Showing posts with label Moshi. Show all posts
Showing posts with label Moshi. Show all posts

Saturday, January 24, 2015

Wanachuo wa Gustavus Adolphus Wako Tanzania

Wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus, ambao niliongea nao kabla ya safari yao, walifika salama Tanzania. Wako Tanzania kwa ziara ya kimasomo kwa mwezi moja. Wamekuwa wakiandika kuhusu ziara yao katika tovuti ya chuo chao.

Walitua uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro wakatembelea sehemu kama hospitali ya KCMC na shule ya wasichana ya Maasae. Kisha walienda Iringa, ambako wameshatembelea sehemu kama vile Chuo Kikuu cha Iringa, soko kuu, na hospitali ya Ilula. Wamesafiri hadi Tungamalenga, pembeni mwa hifadhi ya Ruaha, ambapo wamepata fursa ya kutembelea hospitali na kuangalia utendaji kazi wake.

Kwa ujumla, wanachuo hao, kama ilivyo kwa wa-Marekani wengine wanaotembelea Tanzania, wanaifurahia nchi yetu na watu wake. Wanawasiliana na familia zao na marafiki huku Marekani, na kwa namna hii jina la Tanzania linasambaa kwa namna nzuri. Kwa kawaida, ziara za wanafunzi nazienzi kuliko zile za watalii. Kwa vile wanafunzi wanajumuika na wananchi katika mazingira mbali mbali, wanaondoka wakiwa na ufahamu fulani wa jamii yetu kuliko watalii, ambao wanakaa nchini mwetu siku chache tu, wakikimbizwa kutoka kivutio kimoja hadi kingine, hasa Mlima Kilimanjaro, mbuga za wanyama, na fukwe za bahari.

Kwangu ni heshima na furaha kuweza kuchangia maandalizi ya vijana hao, kama ninavyofanya mwaka hadi mwaka, kupunguza matatizo yanayoweza kutokea sababu ya tofauti za tamaduni. Haiwezekani mgeni aelewe kila anachoshudia katika utamaduni usio wake. Hata mimi ilinichukua miaka mingi hadi kuanza kuelewa misingi muhimu ya utamaduni wa Marekani, kama nilivyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na bado ninajifunza. Ndio maana, wanafunzi wanaporejea tena nchini kwao Marekani, tunajitahidi kuongea nao kuhusu yale waliyoyashuhudia kwenye nchi waliyoitembelea, ili wawe na ufahamu zaidi.

Monday, May 23, 2011

Maktaba ya Mkoa, Kilimanjaro

Tarehe 3 Agosti, mwaka jana, nilikuwa mjini Moshi nikiwa na hamu ya kuufahamu zaidi mji huo. Lengo langu moja lilikuwa kuiona maktaba ya mkoa, kwani nilikuwa sijawahi kufika hapo.

Haikuwa vigumu kufika mahali hapo. Niliingia ndani nikaona kuwa ni maktaba yenye hali nzuri kwa ujumla, kwa upande wa vitabu na majarida, nikifananisha na maktaba kadhaa nilizoziona sehemu zingine za nchi.


Kwa kawaida, ninapoingia katika maktaba za Tanzania, nimezoea kuwaona zaidi wanafunzi. Katika maktaba ya Moshi, niliwaona watu wazima kadhaa wakisoma. Sijui kama hii ndio kawaida katika maktaba hii, lakini niliguswa na jambo hilo.

Kila maktaba duniani, hata kama ni bora namna gani, inahitaji vitabu na majarida mapya muda wote, pamoja na tekinolojia na vifaa vya kisasa vya kupatia maandishi na taarifa. Na ndiyo changamoto kwa maktaba za Tanzania. Nimeona niweke hii taarifa fupi na picha kwenye blogu yangu, ili wengine wapate angalau fununu kuhusu hii maktaba ya Moshi.

Thursday, February 3, 2011

Mji wa Moshi, Tanzania

Moshi ni mji maarufu kaskazini mwa Tanzania, chini ya Mlima Kilimanjaro. Siufahamu sana mji huu, ingawa nimepita hapo mara kadhaa, na hata kulala, mara mbili tatu.






Kama ilivyo katika miji mikubwa ya Tanzania, Moshi kuna hoteli nzuri za kufikia wageni. Wakati moja nililala katika hoteli hii hapa kushoto.









Moshi ni maarufu kwa usafi. Wa-Tanzania wanajua kuwa uongozi wa Moshi una sheria kali kuhusu usafi. Hapo kushoto nipo kituo cha mabasi, pasafi kama vile pamepigwa deki. Nilikuwa safarini baina ya Arusha na Dar es Salaam. Nimechoka, shaghalabaghala; msafiri kafiri na kitabu changu cha Under Kilimanjaro.

Tangu mara yangu ya kwanza kuingia mjini Moshi, nilivutiwa na msikiti unaoonekana kushoto, ambao uko pembeni mwa kituo cha mabasi.







Wakati mmoja nilikuwa Moshi na wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado, niliowaleta nchini kuwafundisha kuhusu mwandishi Ernest Hemingway alivyosafiri nchini mwetu akaandika juu yake. Niliwapeleka hadi Chuo cha Mweka, kinachoonekana kushoto. Kiko nje kidogo ya mji.

Ninapokuwa katika mji wowote napenda kujua maktaba ilipo. Hapo kushoto ni maktaba ya mkoa. Niliingia ndani, nikaona ilivyo nadhifu. Ina majarida na vitabu kiasi cha kuridhisha, nikifananisha na maktaba nilizoziona mikoani Tanzania. Nilivutiwa kuwaona watu wakisoma, sio watoto wa shule tu, kama ilivyo kwenye maktaba zingine.

Nilitembea kutoka Lutheran Uhuru Hostel kuelekea barabara kuu itokayo Arusha, nikaiona hoteli hii inayoonekana kushoto. Nilivutiwa na tangazo la mchemsho, ingawa sikupata kuingia ndani. Hamu ya kuingia nilikuwa nayo, kwa mategemeo ya kupata chakula cha ki-Chagga. Ni suala muhimu la kuzingatiwa siku za usoni, panapo majaliwa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...