Sunday, November 8, 2015

Nimealikwa Kusimulia Hadithi

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mama mmoja m-Liberia aishiye hapa Minnesota. Amejitambulisha kwamba tulikutana katika tamasha la Afrifest, akauliza iwapo nitaweza kwenda kusimulia hadithi mjini Maple Grove tarehe 14 mwezi huu, katika sherehe ya kumbukumbu ya kuzaliwa mtoto.

Nilielezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza nilivyosimulia hadithi katika tamasha la Afrifest, hapa na hapa. Nilisimulia hadithi mbili kutoka katika kitabu cha Matengo Folktales. Mama aliyeniletea mwaliko wa tarehe 14 amenikumbusha kwamba mtoto wake na wengine walioshuhudia hadithi zangu katika Afrifest walivutiwa na wanataka nikasimulie tena.

Hii itakuwa mara yangu ya kwanza kusimulia hadithi katika mkusanyiko wa wanafamilia na marafiki zao, katika sherehe ya kifamilia. Nimezoea kusimulia katika vyuo. Nitatumia sehemu ya muda nitakaokuwa nao kuelezea dhima ya hadithi katika jadi za wa-Afrika na wanadamu kwa ujumla, halafu nitasimulia hadithi, na kisha nitawahimiza wasikilizaji kusaidia kuichambua hadithi nitakayosimulia. Ninawazia kusimulia hadithi kutoka Afrika Magharibi, labda Liberia, Senegal, au Burkina Faso, zilizomo katika kitabu cha West African Folktales.

Hadithi za jadi ni hazina yenye mambo mengi, kama vile falsafa, mafundisho kuhusu saikolojia na tabia za wanadamu, kuhusu mema na mabaya. Ziko zinazosikitisha, zinazofurahisha na kuburudisha, na zinazochemsha bongo, kama zile ziitwazo kwa ki-Ingereza "dilemma tales." Zote ni muhimu katika maisha ya wanadamu, kama nilivyojaribu kuelezea katika kitabu cha Matengo Folktales.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...