
Nilifika saa moja jioni, kama nilivyotegemewa, nikakuta sherehe zimeshamiri. Watoto walikuwa katika michezo, na watu wazima walikuwa katika mazungumzo. Baada ya kukaribishwa kuongea, nilijitambulisha kifupi, nikashukuru kwa mwaliko. Nilifurahi kumwona binti mdogo ambaye alikuwa amehudhuria niliposimulia hadithi katika tamsha la Afrifest. Yeye na mama yake, ambaye alikuwa mwenyeji wangu hiyo jana, ndio watu pekee nilowafahamu.

Baada ya kusimulia hadithi ya Chura na Buibui, nilitumia muda kuwauliza watoto mawazo yao kuhusu hadithi hiyo. Hawakusita kujieleza. Sikushangaa, kwani katika uzoefu wangu wa kuwasimulia watoto hadithi hapa Marekani, nimeona kuwa wanapenda kuelezea maoni yao kuhusu tabia za wahusika, maudhui, na kadhalika.
Vile vile, kabla ya kusimulia hadithi ya pili, nilisema kuwa iwapo watoto wanapenda kuendelea na michezo yao wafanye hivyo, na wale ambao wanapenda kusikiliza hadithi nyingine, wabaki. Nilisema hivyo kwa kuona kuwa watoto wengine walikuwa wadogo mno, ambao hupenda kubadili shughuli mara kwa mara. Sio rahisi kuwakalisha wakakusikiliza kwa zaidi ya dakika 20.

Baada ya hapo, nilisema kuwa ninashughulika na kurekodi na kutafsiri hadithi za jadi, nikawaonyesha kitabu cha Matengo Folktales. Mtu mmoja aliuliza iwapo kinauzwa, nami nikamkubalia. Kwa bahati nzuri nilikuwa na nakala za ziada, na watu walizinunua. Sina shaka kwamba watazifurahia hadithi hizo pamoja na uchambuzi wangu.
Safari ya jana nitaikumbuka miaka ijayo. Unaweza kusoma taarifa nyingine niliyoandika katika blogu ya ki-Ingereza.
No comments:
Post a Comment