Monday, November 2, 2015

Hifadhi ya Majengo ya Kihistoria

Miezi kadhaa iliyopita, niliposikia kuwa jengo la CCM mtaa wa Lumumba, Dar es Salaam, limebomolewa ili kujengwa jengo la kisasa, nilifadhaika. Niliwazia utamaduni ninaouona hapa Marekani wa kuhifadhi majengo ya kihistoria. Nimeona katika miji wanahifadhi maeneo wanayoyaita "historic districts." Mfano ni picha zinazoonekana hapa, ambazo nilipiga mjini Faribault. Ninaona maeneo haya katika miji mingine pia.

Maeneo ya kihistoria, yenye majengo ya zamani, ni kumbukumbu ya historia ambayo inastahili kuhifadhiwa kwa ajili ya vizazi vijavyo. Vile vile, ni kivutio kwa watalii. Kwa mtazamo huo, nililiwazia jengo la awali la CCM Lumumba. Lilikuwa na umuhimu wa pekee katika historia za harakati za kupigania Uhuru. Ni jengo ambamo TANU ilizaliwa. Ni urithi wetu sote wa-Tanzania.

Sijui ni nani walioamua kulibomoa na kwa nini. Sijui kwa nini hawakutafuta sehemu nyingine ya kujenga hilo jengo la kisasa. Ninafahamu kuwa majengo yanaweza kuzeeka mno yakawa si salama kwa watu kuingia. Papo hapo, ninafahamu kuna aina za ukarabati ("restoration") zinazowezekana na jengo likabaki salama. Sidai kwamba nina sababu zaidi ya hizo nilizotoa, na labda mtu ataweza kusema kuwa sababu zangu ni zile ambazo kwa ki-Ingereza huitwa "sentimental."

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...