Wednesday, September 3, 2014

Matamasha Ninayoshiriki ni Kama Shule

Matamasha ninayoshiriki ni muhimu. Ni kama shule. Ninabadilishana mawazo na wadau mbali mbali. Kuna ambayo ninawaeleza na kuwaelimisha, na wao kuna ambayo wananieleza na kunielimisha. Kuna masuali na majibu, au angalau maelezo, kwa upande wao na wangu.

Hapa kushoto naonekana niko katika mazungumzo mazito na jamaa mmoja kutoka Liberia, aitwaye Ahmed. Tumefahamiana kwa miaka kadhaa. Hapo tulikuwa katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park.



Ninapata fursa ya kukutana na watu wa aina aina. Hapa kushoto niko na mama mmoja ambaye alionekana mkimya, lakini alikuwa na dukuduku ya kujua moja mawili. Ilikuwa katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park.









Hapa kushoto nilikuwa katika mji wa Brooklyn Park, na wa-Marekani Weusi wawili. Huyu aliyekaa pembeni yangu tulikuwa tunafahamiana, lakini huyu mwenye kofia ilikuwa ni mara ya kwanza kukutana. Ilikuwa katika tamasha fulani lililoandaliwa na taasisi ya wa-Afrika, inayoshughulikia masuala ya afya.

Huyu mwenye kofia alikuwa mtu asiye na papara katika kuzungumza, bali mwenye tafakari nzito. Unaweza kujionea jinsi tunavyomsikiliza kwa makini.




Shughuli zangu sifanyii Marekani tu. Hapa kushoto nilikuwa Diamond Jubilee Hall, mjini Dar es Salaam, katika tamasha lililoandaliwa na Tripod Media.

Ninaonekana nikiwahamasisha watoto wa shule kuhusu kufanya bidii shuleni,  nikiwapa mfano wangu mwenyewe na hatua niliyofikia maishani. Kuwaambia watoto kama hao kwamba juhudi niliyofanya shuleni imeniwezesha sasa kuwa mwalimu na mwandishi wa vitabu ni namna ya kuwahamasisha wazingatie shule.



Hapa kushoto niko na jamaa wawili, Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam, katika tamasha la Tripod Media nililotaja hapa juu. Kama unavyoona, tuko katika mazungumzo mazito.










Hapa kushoto, katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park, naonekana nikipata mawili matatu kutoka kwa bwana Bolstad, ambaye alizaliwa na kukulia Tanzania, na wazazi wa-Marekani. Ingawa sasa anaishi Marekani, anajisikia kama m-Tanzania, na ki-Swahili anaongea vizuri sana.

Yeye nami tumefahamiana kwa miaka mingi kidogo, na naguswa na jinsi anavyokipigia debe kwa watu mbali mbali kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Watu wa aina yake wanachangia katika kunifanya niwe na ari ya kuandika zaidi, kwa faida ya walimwengu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...