Sunday, September 7, 2014

Ninasoma "Shalimar the Clown," Riwaya ya Salman Rushdie.

Salman Rushdie ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa wanaoandika katika ki-Ingereza. Kwa uandishi wake, amepata tuzo zinazoheshimika sana, kama vile "Booker Prize."

Mimi ni mwalimu wa fasihi ya ki-Ingereza. Mara moja moja ninafundisha kozi ya "South Asian Literature," yaani fasihi ya Asia ya Kusini. Katika kozi hii, ninafundisha maandishi ya watu kama Rabindranath Tagore, R. K. Narayan, Raja Rao, Mulk Raj Anand, Anita Desai, Michael Ondaatje, na Salman Rushdie.

Haiwezekani kusoma au kufundisha maandishi yote. Vile vile, kazi mpya za fasihi zinaendelea kuchapishwa. Kwa hivi, kila ninapofundisha kozi ya namna hii, najua kuwa katika orodha yangu kuna waandishi ambao hawamo. Kuna kazi muhimu za fasihi ambazo hazimo. Huu ndio ukweli, ingawa haupendezi.

Uchaguzi wowote wa waandishi au maandishi ambao ninafanya kwa kufundishia katika muhula fulani wa masomo una utata na unazua masuali. Nilipofundisha kozi ya "South Asian Literature" kwa mara ya kwanza, Salman Rushdie hakuwemo. Nilijiuliza kama hii ni sahihi.

Hatimaye, nilianza kutumia maandishi ya Rushdie. Nilianzia na riwaya yake maarufu ya Midnight's Children. Hii sio riwaya rahisi kuisoma, lakini wanafunzi wangu nami tulifanya bidii tukaimaliza. Salman Rushdie anaandika ki-Ingereza ambacho kina mvuto wa pekee, ingawa sio rahisi, kwa mbinu za kila aina. Anadhihirisha ufahamu mkubwa wa ki-Ingereza, falsafa, fasihi, dini, siasa, na tamaduni mbali mbali. Msomaji unajikuta katika kazi kubwa ya kufikiri na kukabiliana na chemsha bongo mbali mbali.

Midnight's Children ilinipa hamasa ya kutumia maandishi ya Rushdie. Muhula huu wa masomo ambao ulianza wiki iliyopita, nitatumia riwaya yake ya Shalimar The Clown. Sikuwa nimeisoma riwaya hii, bali nimeanza, katika kujiandaa kuifundisha. Panapo majaliwa, hapo tutakapokuwa tumemaliza kuisoma na kuijadili, nitaandika habari zake katika blogu hii. Ila napenda kutoa tahadhari kuwa dhana ya kumaliza kusoma kazi yoyote ya fasihi sio dhana yenye ukweli. Ingawa tunaitumia dhana hii, tunajidanganya.


No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...