Monday, January 19, 2009

Waafrika Wanamwenzi Obama?

Kesho, tarehe 20 January, 2009, Barack Obama anaapishwa kama rais wa 44 wa Marekani. Dunia nzima iko katika heka heka za furaha na matumaini yasiyo kifani kutokana na ushindi wa Obama katika kampeni za urais wa Marekani.

Waafrika nao wamejawa na furaha, na wanajivunia, wakizingatia kuwa baba yake Obama ni Mwafrika mwenzao, kutoka Kenya. Waafrika wanaamini kuwa Rais Obama atajenga uhusiano bora na Afrika, kwani Afrika ni kwake.

Lakini je, Waafrika wanaomshangilia Obama wanamfahamu Obama au wanashangilia tu kwa vile kwa asili yake ni Mwafrika? Ukweli ni kuwa, Waafrika wengi hawana fikra wala mtazamo kama wa Obama kwa mambo mengi. Kwa mfano, Obama amekuwa mstari wa mbele kwa shughuli za kujitolea kwa ajili ya jamii yake na binadamu kwa ujumla, amekuwa mtetezi wa wanyonge, na ameonyesha mfano mzuri wa kujibidisha katika elimu na kuwa binadamu bora.

Ajabu ni kuwa hata Waafrika ambao ni wazembe, wanaoendekeza rushwa na ufisadi, wasiothamini elimu, wasiothamini suala la kujitolea, wote wanamshangilia Obama. Kuna nini katika vichwa na mioyo ya watu hao?

Obama amezingatia sana suala la heshima kwa wanadamu wote bila kujali tofauti za rangi, dini, taifa, na kadhalika. Anaamini kuwa kila mtu anastahili fursa ya kufanya yale ambayo yanaendana na uwezo wake. Ana imani kubwa kuhusu uwezo wa binadamu, na kila binadamu.

Waafrika wengi ni wabaguzi, kwa misingi ya kabila, dini, na kadhalika. Hawatambui usawa wa binadamu, bali wanamthamini mtu wa kabila lao, kijiji chao, ukoo wao, dini yao, na kadhalika. Wakati Obama amechaguliwa na Wamarekani wa rangi na dini mbali mbali, na wakati Obama anawahamasisha Wamarekani kujiona kama kitu kimoja, bila kujali tofauti zao, wawe ni weusi, weupe, wanawake, wanaume, wa dini mbali mbali, na kadhalika, Waafrika wengi hawako tayari hata kumpigia kura mtu wa kabila lisilo lao.

Inashangaza kwamba Waafrika hao ambao wanapigana na kuchukiana kutokana na tofauti za lugha, utamaduni, kabila, na kadhalika, wanashangilia ushindi wa Obama na wanaamini kuwa Obama ni mtu wao. Inashangaza kuwa nao wanaamini wanamwenzi Obama, badala ya kutambua kuwa namna ya kweli ya kumwenzi Obama ni kufuata nyayo zake. Ni sahihi kabisa kuuliza: hao Waafrika wanamwenzi Obama kweli au wanajikanyaga?

1 comment:

Simon Kitururu said...

Nakubaliana na yote uliyosema !Halafu tupo Waafrika ambao mpaka tunasahau kuwa yeye ni Rais wa Marekani na kachaguliwa kuongoza na kutatua matatizo ya Marekani na sio ya Afrika kwanza.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...