Sunday, September 14, 2014

Wa-Kenya Walitia Fora Tamasha la Afrifest

Tarehe 2 Agosti, lilifanyika tamasha la Afrifest, katika mji wa Brooklyn Park, Minnesota. Tamasha hili hufanyika kila mwaka, likijumuisha wa-Afrika na watu wenye asili ya Afrika waishio Marekani, visiwa vya Caribbean, America ya Kati na Kusini, na sehemu zingine, na pia watu wasio wa-Afrika au wa asili ya Afrika. Wote hao hushiriki, kwa lengo la kufahamiana, kuelimishana, na burudani.

Tamasha huanzia siku moja kabla, jioni, kwa burudani ya muziki, maonesho ya mavazi na kadhalika. Hivyo ndivyo ilivyokuwa tarehe 1 Agosti. Siku inayofuata, tamasha hufanyika nje uwanjani. Kunakuwepo na mabanda ya wafanya biashara, pia watoa huduma mbali mbali. Kunakuwepo muziki, michezo ya watoto, na mechi ya soka. Ndivyo ilivyokuwa mwaka huu kule Brooklyn Park.

Mwaka huu, wa-Kenya walijitokeza kwa wingi kuliko wa-Afrika wa nchi nyingine yoyote. Palikuwa na meza ambapo paliwekwa bidhaa na vitu mbali mbali kutoka Kenya. Bendera ya Kenya ilipepea siku nzima. Ilifurahisha kuona wenzetu walivyoonyesha umakini katika kuitangaza nchi yao.

Jambo hili lilitajwa katika mkutano wa Bodi ya Afrifest Foundation. Mimi mwenyewe nilikuwa na meza ambapo nilikuwa nimeweka vitabu na machapisho yangu mengine. Kati ya watu waliofika hapo mezani walikuwepo wa-Kenya.

Mimi na binti zangu tunakumbuka, kwa mfano, jinsi kijana mmoja alivyofika hapo mezani, akaongea nasi kwa ki-Swahili. Alionekana kijana wa kawaida tu, nasi tulidhani ni mmoja wa wale wanaotaka kuelewa shughuli zangu, kuhusu vitabu vyangu, na kisha wanaenda kwenye meza au mabanda mengine. Bila sisi kutegemea, alinunua vitabu vitatu kabla ya kuondoka.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...