Tutafakari suala tata la kupiga marufuku vitabu. Sijui kama wewe mdau unaafiki suala la kitabu kupigwa marufuku. Mimi huwa nakerwa. Kwa kawaida, kitabu kikipigwa marufuku, huwa nakitafuta ili nikisome. Nimeelezea mtazamo wangu kuhusu suala hili kinaganaga katika kitabu cha
CHANGAMOTO. Hapa naleta mifano miwili ya vitabu vilivyopigwa marufuku Tanzania.

Hapa kushoto ni kitabu cha Hamza Njozi kuhusu
mauaji ya Mwembechai. Wako ambao waliona ni muhimu kitabu hiki kupigwa marufuku. Lakini mimi nilikitetea kwa kila namna, hata Njozi mwenyewe amenishukuru katika kitabu chake kilichofuata.

Kitabu kingine ni
Satanic Verses, cha Salman Rushdie. Wako ambao waliona ni muhimu kitabu hiki kupigwa marufuku. Ayatollah Khomeini wa Iran alitangaza fatwa juu ya Salman Rushdie, kwamba ni ruksa kumwua popote. Tangu mwanzo, watalaam wa dini ya ki-Islam sehemu mbali mbali za dunia walipishana mawazo kuhusu jambo hilo. Wako ambao waliafiki fatwa na wengine walipinga. Chuo Kikuu maarufu cha ki-Islam cha Al-Azhar kilisema asiuawe bali kwanza apate fursa ya kujitetea na kutubu.
Suali langu ni je, unaafiki suala la kitabu kupigwa marufuku? Halafu, kwa ujumla wa-Tanzania hawana utamaduni wa kusoma vitabu. Kuna maana gani kupiga marufuku vitabu Tanzania, wakati hata vikiwepo, watu hawavisomi, na huenda wasitambue kwamba vipo?
Kupiga marufuku vitabu Tanzania ni kuwapa wa-Tanzania umaarufu ambao hawastahili, kwamba ni wasomaji wa vitabu. Nimeongelea kirefu zaidi masuala hayo katika kitabu cha
CHANGAMOTO.
No comments:
Post a Comment