Monday, September 22, 2014

Maandamano ya CHADEMA, Bunge la Katiba, na Polisi

Kwa muda wa siku kadhaa, tumesikia kuhusu azma ya CHADEMA kufanya maandamano katika nchi nzima kupinga vikao vinavyoendelea Dodoma kwenye Bunge la Katiba. CHADEMA inasema kuwa kuendelea kwa vikao hivi ni ufujaji wa fedha za wananchi.

Sehemu mbali mbali za nchi, polisi wamekuwa wakifanya juu chini kuzuia maandamano hayo kwa sababu hii au ile. Walioko kwenye hilo Bunge, polisi, na waziri mkuu Mizengo Pinda, wanaendelea kudai kuwa vikao hivi vya Bunge ni halali kwa mujibu wa sheria.

Wazo hili limenifanya nami niandike kifupi mtazamo wangu. Kama raia wa Tanzania, ninayo haki sawa na raia wenzangu, kutoa maoni kuhusu suala hilo na masuala mengine yanayohusu nchi yetu. Wale wanaodhani kuwa kwa vile ninafanya kazi Marekani, na nimekaa huku kwa miaka mingi, basi nimechukua uraia wa Marekani, napenda kuwaambia kuwa dhana hii haina ukweli wowote.

Sijawahi kuwazia kuchukua uraia wa Marekani wala nchi nyingine yoyote. Kwa hivi, nina haki sawa na m-Tanzania aishiye Dar es Salaam, Korogwe au Tunduru kujiingiza katika masuala yanayohusu nchi yetu. Nina haki ya kupigania haki Tanzania, ninapoona haki inakiukwa.

Hii hoja kwamba vikao vinavyoendelea Dodoma ni halali kisheria siipingi. Lakini ni sherti tuzingatie pia kuwa kama ni sheria tu, hata utawala wa makaburu ulikuwa umejengeka katika misingi ya sheria. Ndio maana, waliopinga ukaburu, yaani ANC, PAC, na wengine; akina Nelson Mandela, Robert Sobukwe, na wengine, walionekana wahalifu.

Vikao vinavyoendelea Dodoma ni halali kisheria, lakini hoja ya wapinzani, hasa CHADEMA, kwamba vikao hivi ni ufujaji wa hela za wananchi, ni hoja muhimu.  Wao wanaongelea suala la haki na maslahi ya umma. Panaweza pakawa na jambo ambalo ni sawa kisheria, kama ilivyokuwa wakati wa ukaburu, lakini sheria hiyo ikawa haiendani na haki wala maslahi ya umma.

Polisi wa Tanzania wanapozuia maandamano ya CHADEMA ya kupinga vikao vinavyoendelea Dodoma wanafanya kosa. Kuendelea kwa vikao sio sababu ya kuwazuia watu kutumia uhuru na haki yao ya kuandamana kwa amani.

Polisi wanaposema vikao vinavyoendelea Dodoma ni halali kisheria watambue pia kuwa wananchi bado wana haki zao, ikiwemo haki ya kuandamana kwa amani. Polisi hawana sababu ya kuhujumu haki hiyo, kama wanavyofanya.

Polisi wanapaswa wazingatie kuwa katika nchi yoyote inayoheshimu haki za binadamu, wajibu wa polisi ni kuweka ulinzi kwenye mikutano na maandamano ya amani, ili kuhakikisha kuwa wahusika wanayo fursa kamili ya kutumia haki yao ya kukutana na kuandamana kwa amani. Huu ndio ustaarabu.

Inasikitisha kuwa mambo yanaenda kinyume Tanzania, kwani tumefikia mahali sasa ambapo polisi wamejitwalia jukumu la kutoa vibali vya mikutano na maandamano. Hiyo sio kazi yao. Hawana wadhifa wa kuingilia uhuru na haki ya watu ya kukutana na kuandamana kwa amani. Ila wana wajibu wa kulinda amani kwenye mikutano na maandamano.

Kinachokubalika ni kimoja, kwamba wanaoandaa wawafahamishe polisi kabla ya mkutano au maandamano kwa mujibu wa sheria, ili polisi waende wakaweke ulinzi. Kama kuna watu wanataka kuvuruga mikutano au maandamano, ni wajibu wa polisi kuwashughulikia hao wavurugaji, sio kuwashughulikia wanaokutana au kuandamana kwa amani.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...