Saturday, January 17, 2009

Watanzania na Mkutano wa Sullivan

Mwanzoni mwa mwezi Juni, 2008, mji wa Arusha ulipata fursa ya kuwakaribisha wageni wengi kwenye mkutano mkuu wa nane wa Sullivan. Nilikuwa katika mkoa wa Arusha pamoja na Wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado, ambao nilikuwa nawafundisha kuhusu maandishi na safari za Ernest Hemingway maeneo hayo. Kwa hivi, sikupata fursa ya kuhudhuria mkutano wa Sullivan.

Hata hivi, nilipata fursa tele ya kuongea na Watanzania kuhusu mkutano huo. Lengo la taasisi ya Sullivan ni kuchangia maendeleo ya Afrika, kwa kujenga uhusiano wa kibiashara, kijamii, na kadhalika baina ya Afrika na hasa Marekani na Ulaya. Mwanzilishi wa taasisi alikuwa Mmarekani Mweusi, Rev. Leon Sullivan, na kwa sababu hiyo, taasisi hii imekuwa na mvuto mkubwa miongoni mwa Wamarekani Weusi. Hao wanaikaribisha kwa mikono miwili fursa ya kuwekeza barani Afrika na kuungana na Waafrika katika kutekeleza ajenda ya maendeleo.

Basi, kwenye mkutano wa Arusha, Wamerekani Weusi walikuja wengi sana, wakiwemo watu maarufu katika nyanja mbali mbali, wanasiasa, wafanya biashara, na wanataaluma. Mategemeo ya mkutano yalikuwa mengi, kama vile kutoa fursa ya wawekezaji kuleta mitaji, kujenga ushirikiano baina ya wafanya biashara wa Tanzania na hao wageni, na kujenga ushikiriano katika nyanja mbali mbali.

Katika mazungumzo yangu na Watanzania, nilikuwa nawauliza kama wao wamejiandaa vipi kwa yote hayo. Niliwauliza, Je, wanavyowania kushirikiana na Wamarekani, wamefanya juhudi yoyote kuwafahamu hao Wamarekani? Wanamfahamu Mmarekani Mweusi? Hapo nilimaanisha ufahamu wa tabia, hisia, imani, maadili, namna ya kufikiri, namna ya kuongea, na kadhalika. Je, Mtanzania anafahamu hayo? Au anadhani kuwa ni jambo rahisi tu kukutana na Wamerekani na kushughulika nao?

Maongezi yalikuwa mazuri, na nilipata fursa ya kuwaeleza umuhimu wa kujiandaa. Niliwapa mifano hai kuhusu tabia na hisia za Wamarekani Weusi. Mfano moja niliutoa kwa kutumia tabia za Watanzania wanapokuwa na wazungu. Watanzania, kama walivyo Waafrika wengine, wana tabia ya kumtetemekea mzungu. Katika mahoteli ya utalii, kwa mfano, wahudumu wa kiTanzania wanawahangaikia sana wazungu, na hawaoni tatizo kumwacha mteja Mwafrika akiwa bila huduma au kumwacha akingoja huduma hiyo hiyo, hata kama aliwahi.

Niliwaeleza kuwa endapo Wamarekani Weusi watakuja na kuona tabia hii, hawatafurahishwa; watakata tamaa, na huu unaweza ukawa ndio mwisho wa hili wazo la kujenga ushirikiano. Tatizo ni kwamba Watanzania kwa ujumla hawaelewi undani wa hali ya Marekani na mahusiano baina ya Wamarekani Weusi na weupe. Hawaelewi hisia na fikra za Wamarekani. Niliwaasa Watanzania waache kuishi katika ulimwengu wa giza na ndoto, bali waanze kujielimisha.

Mfano mwingine niliotoa ni namna ya kuongea. Wamarekani wanaongea kwa namna ambayo inaweza kuonekana ni maudhi kwa Mtanzania, wakati wao kwao ni sahihi. Na wao wanaweza kuudhiwa na namna Watanzania wanavyoongea, wakati kwa upande wa Tanzania ni sahihi. Na kuna mambo mengine mengi yanayotofautiana baina ya tamaduni hizi mbili.

Kwa hivi, niliwaambia Watanzania kuwa suala la kujielimisha kuhusu hao Wamarekani ni la msingi. Sikusita kuwaeleza kuwa mimi ni mtafiti na naandika sana kuhusu masuala hayo. Niliwaeleza kuwa waanze kulichukulia suala la kujisomea na kujielimisha kuwa ni suala muhimu, hata katika biashara. Kununua kitabu kwa ajili hiyo ni sawa na kununua kifaa kingine chochote kinachoboresha biashara. Kwa lugha rahisi, kitabu ni zana na mtaji muhimu.

Nitaendelea kufanya mazungumzo ya aina hii, kwa namna yoyote. Kwa bahati nzuri, nimeshaanza sasa utaratibu wa kuendesha semina, ninapokuwa Tanzania. Nilifanya hivyo mwaka jana, kama inavyoonekana hapa, na ndivyo itakavyokuwa siku zijazo, panapo majaliwa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...