Sunday, January 30, 2011

TAMKO LA JUMUIA NA TAASISI ZA KIISLAM JIJINI MWANZA

Nimeona tamko hili nikaamua kuliweka katika blogu yangu, kwa vile ninaheshimu uhuru na haki ya watu kujieleza. Mimi ni m-Katoliki, na ingawa sikubaliani na kila kilichomo katika tamko hili, nimeona lina mengi ya kufikirisha, kwa manufaa ya Taifa letu. Hatuwezi kukwepa ukweli kwamba ni Taifa la watu wa imani mbali mbali na mitazamo mbali mbali, na kwa hivi, pamoja na tofauti zetu, lazima tutafute namna ya kuishi pamoja kwa maelewano. Hatua moja ni kusikiliza maoni ya kila mtu, kwa utulivu na kuheshimiana. Ndio maana nachangia kueneza tamko hili.

---------------------------------------------------------------------------------------

TAMKO LA JUMUIYA NA TAASISI ZA KIISLAMU JIJINI MWANZA KUHUSU HALI YA KISIASA, KAULI ZA MAASKOFU, NA MUSTAKBALI WA NCHI LILILOTOLEWA JUMAPILI TAREHE 23 JANUARI, 2011 KATIKA VIWANJA VYA SHULE YA MSINGI MBUGANI (MUSLIM SCHOOL), JIJINI MWANZA
UTANGUZI:

Mwaka 2010 ulikuwa mwaka wa Uchaguzi wa viongozi wa ngazi mbali mbali wakiwemo madiwani, wabunge, wawakilishi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Zanzibar.

Kabla ya Uchaguzi huo, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), kupitia Idara yake ya Kichungaji ya Tume ya Haki na Amani, lilitoa Waraka wa Kichungaji lililouita "MPANGO WA KUHAMASISHA HUDUMA YA KICHUNGAJI KATIKA JAMII KUELEKEA UCHAGUZI MKUU 2010 na baada ya muda wakatoa walichokiita ILANI YA UCHAGUZI NA VIPAUMBELE VYA TAIFA. Huu ulikuwa mweleko mpya wa Kanisa kuingia katika siasa mia kwa mia kwani huko nyuma Kanisa halikuwahi kutoa Waraka wenye maudhui kama hiyo na halikuwahi kutoa Ilani ya Uchaguzi na Vipaumbele vya Taifa.

Kwa kuelewa hatari ya Waraka na Ilani hiyo ya Kanisa, waislamu walipinga kwa nguvu zote mwelekeo huu mpya wa Kanisa. Hata baadhi ya wanasiasa wenye upeo, akiwemo Mzee Kingunge Ngobale Mwiru, walikemea mweleko huo wa Kisiasa wa Kanisa Katoliki lakini wakabezwa kwa kuambiwa kuwa wamezeeka na kufilisika kisiasa na hata kutakiwa wanyamaze kimya.

Baada ya waislamu kuona kuwa wamepuuzwa, na kwa kuelewa nafasi yao kwa waislamu, Shuura ya Maimamu Tanzania, ikatoa maelekezo kwa waislamu kupitia "MWONGOZO KWA WAISLAMU" ili waislamu "Wasidhulumu wala wasikubali kudhulumiwa" kama Qur'an inavyoagiza (Qur'an 2:279).

Wakati wote wa Kampeni za Uchaguzi, msimamo wa Maaskofu kutoka takriban Makanisa yote ya Kikristo nchini ulikuwa ni kuunga mkono Mgombea Urais wa Chadema na wagombea wengine wa chama hicho nchi nzima. Makanisa yakatumika kumnadi mgombea huyo kama Waraka wao wa Kichungaji ulivyoelekeza wazi kwa kusema;-
"Mungu anakuhitaji, haya si maneno tu, bali ni uamuzi wa makusudi wa Mungu anayetukabidhi wajibu huu. Kutopokea mwaliko huu unaotoka kwa Mungu ni kushindwa kutimiza wajibu wetu, ni dhambi ya kutotimiza wajibu wa wito wetu wa kikristo. Wito wa kutimiza wajibu wa Kijamii, ambao ni kutia chachu ya tunu za Injili na Mafundisho ya Kristo katika masuala na shughuli za kijamii, kiuchumi na kisiasa ya taifa letu". (Tazama: Mpango wa Kuhamasisha Huduma ya Kichungaji Katika Jamii Kuelekea Uchaguzi Mkuu 2010, Uk. 2).

Kwa kuwa Padri Slaa aliamini kwamba yeye ni chaguo la Kanisa, alijiridhisha yeye binafsi, wafuasi wake, viongozi wenzake wa Chadema na Maaskofu kuwa lazima atashinda na akasema wazi kuwa hatokubali matokeo mengine yoyote kinyume na ushindi wake kwani wakristo walishaambiwa kuwa kutokutekeleza waraka wa Maaskofu ni dhambi. Ni muumini gani ataambiwa na viongozi wa dini yake kuwa kutokufanya jambo fulani ni dhambi kisha asilifanye?

Mfano hai, huko Sumbawanga, Kanisa Katoliki liliwatenga waumini wake kwa kile lilichodai kwenda kinyume na maelekezo ya Kanisa kuhusu wagombea wa chama gani wapigiwe kura. Hali hiyo imepelekea Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Mizengo Peter Kayanza Pinda kuwaomba radhi Maaskofu kwa niaba ya Serikali na Chama chake kwa kile alichodai "kuwaudhi Maaskofu hao wakati wa Kampeni za Uchaguzi"!

Hatimaye tarehe 31 Oktoba, 2010, taifa lilifanya Uchaguzi Mkuu na tarehe 5 Novemba, 2010, Tume ya Taifa ya Uchaguzi ikamtangaza Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kuwa mshindi wa kiti cha Urais na akaapishwa tarehe 6 Novemba, 2010.

Wagombea wote wa kiti cha Urais walikubali matokeo yaliyotangazwa na Tume ya Taifa ya uchaguzi isipokuwa Padri Wilbrod Slaa wa Chadema na chama chake waliyakataa matokeo hayo na hata siku ya kutangazwa na siku ya kuapishwa Rais si yeye Padri Slaa wala viongozi wengine wa Chama chake cha Chadema aliyeshiriki. Hata siku ya Rais Kikwete kuzindua Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mjini Dodoma, wabunge wote wa Chadema walitoka nje ya Ukumbi wa Bunge kuonesha kuwa hawamtambui Rais aliyetangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

Baada ya kuona kuwa mpango wao wa kushika madaraka kupitia mgongo wa Chadema umeangukia patupu, Maaskofu na chama wanachokiunga mkono wakaamua kuhakikisha kuwa nchi haitawaliki. Tunachoshuhudia sasa ni kutolewa kauli mbali mbali dhidi ya Uongozi uliko madarakani hata kwa mambo ambayo hayakufanywa na uongozi huu uliopo sasa bali yalifanywa na awamu zilizotangulia.

Kwa mfano, mikataba mibovu ya migodi ya madini inayolalamikiwa ilifanywa wakati wa awamu ya Mkapa, Kuuzwa mashirika ya umma kwa bei za kutupwa kulifanywa wakati huo huo wa Mkapa, kuuzwa kwa nyumba za serikali katika maeneo ya serikali kwa bei ya kutupwa kiasi kwamba baadhi ya viongozi wa serikali hivi sasa wanaishi nyumba za wageni (guest house) kulifanywa wakati wa Mkapa. Aidha, uvunjaji mkubwa wa haki za binadamu, Kufukiwa wachimba dhahabu Bulyankulu, mauaji ya raia wasio na hatia – Mwembechai, Zanzibar, Pemba, Morogoro, ufisadi na rushwa, Kuvunjwa maadili ya Uongozi, Kashfa za EPA, Meremeta, Kagoda, Net Group Solutions yote hayo hayakufanyika katika awamu hii bali wakati wa awamu ya Mkapa.

Wakati wa awamu ya Mkapa, hatukusikia Maaskofu wakijitokeza kuyakemea haya wala kulaani mauaji ya raia wasio na hatia kama wafanyavyo hivi sasa ila wamekuwa mbogo wakati wa Uongozi huu kama walivyokuwa mbogo wakati wa awamu ya pili ya Mzee Mwinyi. Kinachowasukuma si kingine bali kuogopa ile waliyoiita "dhambi" ya kutokutekeleza wito wao wa Kichungaji wa kuhakikisha kuwa "Tunu za Injili na Mafundisho ya Kristo vinaonekana katika masuala na shughuli za kijamii, kiuchumi na kisiasa za taifa". Laiti isingekuwa hivyo, basi wangesimamia uadilifu wa kukemea maovu katika jamii wakati wote.

Aidha, kwa kuona kuwa mawakala wao wameshindwa kushika nafasi walizoamini kuwa ni haki yao, Maaskofu na chama wanachokiunga mkono hivi sasa wamehamishia juhudi zao zote kudai katiba mpya ya Tanzania kwa nguvu zote (By all means possible) ikiwemo hata kumwaga damu. Mmoja wa viongozi wa juu wa Chadema, Mabere Marando, amesikika akisema wazi katika Mdahalo wa Katiba Mpya Ukumbi wa Nkurumah Chuo Kikuu Dar es Salaam siku ya Jumamosi tarehe 15 Januari, 2011 kuwa "Damu iliyomwagika Arusha ndiyo wino wa kuandika dibaji ya Katiba Mpya Tanzania".
Watu waliotayari kumwaga damu za watanzania kwa malengo ya kisiasa na kudai katiba mpya ni hatari kwa amani na usalama wa nchi yetu kwa sababu katiba huandikwa kwa wino wa kalamu wala si kwa damu ya raia.

Hii inaonesha mwelekeo wa hatari wa kundi hili la Maaskofu na wanasiasa kwa amani na usalama wa Taifa letu. Katiba ya nchi haiwezi kuandikwa kwa damu ya watanzania. Aidha katiba ya nchi haiwezi kuundwa katika mazingira ya vurugu, fujo, uasi kwa viongozi, dharau, kibri, uchu wa madaraka na ubinafsi. Katiba itakayoundwa katika mazingira haya, haitokuwa kwa maslahi ya taifa bali kwa maslahi ya Kanisa.

Hatari nyingine kubwa inayolinyemelea taifa letu, ni ile ya viongozi wa Chama kilichopo madarakani na wale wa serikali kupingana kauli katika mambo ambayo wangepaswa kuwa na kauli moja (Collective responsibility). Mwenendo huu unatishia mustakbali wa nchi yetu kwa sababu utawala uliogawanyika hauwezi kutekeleza majukumu yake kwa raia wake, na ndivyo Maaskofu wanavyotaka iwe. Rais mmoja wa Marekani alipata kusema "A house divided can not stand by itself"-yaani nyumba iliyogawanyika haiwezi kusimama yenyewe. Tunaamini kwamba kugawanyika huku kwa Mawaziri wa serikali iliyopo madarakani ni kazi ya kundi hili hili la Maaskofu na mawakala wao katika Chama tawala na Serikali.

TAMKO LA JUMUIYA NA TAASISI ZA KIISLAMU
JIJINI MWANZA.

Kwa vile, Baadhi ya Maaskofu wamejitokeza wazi wazi kuupinga uongozi uliotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi wakati walikuwa kimya kipindi chote cha awamu ya tatu,

Na kwa vile, mwelekeo na kauli za Maaskofu hao vinapelekea kuiyumbisha nchi ili isitawalike wapate kudai kuwa Rais aliye madarakani hafai bali chaguo lao Padri Slaa ndiye anayefaa,

Na kwa vile, tayari madhara ya mwelekeo huu yameshajitokeza huko Arusha kwa kuuawa watu katika vurugu zilizotokana na uchu wa madaraka ya Umeya wa Jiji hilo na kuchangiwa na kauli za Maaskofu kutomkubali Meya huyo,

Na kwa vile, waislamu ni watu wapenda amani, haki na usawa kwa watu wote bila kujali rangi, jinsia, kabila, dini wala itikadi za kisiasa,

Na kwa kuwa, kuna kila dalili ya kutoweka kwa amani kupitia kauli na vitendo vya Maaskofu kuunga mkono Chama maalum cha siasa,

Na kwa kuwa, baadhi ya Mawaziri wa Serikali ya Rais Kikwete wameonesha wazi kuipinga Serikali yake,

Sisi waislamu wa Jiji la Mwanza tunatamka yafuatayo;-

1. Tunaunga mkono mia kwa mia yote yaliyoandikwa katika tamko la Waislamu lililotolewa Diamond Jubilee Dar es Salaam siku ya Jumamosi tarehe 15 Januari, 2011.

2. Maaskofu kuunga mkono Chama kinachopinga matokeo ya Urais ni kitendo cha Uhaini, U-dini na ni hatari kwa mustakbali wa Taifa letu. Hali kadhalika ni kukiuka hata maandiko ya Biblia yao wenyewe yasemayo "Heri walio wapatanishi kwa maana wataitwa wana wa Mungu. ( Mathayo: 5 msitari wa 9 ).

Tulitaraji viongozi wa dini, Maaskofu wakiwepo, wawe wapatanishi pale wanasiasa wanapogombana. Inapokuwa wao ndiyo sehemu ya ugomvi huo ni nani atawapatanisha wana siasa? Kama Maaskofu wamekuwa wagomvi, watakuwa wana wa nani kama si wa Shetani?

3. Tunawaonya Maaskofu waache kuivuruga Serikali kwa matamshi yao yaliyojaa chuki za U-dini kwani watapelekea amani ya nchi hii kuvurugika kama walivyochangia mauaji ya Kimbari ya Rwanda mwaka 1994.

4. Kwa kuwa Kauli za Maaskofu huko Arusha kutomtambua Meya aliyechaguliwa kwa kufuata taratibu zote za kisheria, zilichangia kuuawa kwa watanzania wasio na hatia, tunaitaka Serikali kuwafikisha Mahakamani Maaskofu wote waliotoa kauli hizo za uchochezi.

Hakuna mtu aliye juu ya sheria. Kama Masheikh hufukishwa Mahakamani na wengine hata kuswekwa kizuizini bila kupelekwa mahakamani, Mfano Al Marhum Sheikh Al Amin Abdallah wa hapa Mwanza na Masheikh wengine mwaka 1964 na wengine kuswekwa ndani kwa kesi za kubumba, Maaskofu wametenda kosa hili la uchochezi wazi wazi hivyo kwa nini sheria isichukue mkondo wake dhidi yao?

5. Kama uchu wa madaraka ya Umeya wa Jiji la Arusha tu umesababisha maisha ya watanzania watatu kupotea, damu za wengi kumwagika na mali kuharibiwa pamoja na kusimamisha shughuli za kiuchumi katika Jiji hilo la kitalii, hali itakuwaje kwa uchu wa kutaka kiti cha Urais? Ni watanzania wangapi watapoteza maisha yao na damu za watanzania wangapi zitamwagika ili Padri Slaa aingie Ikulu?

6. Wakati wa ziara ya Papa Yohana Paulo wa Pili nchini Tanzania mwaka 1990, Kanisa Katoliki lilimtaarifu kuwa linayo Tume ya Majeshi. Hivi jeuri hii ya Maaskofu ni kwa kuwa wanayo hiyo tume ya majeshi? Hata kama wanayo hiyo tume ya majeshi, sisi waislamu kamwe hatuiogopi kwa sababu Mwenyezi Mungu anasema:

"Je, mnawaogopa? Basi Allah anastahiki zaidi ninyi kumuogopa ikiwa mu-waumini wa kweli" (Qur'an 9 : 13).
Pamoja na hayo, tunarudia kuitaka Serikali kuueleza umma wa watanzania tume ya majeshi ya Kanisa ni ya nini? Au hawayaamini majeshi yetu ya ulinzi na usalama?

7. Waislamu tunamtaka Rais Kikwete awawajibishe mara moja Mawaziri wote wanaoipinga Serikali yake kama Mwalimu Nyerere alivyomfanya Kambona alipopinga sera ya Utaifishaji ya serikali yake mwaka 1967. Tunamtaka Rais asiwaonee haya hata kidogo Mawaziri hawa wanaoipinga Serikali yake kwani waswahili husema "Mchelea mwana kulia, hulia mwenyewe" na "Mchelea mwiba, mguu huota tende".

8. Baadhi ya vyombo vya habari vimechangia sana kuzorotesha hali ya amani nchini kwa kuandika au kutangaza habari za uchochezi na hivyo kupelekea kuvunjika kwa amani. Tunavitaka vyombo hivyo vya habari kuacha mara moja kushabikia U-dini na vitende haki. Vinginevyo waislamu tutavitangaza hadharani na kuwahimiza waislamu wasivinunue, kusikiliza au kuvipa matangazo. Tukumbuke pia kuwa mauaji ya kimbari nchini Rwanda yalichangiwa sana na vyombo vya habari.

9. Vyombo vya dola navyo, Jeshi la Polisi, Usalama wa Taifa, Jeshi la Wananchi vitende haki kwa kufanya kazi zao kwa uadilifu, kwa ukweli na uzalendo na kutokupendelea Chama au kundi jamii fulani kwani kwa kufanya hivyo vitasababisha kutoweka kwa amani nchini. Kwa mfano, inapokuwa jambo linahusu Masheikh au waislamu, vyombo hivyo, husuusan Jeshi la Polisi, huwa na ujasiri wa kuwapiga na kuwasweka ndani waislamu lakini ujasiri huo hatuuoni kwa Maaskofu na viongozi wengine wa Kikristo wanapovunja sheria.

10. Kwa wanasiasa na wanaharakati wa mashirika ya kijamii, tunawataka waache kutoa kauli za uchochezi na vurugu kwani amani itakapotoweka hakutakuwa na wanachama wa kuwaongoza. Tumieni busara zenu kujadili mambo kwa hoja na msiporidhika pelekeni malalamiko yenu Mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake.

11. Waislamu tunaunga mkono tamko la Rais Jakaya Kikwete kuhusu kuundwa kwa Katiba mpya. Pamoja na hayo, kwa mwenendo wa Maaskofu na Chama chao wanachokiunga mkono, tunamtahadharisha Rais kwamba amebeba dhamana kubwa ya usalama wa watanzania wote hivyo asisite kuwachukulia hatua wale wote watakaotaka kutumia mjadala wa katiba mpya kwa njia zitakazohatarisha amani au kudhoofisha Serikali.

12. Kwa kuwa mchakato wa Katiba mpya ndiyo kwanza unaanza, waislamu tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwani sasa kupitia Katiba mpya tutadai haki zetu zote ikiwemo ya Mahakama ya Kadhi kuwepo katika katiba kama ilivyo nchini Kenya, Nigeria, Ethiopia, Gambia, Zanzibar na hata Uganda.

13. Tunataka Katiba mpya itamke wazi kuwa Tanzania inaamini kuwepo kwa Mungu Muumba, serikali haina dini ila wananchi wake ndio wana dini mbali mbali. Katiba ya sasa haitambui kuwepo kwa Mwenyezi Mungu jambo ambalo linaifanya Tanzania kuwa nchi ya Kikafiri. Katiba za nchi nyingi duniani zimetamka kuamini kuwepo kwa Mwenyezi Mungu na hata baadhi kusema wazi "In God We Trust" – Tunategemea kwa Mungu.

Kama hatuamini kuwepo kwa Mwenyezi Mungu kwa nini watu huapishwa Mahakamani? Kwa viongozi, kwa nini waapishwe kwa kutumia vitabu vya dini, Ikulu na Bungeni na kwa nini kuwepo dua ya kuliombea Bunge? Ni Mungu gani huyo anayeombwa hapo?

14. Tunataka Katiba mpya ya Tanzania iweke mgawanyo wa madaraka kwa uadilifu kwa kutamka wazi kuwa Rais akiwa Muislamu, Waziri Mkuu awe Mkristo na Rais akiwa Mkristo, Waziri Mkuu awe Muislamu kama ilivyo Nigeria na Lebanon ili kuepuka U-dini. Na vivyo hivyo kwa ngazi zote za madaraka mgawanyo uwe nusu kwa nusu.

15. Tunataka iundwe Wizara Maalumu ya Mambo ya dini ili ishughulikie masuala ya dini kuliko kuyaacha kama yalivyo sasa hayana Wizara inayoyashughulikia. Kama mambo ya kipuuzi tu kama vile muziki na maagizo yana Wizara maalum, vipi dini zisiwe na Wizara yao?

16. Tunataka Katiba mpya isiruhusu Serikali kuingia Mkataba wa upendeleo na kundi jamii moja kama ilivyofanya kupitia Makubaliano ya Maridhiano na Makanisa ya Kikristo mwaka 1992, makubaliano ambayo yanatekeleza andiko la Bibilia "Mwenye nacho ataongezewa na asiyekuwa nacho atanyang'anywa hata kile kidogo alicho nacho"(Luka 8 msitari wa 18). Wakristo walikuwa na shule, hospitali, Vyuo vya Ualimu, Vyuo Vikuu n.k huku waislamu wakiwa hawana kitu. Badala ya kupewa Waislamu wasiokuwa na rasilimali hizo wakapewa Wakristo na hivi sasa wanaongezewa kupitia Makubaliano ya Maridhiano kati yao na Serikali.

17. Kwa kuzingatia tamko namba 16 hapo juu, tunaitaka Serikali iache mara moja kutekeleza Maridhiano hayo batili kati ya Serikali na Makanisa na pia ituambie hadi sasa imeshayapa Makanisa ya Kikristo Mabilioni mangapi tangu mwaka 1992? Aidha tunataka watendaji wote wa serikali waliohusika kuandaa na kupitisha Maridhiano hayo ya U-dini wachukuliwe hatua za kisheria kwani huu nao ni ufisadi kama ule wa EPA, Kagoda, Meremeta, Dowans n.k.

18. Sambamba na hilo, tunaitaka Halmashauri ya Jiji la Mwanza ikabidhi kwa waislamu Shule ya Msingi Mbugani (Muslim School) mara moja kama alivyoagiza Rais Mkapa miaka kumi na tano iliyopita. Hali kadhalika tunaitaka Serikali irejeshe shule zote zilizokuwa Muslim Schools ambazo zilitaifishwa wakati waislamu walikuwa na shule chache kulinganisha na Wakristo waliokuwa wakipata misaada kutoka serikali ya Kikoloni na sasa kupitia Makubaliano ya Maridhiano na Serikali tuliyoyaeleza hapo juu.

19. Tunataka Katiba Mpya itamke wazi kuwa Siku ya Ijumaa nayo ni siku ya mapumziko ili waislamu nao waweze kwenda kusali sala ya Ijumaa kwa utulivu pasina kuhofia kufukuzwa kazi au kukosa masomo kama ilivyo sasa ambapo kwenda kusali ijumaa ni fadhila tu. Kama hilo halikubaliki, basi siku zote tatu Ijumaa, Jumamosi na Jumapili ziwe siku za kufanya kazi nusu siku ili sote tuwe sawa. Mkao wa sasa wa mapumziko Jumamosi na Jumapili unaonesha kuwa nchi hii ni ya Kikristo.

20. Tunataka wimbo wa Taifa uliopo ufutiliwe kwa mbali kwani unaonesha wazi Tanzania ni nchi ya Kikristo kwa sababu hakuna asiyejua historia ya wimbo huo kuwa ulianzia Kanisani huko Soweto Afrika ya Kusini. Kwa Kizulu wimbo huo unaitwa "Nkosi Sikeleli Afrika". Pia hakuna asiyejua kuwa upo katika kitabu kiitwacho "Chuo Kidogo cha sala na Maombi cha Kanisa Katoliki". Hata Mashahidi wa Yehova huko Mbeya waliwahi kuukataa.

21. Tunataka Katiba Mpya itamke wazi kuwa Rais akitoka Bara, Raisi wa awamu nyingine atoke Zanzibar ili kuwatendea haki Wazanzibari. Tayari hivi sasa, Tanzania bara imeshatoa Marais mara tatu, Mwalimu Nyerere, Rais Mkapa na Rais Kikwete. Ni Rais Mwinyi tu ndiye aliyetoka Zanzibar kwa hiyo Rais ajaye lazima atoke Zanzibar kutoka chama chochote kile kiwacho.

22. Tunamtaka Rais Kikwete aongoze mchakato wa kuleta Katiba mpya kwa amani, haki, ujasiri, bila woga wala upendeleo wowote. Katu asiruhusu dharau kutoka kwa kiongozi yeyote awe wa kisiasa ndani au nje ya Serikali yake au hata kiongozi wa kidini. Na pale atakapoona mazingira ya nchi hayapo katika utulivu na amani, ni kheri ausitishe mchakato wa Katiba mpya kwani Katiba haiandaliwi katika mazingira ya vurugu, chuki na uhasama kama tuliyo nayo hivi sasa.

HITIMISHO:

Nchi hii ni ya Watanzania wote. Hakuna aliye na haki zaidi ya mwingine. Kama taifa, watanzania tunafanana na watu walio katika merikebu. Hivyo tunapomuona mmoja wetu anataka kuitoboa merikebu yetu, hatupaswi kumwangalia tu atimize azma yake kwani akifanikiwa tutaangamia sote.

Tunawataka watanzania wote kwa makundi jamii yao, vyama vyao, dini zao na tabaka zao mbali mbali kutanguliza mbele maslahi ya taifa kwanza. Aidha tunawataka Maaskofu kuheshimu imani za dini nyingine katika kutekeleza wito wao wa kichungaji. Si lazima umkandamize mwingine asiendelee ili wewe uendelee.

Tukumbuke kuwa hakuna mahali pengine ambapo watanzania wanapategemea kuishi wao na vizazi vyao hivyo tuilinde nchi yetu kwa faida yetu na vizazi vijavyo.

Kama ambavyo waislamu walimlinda Mwalimu Nyerere dhidi ya wakoloni na tukavumilia madhila yote tuliyofanyiwa ili kulinda na kudumisha amani, sasa tunasema wazi wazi kuwa hatutakuwa mhanga wa agenda za Maaskofu na Mfumo Kristo bali tutakuwa tayari kuitetea dini yetu kwa hali na mali.

Waislamu kamwe si wachokozi. Lakini hapa tulipofikishwa na Mfumo Kristo, tunapenda Maaskofu na mwingine yeyote yule aelewe wazi kuwa waislamu nchini Tanzania hivi sasa tuko tayari kufa kuliko kuishi huku tukiiona dini yetu ikidhalilishwa kwani hatuna cha kupoteza- Kwetu ni mawili tu, ima Ushindi Dhidi ya Dhulma au Kuuwawa Tupate Pepo.

Na Mwenyezi Mungu Ndiye Mjuzi na Muweza wa Yote.

Wabillaahi Tawfiiq.

Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi.

4 comments:

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Inahuzunisha kuona waislamu wakijirahisi kutumiwa na mafisadi bila wao kujua. Matatizo ya nchi yetu hayajui dini wala kabila. Hebu nenda kwenye nyumba za kupanga au daladala hata barabarani kwenye misongamano. Hebu angalia tatizo la mgao wa umeme au kufeli kwa wanafunzi watu na bei za vitu sokoni na dukani. Hakuna dini hapa zaidi ya ombwe la uongozi.
Ningewashauri wanaojiita wakristo au waislamu wajihesabu kama watanzania kabla ya hivi vilemba vya ukoko tulivyoletewa na wazungu na waarabu.
Hili tamko ni la kifisadi hata kama litaitwa la kiislamu. Uislamu unapinga sana ufisadi na ujahiri. I
nasikitisha kuona wale wanaojiita viongozi wa kiislamu wakikumbatia ufisadi na ujahiri. Ufisadi huleta ufakhiri ambao mtume aliupinga sawa na ujinga na ukafiri. Je ukafiri ni kusema yule ni kafiri au kutenda sawa na makafiri?
Kuna haja ya kuwaelimisha na kuwaogopa wachumia tumbo wanaotumia dini kutetea upuuzi na ufisadi.

Mbele said...

Shukrani kwa mchango wako. Ni changamoto ya kufikirisha. Kwa kugusia kipengele kimoja tu, ni kwamba unavyosema kuwa Mtume Muhammad alihimiza elimu ni kweli, maana nami nimefanya kautafiti kidogo, nikawa njiani kuandika kwenye blogu hii kuhusu suala hilo. Nitaibandika siku za usoni.

Unknown said...

Kupima imani yako ni kwa thamani kuliko dhahabu.

Kuna haja ya kujikubali halafu Kujiamini.

Kazi ya kutengeneza tabia haiwezi kufanyika kwa siku moja/dakika.

Mbele said...

Kwa mtu kama mimi, ambaye naheshimu uhuru wa watu kujieleza, uzuri wake ni kuwa nafahamu kuwa mtu mmoja akishatoa mawazo yake, sio mwisho wa habari. Na wengine wana yao, ambayo sherti yasikilizwe.

Kwa maana hii, baada ya kuweka hili tamko la wa-Islam, niko tayari kuweka matamko ya wengine pia, iwe ni ya kukubali au kupinga tamko la wa-Islam, kwangu sawa tu, kwani nao wana uhuru na haki hiyo.

Tunapokuwa na uhuru wa namna hii, lazima hatimaye ukweli utajitokeza. Dini zetu, wa-Islam na wa-Kristu, zinatutaka tuwe watafutaji na watetezi wa ukweli.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...