Tuesday, November 24, 2015

Kitabu Changu Bado Kiko Maoneshoni

Nimepita tena katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf, kama ilivyo kawaida yangu, kuangalia vitabu vipya, na pia kuangalia vitabu ambavyo maprofesa wa masomo mbali mbali wanapangia kufundisha.

Katika kuzunguka humo dukani, nilipita tena sehemu ambapo vinawekwa vitabu vilivyoandikwa na maprofesa wa chuo hiki. Kabla sijafika kwenye sehemu hiyo, macho yangu yalivutiwa na kitabu change cha Matengo Folktales, ambacho kilikuwa bado kiko sehemu maalum vinakowekwa vitabu ambavyo uongozi wa duka huamua kuvipa fursa ya kuonekana vizuri zaidi kwa kipindi fulani, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii.

Kuna mambo yanayonigusa kila niingiapo katika duka hili la vitabu na maduka mengine ya vitabu popote hapa Marekani. Kubwa zaidi ni jinsi wahudumu wanavyokuwa ni watu makini katika masuala ya vitabu. Wanajua habari za vitabu, na wanaweza kukuelimisha kwa namna mbali mbali. Hawako katika kazi hii kwa kubahatisha au kwa kubabaisha. Wanajua wanachokifanya. Unaweza kuingia katika duka la vitabu hapa Marekani bila mpango wa kununua kitabu, lakini ukianza kuongea na wahudumu, unaweza kujikuta umeelimishwa kuhusu vitabu fulani ukaishia kununua.

Katika haya maduka ya vyuo, nimeona wana huu utaratibu wa kuwa na sehemu ya kuweka vitabu vilivyoandikwa na maprofesa wa vyuo hivyo, na pengine pia vitabu vya watu waliohitimu zamani, ambao huitwa "alumni" (wanaume) au "alumnae" (wanawake). Ni namna mojawapo ambayo taasisi hizo huwatambua na kuwaenzi waalimu na wahitimu. Nami najisikia vizuri kama profesa wa chuo hiki cha St. Olaf kuwa kazi zangu zinatambuliwa, vikiwemo vitabu.

Kwa upande wa biashara, naona kuwa haya maduka ya vitabu ya vyuo vya Marekani yanaonyesha ubunifu wa kibiashara kwa kuweka vitabu vyetu namna hiyo. Mbali  ya wanafunzi, tuna wageni wengi wanaopita hapa chuoni kila siku, wakiwemo wazazi wa wanafunzi, wahitimu wa zamani, na wale wanaokuja kuangalia ubora wa chuo ili wawalete vijana wao kusoma hapa. Duka la vitabu ni sehemu moja muhimu wanamoingia. Humo wanakuwa na fursa ya kununua vitabu vyetu hasa inapokuwa kwamba wamesikia habari zetu. Kwa mfano, duka la St. Olaf limeshauza nakala mia kadhaa za vitabu vyangu.

Hayo ni baadhi ya mambo niliyojifunza katika suala hili ambayo nimeona niyaweke katika blogu yangu, kwa lugha rahisi kabisa. Labda yanaweza kuwa na manufaa kwa vyuo nchini mwangu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...