Thursday, September 11, 2014

Kitabu Kimeingia Katika Chuo Kikuu cha Cincinnati, Marekani

Pamoja na mengine yote, blogu hii ni mahali ninapohifadhi kumbukumbu za shughuli zangu mbali mbali, hasa zile ninazofanya katika jamii, nje ya chuo ninapofundisha. Kumbukumbu hizi ni pamoja na taarifa kuhusu namna vitabu vyangu vinavyotumika katika jamii.

Miezi kadhaa iliyopita, niliona taarifa mpya, ila sikupata fursa ya kuiweka katika blogu hii. Taarifa yenyewe ni kuwa kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimependekezwa kwa wanafunzi katika chuo cha matibabu cha Chuo Kikuu cha Cincinnati kilichopo katika jimbo la Ohio, hapa Marekani.

Profesa wa programu ya kupeleka wanafunzi Ghana, Dr. Jason Blackard, ambaye picha yake nimeiweka hapa kushoto, ndiye aliyekipendekeza kitabu hiki--pamoja na vingine vitatu--akiwataka wanafunzi kuwa kila mmoja achague kitabu kimojawapo, akisome, halafu aandike ripoti fupi kielezea aliyojifunza. Taarifa hizi zimo katika "syllabus" yake ya programu hiyo ya Ghana.

Simfahamu profesa huyu, na wala hatujawahi kuwasiliana. Ningekuwa na mawasiliano naye, ningependa kujua alizipataje taarifa za kitabu hiki. Najua taarifa ziko tele mtandaoni, lakini najua pia mara kwa mara watu hupata taarifa kutoka kwa wenzao waliokisoma kitabu. Kwa vile nina dukuduku ya kujua, huenda nikawasiliana na profesa huyu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...