Saturday, November 24, 2018

Kumbukumbu ya Matengo Folktales Kutajwa Katika "Jeopardy."

Kipindi kama hiki, mwaka jana, kitabu cha Matengo Folktales kilitajwa katika kipindi maarufu cha televisheni kiitwacho Jeopardy." Ilikuwa tarehe 23 Novemba, nami niliandika taarifa katika blogu hii.

Tukio hili la kushtukiza lilinifungua macho nikatambua kuwa "Jeopardy" ni maarufu sana hapa Marekani. Bado sijui taarifa za kitabu changu zilifikaje kule, ila ninafurahia kuwaambia waMarekani taarifa hizo kila ninaposhiriki matamasha ya vitabu.

Thursday, November 22, 2018

Vitabu Kama Zawadi ya Sikukuu

Kwa watu wengi, huu ni wakati wa maandalizi ya sikukuu ya Krismasi. Pamoja na mengine, ni kununua zawadi kwa ajili ya ndugu, marafiki na kadhalika. Hapa Marekani, vitabu ni zawadi mojawapo inayothaminiwa.

Hapa kushoto ni picha niliyopiga tarehe 16 Novemba katika duka la vitabu la Barnes and Nobel mjini Burnsville. Inaonyesha kabati la vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka. Nilipiga picha hiyo kwa sababu kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kipo hapo. Kimekuwepo kwa wiki nyingi. Bila shaka kuna wateja wanaoingi na kuchungulia kwenye kabati hilo ili kupata wazo juu ya kitabu cha kununua, kwani tayari kimependekezwa na watu wazoefu wa vitabu.

Utamaduni wa kuvihesabu vitabu kama zawadi muafaka kwa sikukuu au mazingira yeyote mengine unanivutia, kama nilivyowahi kueleza katika blogu hii. Ninatamani utamaduni huu uote mizizi katika nchi yangu. Nawazia furaha watakayokuwa nayo watoto kwa kupewa vitabu kama zawadi, kwa sababu ninajua kuwa watoto wanapenda vitabu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.  Nawazia namna ambavyo mitazamo na fikra za watu zingeboreka kwa kuwa na utamaduni wa kuthamini na kusoma vitabu vya aina mbali mbali.

Saturday, November 10, 2018

Nimeongea na Lumen Christi Book Club

Miezi kadhaa iliyopita, nilipata mwaliko wa kwenda Lumen Christi Catholic Community kuongelea kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Aliyenialika ni Jackie ambaye alikuwa amekisoma kitabu hicho. Alisema kwamba jumuia ya waumini hao wana klabu yao ya usomaji vitabu, na kwa sasa wamejikita katika vitabu vinavyohusu Afrika.

Nilipoingia ukumbini, niliona meza imepangwa vizuri karibu na mlandoni, yenye vitabu vyangu na vya waandishi wawili ambao tunafahamiana: Maria Nhambu ambaye alizaliwa Tanzania, na Afeworki Ghorghis, jaji mstaafu wa mahakama kuu ya Eritrea.

Baada ya Jackie kunitambulisha, nilielezea kifupi nilivyokulia Tanzania, katika utamaduni wa wa-Matengo, na hatimaye nilivyokutana na utamaduni wa Marekani, nilipokuwa masomoni katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, na kufikia kuwa mshauri kwa vyuo vinavyopeleka wanafunzi Afrika, kama nilivyoandika katika utangulizi wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Katika kuelezea uandishi wangu juu ya masuala ya utamaduni, nilianza na kitabu cha Matengo Folktales.

Baada ya hapo, Jackie alitaja vipengele vilivyomo kitabuni ili nielezee, na wengine waliniuliza masuali yao. Kati ya masuala tuliyoongelea ni "gifts" (sio kwa maana ya zawadi), uzee, na "African time." Nilielezea nilivyoandika kitabuni kuhusu masuala hayo. Klabu hii ya vitabu ni ya aina yake, kwa maana kwamba watu wanahudhuria hata bila kusoma kitabu kinachojadiliwa.

Mkutano ulikuwa mzuri na wenye manufaa. Binafsi, nilitoa shukrani kwa fursa ya kufahamiana na watu wapya, kwani inatajirisha maisha yangu. Nilifurahi kuweza kuwaelezea shughuli zangu kama mtoa ushauri chini ya mwavuli wa Africonexion.  Baada ya mimi kurejea nyumbani, Jackie aliniletea ujumbe kwamba atanitambulisha kwa mkurugenzi wa East Side Freedom Liabrary ambaye wakati huu anaandaa programu kuhusu Afrika. Sikuwa ninajua kuhusu maktaba hiyo. Ninasubiri.

Thursday, October 25, 2018

Nimepeleka Vitabu kwa wa-Matengo

Mwezi Julai mwaka huu nilikwenda Tanzania, nikiwa nimechukua vitabu vingi. Baadhi ni vile nilivyoandika mwenyewe, ambavyo niliviwasilisha katika maduka ya Kimahama, na A Novel Idea. Nilichukua pia nakala 16 za Matengo Folktales kwa ajili ya kuzipeleka kwa wa-Matengo, wilayani Mbinga, katika mkoa wa Ruvuma.

Ninasema hivyo, na kutaja kabila langu, nikijua kwamba kwetu wa-Tanzania, hii ni kauli tata, isiyopendeza, kwani inaashiria upendeleo au ubaguzi kwa msingi wa kabila. Utamaduni wa Tanzania, uliojengwa na chama cha TANU, hauafiki ubaguzi wa makabila au wa aina nyingine. Sasa kwa nini nimetoa kauli hiyo? Kwa nini niliamua kupeleka nakala hizi za Matengo Folktales kwa wa-Matengo? Napenda kuthibitisha kwamba nilifanya jambo muafaka.

Matengo Folktales ni mkusanyo wa hadithi za jadi ambazo nilizirekodi nyumbani u-Matengo miaka ya sabini na kitu. Nilizirekodi katika kaseti, kisha nikachagua hadithi kumi na kuzitafsiri kwa ki-Ingereza. Niliandika uchambuzi wa kila hadithi na nikaongezea insha ya kitaaluma kuhusu hadithi. Huu ukawa ni mswada ambao ulichapishwa kama Matengo Folktales.

Mimi ni mwanataaluma katika taaluma hii inayojulikana kama "Folklore." Kama ilivyo katika taaluma zingine, tuna taratibu na maadili ya utafiti, uandishi na uchapisahji. Kati ya hayo ni utaratibu wa kuwarudushia fadhila watu wanaowezesha utafiti wetu. Watafiti tusiwe tunachukua yale tunayopewa bila kuwarejeshea kwa namna moja au nyingine wale wanaotupa hayo tunayotafuta. Dhana hiyo huitwa "reciprocity" kwa ki-Ingereza.

Kuna nämna mbali mbali za kurudisha fadhila, kufuatana na mila na desturi za mahali husika na kufuatana na ridhaa ya mtu binafsi anayetuwezesha. Kuna namna mbali mbali za kutoa shukrani. Kwa upande wangu, na kwa watafiti wengi, namna bora kabisa ya kurudisha fadhila ni kuwapa nakala ya yale ninayorekodi na kuondoka nayo, kama vile kaseti au picha ninazopiga.

Kwa msingi huo, baada ya kuchapisha Matengo Folktales, nilijua kwamba nina wajibu wa kupeleka nakala kwa wa-Matengo. Kwa kuwa nimechapisha kitabu kwa ki-Ingereza, ilibidi nisubiri hadi ipatikane sehemu muafaka ya kupeleka.

Fursa imepatikana kwa kuwepo kwa shule za sekondari. Hizi nakala 16 nilimkabidhi mwalimu Frank Kinunda mjini Mbinga, baada ya mawasiliano naye, naye amezisambaza kwenye hizo shule. Zitawaelimisha vijana na walimu kuhusu utamaduni wa wahenga, na pia kuhusu taaluma ya "Folklore." Vile vile, kwa kuwa  nimeandika kwa uangalifu mkubwa kama mwalimu wa lugha ya ki-Ingereza, Matengo Folktales ni kitabu cha kujiongezea ujuzi wa ki-Ingereza. Kitabu hiki kinatumika kufundishia katika vyuo hapa Marekani, na ninafurahi kimeanza kuwa mikononi mwa wanafunzi na walimu Tanzania

Sunday, October 21, 2018

Minnesota Black Authors Expo Imekaribia

Bado siku sita tu hadi maonesho yaitwayo Minnesota Black Authors Expo yatakapofanyika. Hii ni mara ya pili kwa maonesho haya kufanyika. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka jana.

Waandaaji waliniomba niwemo katika jopo la waandishi watakaoongelea masuala mbali mbali ya uandishi wa vitabu. Nilikubali. Jopo linategemewa kuwa kivutio kikubwa katika tamasha hilo.

Friday, October 19, 2018

Waandishi Marafiki Tumekutana

Tarehe 13 mwezi huu, nilishiriki tamasha la vitabu liitwalo Deep Valley Book Festival mjini Mankato, jimbo hili la Minnesota. Nilishahudhuria mara tatu tamasha hili linalofanyika mara moja kwa mwaka. Nilijua kuwa mmoja wa waandishi ambao walikuwa mbioni kushiriki ni rafiki yangu Becky Fjelland Brooks anayeonekana pichani kushoto.

Becky ni mwalimu katika South Central College hapa Minnesota. Tulianza kufahamiana wakati yeye na Profesa Scott Fee wa Minnesota State University Mankato waliponialika kwenda kuongea na wanafunzi waliokuwa wanawaandaa kwa safari ya masomo Afrika Kusini.

Watu wengi walihudhuria mhadhara wangu kuhusu tofauti za tamaduni, na nakala nyingi za kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences zilinunuliwa. Baada ya hapo, nimepata mialiko ya kwenda kuongea na wanafunzi hao kila mara wanapoandaliwa safari ya Afrika Kusini.

Mwalimu Becky ni mmoja wa wale wa-Marekani ambao wanaipenda Afrika na wanajibidisha kuwaelimisha wenzao kuhusu Afrika. Kuandaa programu za kupeleka watu Afrika ni kazi ngumu, yenye changamoto nyingi. Inahitaji ujasiri na uvumilivu. Nina uzoefu wa shughuli hizo, na ninawaenzi watu wa aina ya mwalimu Becky.

Mwalimu Becky ni mwandishi mwenye kipaji. Tayari ameshachapisha vitabu kadhaa, kwa ajili ya watoto, vijana, na watu wazima. Umaarufu wake unaongezeka mwaka hadi mwaka, na ameshatambuliwa na tuzo kama Midwest Book Awards. Ni faraja kwangu kwamba mwalimu Becky, mwandishi maarufu, anakipenda sana kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na anaipenda mihadhara yangu, kama inavyonekana hapa na hapa.

Hii tarehe 13, kwa kuwa mwalimu Becky na mimi tulifahamu kuwa tungekutana, nilichukua nakala yangu ya kitabu chake kiitwacho Slider's Son ili anisainie. Ninavyo vitabu vyake vingine ambavyo alivisaini siku zilizopita. Tulifurahi kukutana. Ninajiona nimebarikiwa kuwa na rafiki kama huyu. Picha hiyo hapa juu aliiweka Facebook akiwa ameambatisha ujumbe huu: "With my dear friend Joseph Mbele, author of the enlightening and humorous book, "Africans and Americans," sharing stories and friendship at the Deep Valley Book Festival today...."

Thursday, October 18, 2018

Kitabu Bado Kiko Dukani Barnes and Noble

Juzi nilienda Apple Valley na Burnsville kuangalia maduka ya vitabu, kama nilivyoandika katika blogu hii. Kule Burnsvile, mji jirani na Apple Valley, nilitaka kuingia katika duka la Barnes and Noble ambamo kitabu changu kilikuwa kimewekwa sehemu maalum ya vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Sikujua kama ningekikuta, kwani sijui utaratibu wanaofuata katika kuvionesha vitabu hivyo sehemu hiyo. Nilidhani labda vinawekwa kwenye kabati hili kwa wiki moja hivi. Nilishangaa kukiona kitabu changu bado kipo, na kimewekwa juu zaidi ya pale kilipokuwepo kabla. Hapa kushoto ni picha niliyopiga wiki iliyopita, na kulia ni picha niliyopiga juzi. Ninafarijika na kufurahi kukiona hapa. Ninasubiri siku ya kwenda kukiongelea, kama nilivyodokeza.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...