Nafurahi pia kuwa sitaenda kuzungumza tu, bali pia, k kuoutakuwa na shughuli ya watu kununua na kusainiwa kusaini vitabu vyangu. Vitabu vitadumisha ujumbe wangu katika maisha ya watakaovisoma.

Tuesday, February 6, 2018

Mteja Anapokupigia Debe

Tarehe 3 Februari, nilipata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa dada au mama ambaye amejitambulisha kwa jina la Cynthia, ila simjui. Ameandika kuulizia kitabu changu namna hii:

Hello,

I am planning a trip to Tanzania and someone recommended your book about cultural differences between Africans and Americans. How can I purchase your book? Thank you very much.

Kwa wasiojua ki-Ingereza, tafsiri yake ni hii:

Habari

Ninapanga safari ya kwenda Tanzania na mtu fulani alikipendekeza kitabu chako juu ya tofauti za tamaduni za wa-Afrika na wa-Marekani. Nitakinunuaje kitabu chako? Shukrani sana.

Kwa mwandishi, habari ya aina hii ni habari njema. Kwamba mtu fulani ambaye alitumia hela zake kununulia kitabu chako alikisoma akaridhika au kufurahi kiasi cha kukipendekeza kwa mwingine, si jambo jepesi. Mtu anapopendekeza kitu kwa mwingine namna hii, anajiweka katika hali ya kueleweka vibaya, iwapo kile anachopendekeza hakitamridhisha huyu mwingine. Tunapendekeza vitu kwa marafiki zetu tukiwa na uhakika na hicho tunachopendekeza.

Sisi wote ni wateja wa hiki au kile, iwe ni vitu au huduma. Muda wote tunawashawishi wenzetu wakanunue kitu fulani au wanapohitaji huduma, tunawaelekeza sehemu ambayo tunaiamini. Tunapopendekeza kitu au huduma tunatoa tamko kuhusu ubora wa kile tunachopendekeza. Nimekuwa nikielezea masuala haya katika blogu hii.

Muda wote sisi binadamu tunafanya hii shughuli ya kupiga debe bila malipo. Tunafanya hiki kibarua kisicho na malipo bila hata kujitambua. Ni sehemu ya mazungumzo yetu na marafiki au watu wengine. Mwenye kuuza bidhaa au kutoa huduma anafaidika bila kutumia hela kulipia matangazo.

Hayo ni baadhi ya mawazo yangu wakati huu ninapotafakari suala la huyu mpiga debe asiyejulikana ambaye amekipendekeza kitabu changu kwa mtu huyu aitwaye Cynthia, ambaye naye simjui. Nimemjibu Cynthia nikamwambia sijui mahali alipo, lakini kitabu anaweza kukipata mtandaoni.

Wednesday, January 24, 2018

Mahagonny: Tamthilia ya Bertolt Brecht

Mwishoni mwa mwaka jana, mwanafunzi wangu mmoja hapa chuoni St. Olaf aliniomba afanye kozi ya kujitegemea chini ya usimamizi wangu. Tuna utaratibu wa kuwapa wanafunzi wanaohitaji fursa ya kufanya kozi za aina hiyo. Mwanafunzi anajitungia mada kwa kushauriana na profesa, na anaifanya kozi kwa kusoma vitabu na maandishi husika, kukutana na profesa mara kwa mara kujadiliana, anaandika makala na kufanya mitihani kadiri profesa anavyopanga.

Baada ya mazungumzo ya awali na mimi kuelewa alichotaka mwanafunzi huyu, kwamba alitaka kujielimisha kuhusu Marxism, na kwa kuzingatia masomo mengine anayosoma, katika sayansi ya jamii, nilimshauri kuwa mada ya kozi yake iwe  "Marxism, Alienation and Culture." Ingekuwa rahisi kwangu kuandika makala hii kwa ki-Ingereza, kwani sina hakika nitafsiri vipi dhana ya "alienation" kwa ki-Swahili.

Ili kuitafakari mada hii kinadharia, nilipendekeza mwanafunzi asome na tujadili ufafanuzi wa Marx na Istvan Meszaros kuhusu "alienation." Nilipendekeza tusome na kujadili jinsi dhana hii inavyotumiwa na Bertolt Brecht na inavyoweza kuhusishwa na riwaya ya Albert Camus, The Stranger.

Kwa kuwa Marx alijenga dhana ya "alienation" kwa kuihusisha zaidi na ubepari, nilipendekeza tusome tamthilia ya Bertolt Brecht iitwayo The Rise and Fall of the City of Mahagonny na tamthilia ya Arthur Miller iitwayo Death of a Salesman. Nilishauri pia tusome mawazo ya Ernest Hemingway kuhuru uandishi katika mfumo wa kibepari, alivyoandika katika Green Hills of Africa, na pia tusome shairi la Wordsworth, "The World is Too Much with Us," ambalo nililitaja katika blogu hii. Nilipendekeza pia tusome na kujadili pia ufafanuzi wa Walter Benjamin katika "The Work of Art in the Age of Mechanical Reproduction" na Raymond Williams katika "Culture is Ordinary."

Ingawa tumeshajadili mengi ya hayo maandishi, napenda kusema neno kuhusu tamthilia ya Brecht, The Rise and Fall of the City of Mahagonny. Niliona muhimu kumweka Brecht katika orodha, kwa sababu alielezea mbinu za utungaji na uigizaji wa tamthilia ambazo huitwa "alienation effects" zilizokusudiwa kuifanya tamthilia kuwa zana ya kuelimishia badala ya kuwa burudani tu na kichocheo cha hisia. Kwa kutumia mbinu hizo, Brecht alitaka watazamaji wa tamthilia wakumbane na masuala ya kufikirisha.

Brecht alikuwa na mwelekeo wa ki-Marxisti. Alifahamu jinsi ubepari unavyohujumu ubinadamu au utu. Hayo nilifahamu tangu nilipoanza kumsoma Brecht nilipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Dar es Salaam, kuanzia mwaka 1973. Miaka ile tulisoma Mother Courage and her Children na The Caucasian Chalk Circle, lakini tulifahamu pia kuhusu tamthilia zake zingine, kama vile Galileo. Nilivutiwa na Brecht kiasi kwamba nilijisomea The Rise and Fall of the City of Mahagonny.

The Rise and Fall of the City of Mahagonny inatuonyesha jinsi katika ulimwengu huu unaotawaliwa na pesa, hapendwi mtu, kama wa-Tanzania wasemavyo, bali ni pesa tu. Ukiwa na pesa, unakuwa na marafiki wengi. Ukiishiwa, huwaoni tena, na utajutia. Mhusika mmoja anasema: "What man's viler than a broke one?" yaani kuna mtu mbaya gani kumzidi aliyeishiwa? Tunaambiwa pia kuwa kuishiwa ni kosa la jinai na kwamba mtu asiye na pesa hastahili kuhurumiwa wala kusamehewa.

Pesa imekuwa kama ugonjwa ulioenea katika jamii. Hata mahakamani kumetawaliwa na pesa, kwani mahakimu na mawakili wananunulika. Ni kama alivyoandika Marx katika The Communist Manifesto: "The bourgeoisie has stripped of its halo every occupation hitherto honored and looked upon with reverent awe."

The Rise and Fall of the City of Mahagonny inatupa taswira ya jamii ambayo maadili yake yamevurugwa kabisa na suala la pesa.  Ingawa hapendwi mtu bali pesa, kwenye suala la pesa hakuna urafiki, kwa maana kwamba ukiwa na shida ya pesa, usimtafute wala usitegemee mtu wa kukusaidia. Hutampata, hata kama anazo. Tunashuhudia hayo yanavyomsibu mhusika aitwaye Jimmy. Tunamwona anavyowanunulia watu vinywaji wakati alipokuwa na pesa, lakini anapoishiwa na kujikuta matatani, watu wale wale wanamkwepa kabisa, bila aibu.

Tunakaribia kumaliza kozi yetu. Mada ya "Marxism, Alienation, and Culture" ni pana. Nategemea kuwa kwa siku chache zilizobaki, tutazama zaidi katika kile kinachoitwa "popular culture." Hata hivyo, tumeweza kuichambua kiasi cha kufahamu angalau vipengele vyake muhimu, hasa mitazamo juu ya dhana ya "alienation."

Saturday, January 13, 2018

Mwalimu Nyerere na Vyama vya Upinzani

Ninakumbuka jinsi mchakato wa kuanzishwa kwa vyama vya siasa Tanzania ulivyokuwa. Hapa simaanishi vyama vya ile miaka ya Uhuru, bali miaka hii ya CCM. Mchakato ulisukumwa na mambo kadhaa, yakiwemo mabadiliko ya ulimwengu na msukumo kutoka katika jamii ya wa-Tanzania.
Kati ya watu waliosukuma mchakato huu kutoka ndani ya Tanzania ni Mwalimu Nyerere. Alifanya hivyo kutokana na kukerwa hadi kuchoshwa na tabia ya CCM, ya kujisahau na kuwa ni chama kilichoingiwa na kansa na ubovu katika uongozi wake. Mwalimu Nyerere mwenyewe aliandika katika kitabu chake, "Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania," kuwa ubovu wa uongozi wa CCM ndio ulimfanya ahamasishe uwepo wa vyama vingi. Mwalimu Nyerere aliamini kuwa kuwepo kwa vyama vya upinzani kungeweza kuinyoosha CCM.
Lakini CCM haikuwa na msimamo huo. Tangu vilipoanzishwa vyama vya upinzani, CCM ilikuwa inajaribu kwa kila namna kuvihujumu. Kwa mfano, ninakumbuka kwamba Lyatonga Mrema alikuwa kiongozi wa upinzani aliyependwa sana. Katika mikutano yake, wanachama wake walikuwa na tabia ya kusukuma gari lake baada ya mikutano, kama ishara ya mapenzi yao kwake.
CCM walikuwa wakizuia wanachama wale wasisukume gari la Mrema. Mwalimu Nyerere aliwakanya CCM, akasema kuwa wawaache watu wasukume gari. Hicho ninachosema ni ukweli.
Mwalimu Nyerere aliendelea kuwa na msimamo wake wa kutetea vyama vya upinzani, ingawa yeye mwenyewe aliendelea kuwa mwana CCM. Katika kitabu hicho cha "Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania" (uk. 66), Mwalimu Nyerere alitamka wazi kuwa kutokana na ubovu wa CCM, alitamani kipatikane chama bora cha upinzani ili kiongoze nchi badala ya CCM.
Wazo hili la chama kingine kuongoza nchi halijawahi kukubaliwa na CCM, hadi leo. Badala yake, CCM imezidisha nguvu ya kuvihujumu vyama vya upinzani. Leo hii, CCM inatumia polisi wazi wazi, kinyume kabisa na sheria ya vyama vya siasa. CCM imekwenda mbali sana, na leo inawaona wapinzani kama si wazalendo. Inatisha kwamba tumefika hapa.
Ninawashauri wa-Tanzania wenzangu tusikilize mawaidha ya Baba wa Taifa. Angalau tusome vitabu vyake, hata kama ni viwili vitatu tu. Kuna usemi wa wahenga kuwa asiyesikia la mkuu huvunjika guu. Kwa kutozingatia ushauri wa Mwalimu Nyerere kuhusu umuhimu wa upinzani, CCM itaendelea kuipeleka Tanzania kubaya. Hatimaye ni kuvunjika guu.
Rais Magufuli anasema daima kwamba msema ukweli ni mpenzi wa Mungu. Nadhani anamaanisha wale wanaosema yaliyomo moyoni na akilini mwao, bila unafiki. Kama nimemwelewa vizuri, basi mimi ni mmoja wa hao wasema ukweli. Sikubaliani na sera yake Rais Magufuli ya kuubana upinzani. Ninataka afuate nyayo za Mwalimu Nyerere, ambaye alitetea upinzani, mikutano na maandamano ya amani, hata kusukuma magari.

Friday, January 12, 2018

"The World is Too Much With Us" (William Wordsworth)

William Wordsworth ni mmoja kati ya washairi maarufu kabisa katika ki-Ingereza. Kila ninapoona au kukumbuka jina la Wordsworth, shairi lake refu na maarufu liitwalo "Tintern Abbey" linanijia hima akilini. Leo napenda kuleta shairi moja ambalo linatuasa juu ya mahangaiko yetu na mambo ya dunia, hasa kusaka pesa na kutumia, ambayo yanafuja vipaji vyetu vya asili na kutusahaulisha yale ambayo yangetuletea faraja ya kweli. Shairi hili linaitwa "The World is Too Much With Us." Mtazamo huu umejengeka katika mkondo wa ushairi na sanaa kwa ujumla ambao unaojulikana kama "Romanticism," ambamo alikuwemo Wordsworth pamoja na washairi wenzake maarufu kama Samuel Taylor Coleridge, Percy Bysshe Shelley, Lord Byron na John Keats.


THE WORLD IS TOO MUCH WITH US

The world is too much with us; late and soon,
Getting and spending, we lay waste our powers;
Little we see in Nature that is ours;
We have given our hearts away, a sordid boon!
The sea that bares her bosom to the moon;
The winds that will be howling at all hours,
And are up-gathered now like sleeping flowers;
For this, for everything, we are out of tune;
It moves us not.--Great God! I'd rather be
A pagan suckled in a creed outworn.
So might I, standing on this pleasant lea,
Have glimpses that would make me less forlorn;
Have sight of Proteus rising from the sea;
Or hear old Triton blow his wreathed horn.

(William Wordsworth, 1770-185)

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...