Saturday, March 4, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilikwenda Minneapolis, na wakati wa kurudi nilipitia Apple Valley nikaingia katika duka la Half Price Books. Kama kawaida, nilitaka kuona vitabu mbali mbali, lakini nilikuwa hasa na dukuduku ya kuona kama kuna vitabu juu ya Ernest Hemingway.

Kwa hivyo, nilivyoingia tu dukani, nilienda moja kwa moja kwenye sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway, yaani vilivyoandikwa naye au juu yake. Tofauti na siku zingine, leo nilikuta vitabu vichache, na vyote ni vile alivyoandika Hemingway mwenyewe. Nilikiona kitabu ambacho sikumbuki kama nimewahi kukiona kabla, The Fifth Column and Four Stories of the Spanish Civil War, nikakiangalia.

Niliona kuwa "The Fifth Column" ni tamthilia, ambayo sina katika maktaba yangu. Papo hapo nilihisi kuwa hadithi zilizomo katika kitabu ziko katika kitabu cha The Complete Short Stories of Ernest Hemingway, ambacho ninacho. Nimethibitisha hivyo baada ya kuja nyumbani.

Nilipotoka sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway, nilienda sehemu ambapo sikosi kuangalia, kwani hapo vinawekwa vitabu ambavyo vinauzwa kwa bei ndogo sana. Kama kawaida, niliviangalia vitabu vingi, nikaamua kuchukua kitabu cha Gulliver's Travels cha Jonathan Swift.

Hii nakala ya Gulliver's Travels niliyonunua ni toleo la andiko halisi la Swift, si toleo lililorahisishwa. Jambo hilo lilinivutia. Jambo jingine ni kuwa kuna utangulizi ulioandikwa na Jacques Barzun, mwandishi ambaye maandishi yake nimeyafahamu tangu miaka ya themanini na kitu nilipokuwa ninasoma katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison. Katika nakala hii, kuna pia michoro aliyochora Warren Chappell.

Thursday, March 2, 2017

Nimemsikiliza Angela Davis Leo

Leo hapa chuoni St. Olaf tumepata fursa ya kutembelewa na Angela Davis, profesa na mwanaharakati maarufu. Kwangu imekuwa siku ya kumbukumbu. Mara ya kwanza kumsikiliza Angela Davis ni siku alipotoa mhadhara Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1974, kama sikosei. Nilikuwa mwanafunzi na ninakumbuka jinsi mwanaharakati huyu mrefu mwenye Afro kubwa kichwani alivyotusisimua kwa hotuba yake katika ukumbi wa Nkrumah.

Leo ameongelea hali ya ulimwengu kwa kuzingatia majanga yanayotokana na mfumo wa ubepari na mikakati ya kukabiliana yao.  Hotuba yake hii hapa:
https://www.stolaf.edu/multimedia/play/?e=1816

Monday, February 27, 2017

Mahojiano: Beca Lewis na Joseph Mbele

Miezi michache iliyopita, jirani yangu mmoja, mama Mmarekani, aitwaye Merrilyn, ambaye ni mpiga debe wa maandishi na shughuli zangu za uelimishaji, alimwelezea habari zangu rafiki yake aishiye Ohio. Halafu alimpelekea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wakati huo huo, alituunganisha kupitia mtandao wa Facebook.

Beca Lewis, nilikuja kufahamu, ni mwandishi, mwelimishaji, na mmiliki na mwendeshaji wa kituo cha mawasiliano kiitwacho The Shift. Kutokana na alivyomsikia rafiki yake Merrilyn na kutokana na kusoma kitabu changu, Beca Lewis aliniuliza kama ningekubali kufanya mahojiano naye. Nilivyokubali, tulipanga siku, tukafanya mahojiano tarehe 14 Februari, saa tano asubuhi.

Leo, Beca Lewis ameyaweka mahojiano yetu hewani, nami nayaleta hapa katika blogu yangu:
http://theshift.com/podcast/every-culture-is-weird-and-wonderful/

Sunday, February 26, 2017

Mpiga Debe Wangu Kutoka Liberia

Nina jadi ya kuwatambulisha wasomaji na wapiga debe maarufu wa vitabu vyangu katika blogu hii. Ninafanya hivyo ili kuwashukuru, nikizingatia kuwa wanachangia mafanikio yangu kwa jinsi wanavyoupokea mchango wangu.

Leo ninapenda kumtambulisha Charles Chanda Dennis, raia wa Liberia ambaye anaishi hapa Marekani, jimbo la Minnesota. Huyu ni mtu maarufu, hasa katika jamii ya wa-Afrika na wa-Marekani Weusi. Ni mtangazaji na mwendeshaji wa kipindi kiitwacho African Roots Connection katika KMOJ Radio.

Sikumbuki ni lini nilifahamiana na Charles, lakini nadhani ni miaka karibu kumi iliyopita. Aliwahi kunialika kama mgeni katika kipindi chake tukahojiana juu ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wiki chache zilizopita, alinialika tena, tukafanya mahojiano marefu na ya kina ambayo unaweza kuyasikiliza hapa:

https://www.dropbox.com/home?preview=Story+Telling.mp3

Miaka yapata mitano iliyopita, Charles alialikwa na wanafunzi hapa chuoni St. Olaf kutoa mhadhara juu ya historia ya mahusiano na harakati za watu wa asili ya Afrika. Nilihudhuria mhadhara ule. Charles alithibitisha kuwa ni msomi wa uhakika, mwenye uwezo mkubwa wa kuchambua mambo. Anafahamu vizuri njia waliyopitia watu weusi barani Afrika na nje ya Afrika, hasa Marekani.

Alivyonialika kwenye mahojiano safari hii, hatukuongelea angenihoji kuhusu nini hasa, bali nilihisi kuwa alitaka kufuatilia masuala ambayo ninashughulika nayo katika jamii, kama mwalimu na mtoa ushauri kuhusu tamaduni. Niliguswa na masuali yake, kama inavyosikika katika ukanda wa mahojiano niliyoweka hapa juu.

Niliguswa kwa namna ya pekee jinsi Charles alivyonitambulisha kwa wasikilizaji, akinipigia debe kwa bidii na kuwahamasisha watu wasome Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ninamshukuru kwa hilo, nikizingatia umaarufu wa kipindi chake cha African Roots Connection na KMOJ Radio kwa ujumla.

Saturday, February 25, 2017

Tafsiri Yangu ya "A Time to Talk" (Robert Frost)

Leo nimetafsiri shairi fupi la Robert Frost, "A Time to Talk." Hili ni shairi nililolisoma kwa mara ya kwanza miaka mitatu iliyopita, baada ya binti yangu Zawadi kuninunulia kitabu cha mashairi ya Frost, Robert Frost: Selected Poems. Kama nilivyoelezea katika blogu hii, nilikuwa nimelazwa hospitalini mjini Minneapolis, na binti yangu, kwa kujua ninavyopenda vitabu, alininunulia hiki kitabu kinisaidie kukabili hali niliyokuwemo.

Shairi hili la "A Time to Talk" lina mawaidha mazito kuhusu maisha. Linatukumbusha umuhimu wa uungwana na ukarimu katika mahusiano yetu binadamu. Tuache fikra ya kwamba hatuna muda wa kujumuika na wenzetu, kujuliana hali, na kadhalika. Robert Frost anavyoelezea mambo katika shairi hili ananikumbusha maisha ya vijijini, ambayo niliishi tangu utotoni. Kusalimiana ni wajibu, na watu hutumia muda kujuliana hali.

Bila shaka, Frost anaukosoa utamaduni wa ubinafsi, na utamaduni wa kila mtu na maisha yake. Anaikosoa hali ambayo wanafalsafa kama Karl Marx na wafuasi wake wameiongelea vizuri kwa kutumia dhana ya "alienation." Anavyoongelea kuhusu kuwa na muda wa kuongea na wenzetu, ninaona kuwa Frost anaikejeli jamii ambayo imejiaminisha kuwa muda ni hela ("time is money"). Ninavyosema hayo mambo yanayohusu utamaduni, kama yalivyoelezwa katika shairi hili, ninakumbuka nilivyoyaelezea katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa kumalizia, napenda nirudie jambo ambalo ninalitamka daima. Kutafsiri kazi ya fasihi ni shughuli ngumu yenye mitego na vipingamizi vingi. Nilivyojaribu kulitafsiri shairi la Frost, simaanishi kuwa tafsiri yangu ndio kilele cha ufanisi. Msomaji makini anayezifahamu vizuri sana lugha za ki-Ingereza na ki-Swahili, na sio lugha tu, bali lugha ya kifasihi, bila shaka ataona vipengele ambayo vingeweza kuboreshwa. Kwa mfano, katika mstari wa pili, utatafsirije "a meaning walk," ili uziwasilishe kwa ki-Swahili dhana zilizomo katika huo usemi wa ki-Ingereza?
------------------------------------------------------------------------------------------------------------

A TIME TO TALK (Robert Frost, 1874-1963)

When a friend calls to me from the road
And slows his horse to a meaning walk,
I don't stand still and look around
On all the hills I haven't hoed,
And shout from where I am, What is it?
No, not as there is a time to talk.
I thrust my hoe in the mellow ground,
Blade-end up and five feet tall,
And plod: I go up to the stone wall
For a friendly visit.

MUDA WA MAONGEZI

Rafiki anaponiita kutoka barabarani
Huku akipunguza kwa makusudi mwendo wa farasi wake,
Sisimami tu na kuangalia huko na huko
Kubaini idadi ya vilima ambavyo bado sijalima
Na kisha kupaaza sauti pale nilipo, Vipi?
Hapana, hapana kwani kuna muda wa kuongea.
Nasimika jembe langu katika ardhi tepetepe,
Ubapa wa jembe ukiwa juu futi tano toka ardhini,
Na ninatembea taratibu: ninaelekea kwenye ukuta wa mawe
Kukutana na rafiki.

Friday, February 24, 2017

Ninafurahia Kusoma "Eugene Onegin"

Siku chache zilizopita, niliandika kuwa utungo wa Pushkin, Eugene Onegin, ni mtihani. Madhumuni ya kuandika taarifa ile ilikuwa ni kujiwekea kumbukumbu ya usomaji wangu, sio kufanya uchambuzi au tathmini ya utungo. Nilivyotaja dhana ya mtihani, nilimaanisha kuwa utungo huo unahitaji tafakari ya dhati kuelewa vizuri. Wazo hilo lilijengeka akili mwangu wakati nasoma sura ya kwanza ya Eugene Onegin.

Lakini lazima nikiri pia kuwa kuna beti ambazo hazihitaji juhudi kubwa kuzielewa. Kwa kuwa ninasoma tafsiri, siwezi kujua kama ugumu unatokana na utungo wa asili au tafsiri. Kwa pamoja, ingawa ni tafsiri, hizi beti zote zinavutia kwa ukwasi wa sanaa. Mfano ni beti mbili za mwanzo wa sura ya pili ya Eugene Onegin:

They bored Onegin past all measure
These woodlands, though a charming spot.
A friend of innocent, sweet pleasure
Might well thank Heaven for this plot.
The lonely manor found protection
From wind in hills, and in reflection
It danced upon the brook below.
The distant meadows' blurry glow
Was gold from untold blooms collected.
Far hamlets glistened through the air,
And flocks sought pasture here and there.
A garden, grand but long neglected,
Was choked with weeds grown thick and tight:
Fine shelter for a dreamy sprite.

The stately manse had been erected
As manses ought to be: to last.
'Twas solid, tranquil, well-protected:
A tasteful tribute to the past.
The rooms were high and overawing,
And in the drawing-room, some drawing --
Tsarina, tsar -- graced every tall
And plushly damask-covered wall.
The ovens featured flow'ry tiles.
Although this sounds passe today,
The reason why, I can't quite say.
At any rate, to all such styles
The squire was equally undrawn:
At old rooms, new rooms, he'd just yawn.

Katika beti hizi, tunaona kuwa Onegin, ambaye ndiye mhusika mkuu, ni mtu wa ajabu. Mazingira ambayo yangemvutia binadamu mwingine, yeye hayamshitui, wala haoni mvuto wake. Mazingira haya yanaelezwa kwa mtindo unaonikumbusha mkondo wa fasihi uitwao "Romanticism," kama inavyodhihirika, kwa mfano, katika shairi la William Wordsworth, "Lines Composed a Few Miles Above Tintern Abbey," ambalo linaanza hivi :

Five years have past; five summers, with the length
Of five long winters! and again I hear
These waters, rolling from their mountain-springs
With a soft inland murmur.--Once again
Do I behold these steep and lofty cliffs,
That on a wide secluded scene impress
Thoughts of more deep seclusion; and connect
The landscape with the quiet of the sky.

Pushkin alifahamu fasihi za mataifa mbali mbali, kama nilivyogusia katika blogu hii.
Hata hao waandishi wa mkondo wa "Romanticism" aliwafahamu. Kwa mfano, katika sura ya pili ya Eugene Onegin, kwa mfano, Pushkin anawataja Goethe na Schiller, waandishi maarufu wa Ujerumani.

Tuesday, February 21, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Fundamentals of Tawheed"

Leo nilikuwa mjini Minneapolis. Baada ya shughuli zangu, niliamua kwenda kwenye duka la vitabu vya dini ya Uislam liitwalo Akmal Bookstore. Niliwahi kulitembelea duka hilo, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Kama nilivyoona mara ya kwanza, duka hili lina vitabu vingi vya Uislam. Leo nilitumia muda kuvipitia. Hatimaye niliamua kununua The Fundamentals of Tawheed: Islamic Monotheism, cha Dr. Abu Ameenah Bilal Philips. Huyu nilifahamu habari zake tangu miaka kadhaa iliyopita. Alizaliwa Jamaica, lakini alikulia Canada, ambako alisilimu mwaka 1972. Nimesikiliza hotuba zake mtandaoni. Ni mmoja wa watu wanaosifika kwa ufahamu wao wa dini ya Uislam.

Kama nilivyowahi kuandika tena na tena katika blogu hii, ninasoma vitabu vya Uislam na dini zingine kwa ajili ya kujielimisha, sio kwa ajili ya kubadili dini. Nina dini yangu, na nitabaki hivyo. Ninaiheshimu dini yangu, na ninaziheshimu dini za wengine. Ninategemea wengine nao wafanye hivyo, vinginevyo sisiti kuwakabili kwa hoja.

Vile vile, kwa kuwa ninafundisha kozi niliyoitunga iitwayo Muslim Women Writers, na mara kwa mara katika kozi zingine za fasihi ninafundisha maandishi ya wa-Islam, ni muhimu nijielimishe juu ya Uislam. Mwalimu wa somo lolote ana wajibu wa kujielimisha daima. Katika kufundisha tunachambua mambo, hatufundishi kama wafanyavyo katika nyumba za ibada, kwa lengo la kuimarisha imani ya dini au kuwavuta watu wawe waumini wa dini. Darasa langu si kanisa au msikiti. Hoja zozote zinakaribishwa na kutafakariwa kwa uhuru kamili, hata zile zinazokosoa au kupinga dini.

Kwa mtazamo wangu, kila mtu ana wajibu wa kujielimisha kuhusu dini za wengine. Kujielimisha kuhusu dini mbali mbali ni sawa na kujielimisha juu ya tamaduni mbali mbali. Ni hatua muhimu katika kujenga maelewano duniani, kama ninavyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...