Tuesday, May 29, 2012

Tamko la Askofu Mkuu Kufuatia Vurugu za Zanzibar

TAMKO LA ASKOFU MKUU WA TANZANIA ASSEMBLIES OF GOD, DK.BARNABAS
MTOKAMBALI, KUHUSU MATUKIO YANAYOASHIRIA UVUNJIFU WA AMANI NCHINI.

Kwa kipindi kirefu sasa kumekuwa na mfululizo wa matukio yanayoashiria
uvunjifu wa amani, umoja na utengamano wa taifa letu la Tanzania, haya
ndiyo yanayonisukuma kutoa tamko hili leo ili kuonya na kushauri.

Katika siku za karibu kiumeibuka makundi mbalimbali ya kidini ambayo
yalianza kutoa matamko yenye kuchochea ghasia za kidini Tanzania, na
pengine kauli hizo ndizo zinazotimizwa kwa vitendo hivi sasa.

Miongoni mwa matukio hayo ni:
Januari sita mwaka huu, kikundi kimoja kinachoitwa JUAKATA, kiliitisha
kongamano la kujadili katiba mpya Tanzania, kwa upande wa Waislam.
Katika kongamano hilo lililofanyika kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee,
Dar es Salaam kauli zifuatazo:
1. Lazima Rais ajaye atoke Zanzibar
2. Kukabiliana na ukuaji wa kasi wa dini ya Kikristo
3. Kupinga Muungano ili kuupa nguvu Uislamu
4. Kupigana kufa na kupona kutetea maslahi yao wakati huu wa kuandaa
katiba mpya.

Kauli hizo zilitolewa na Sheikh Nasor Mohameed, kutoka Zanzibar,
ambaye alikuwa mgeni rasmi. Baadaye zikaandaliwa kanda za CD
zilizosambaza ujumbe huo.

Uchunguzi unaonesha kuwa miongoni mwa makanisa yaliyochomwa hivi
karibuni huko Zanzibar ni ya EAGT, Elimu Pentecost na TAG, Anglikana,
Katoliki na FPCT, hivyo kujenga taswira ya ubaguzi wa kidini ambao
kama hautapatiwa dawa unaweza kuligawa taifa la Tanzania kama
ilivyotokea Nigeria na kwingineko barani Afrika.

Hofu yangu ni kuwa, roho hii ya ubaguzi wa kidini ambayo Baba wa Taifa
hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere aliifananisha na dhambi ya kula
nyama ya mtu, imekuwa ikiyatafuna mataifa ya Afrika kama ifuatavyo:

1. Mwaka 2000, vuguvugu la kuanzishwa kwa utawala wa Kiislamu
(Sharia), lilianza kwenye majimbo ya Kaskazini mwa Nigeria, miaka
michache baadaye majimbo kadhaa yakajitangazia sheria hizo na tangu
wakati huo kumekuwa na mapambano yasiyoisha. Takwimu zinaonesha kuwa
katika miaka ya karibuni zaidi ya Wakristo 500 wameuawa kikatili na
makanisa kuchomwa moto.

2. Roho hii imekuwa ikienea kwa kasi katika maeneo mbali mbali ya
Afrika ambapo imelikumba taifa la Mali, majimbo ya kaskazini tayari
yametangaza kujitenga na kuna vuguvugu lenye kuhusisha mapigano ya
silaha.

3. Itakumbukwa kuwa wiki chache tu zilizopita vuguvugu hili la kudai
utawala wa kidini liliibuka nchini Kenya ambapo watu wanaojiita
wanaharakati walianzisha madai ya kutaka eneo la Pwani kujitenga na
Jamhuri ya Kenya na kujitangazia taifa la Kiislamu.

4. Ni wakati huu ambao kundi la Uamsho linalopinga kuandikwa kwa
katiba mpya kabla ya kuitishwa kwa kura ya maoni ili wanzazibar waamue
kuhusu Muungano liliibuka na kuanzisha ghasia Zanzibar ambazo
zimepelekea makanisa kadhaa kuchomwa moto na mali kuharibiwa, huku
watu wa bara wakitishiwa maisha.

USHAURI WANGU KWA SERIKALI NA VIONGOZI WA DINI

Ni wajibu wa kila Mtanzania kutii sheria na mamlaka kwa kuwa zimewekwa/
kuruhusiwa na Mungu, hivyo kuziasi ni Kumuasi Mungu, yaani ni dhambi.
Hivyo kila Mtanzania anastahili kukumbuka wajibu wake wa kutii
mamlaka.

Viongozi wenzangu wa dini wakumbuke kuwa wana wajibu mkubwa katika
jamii, na jamii inawasikiliza hivyo ni vyema wakawa makini katika
matamshi na maelekezo yao ili wasiwe chanzo cha kuchochea vurugu za
kidini na uvunjaji wa amani.

Ni vyema wakati huu wa kuandikwa kwa katiba mpya, kila kikundi
kikafuata utaratibu uliowekwa badala ya kuchochea ghasia ambazo
madhara yake yatawakumba watanzania wote ikiwa ni pamoja na wao
wenyewe watoto na wajukuu zao.

Pia ningependa kuwashauri viongozi wa serikali kusimama imara katika
kusimamia sheria na haki, na kuepuka kauli au vitendo vitakavyofanya
baadhi ya watanzania kudhani kuwa hawatendewi haki.

Ni vema ieleweke kuwa matukio kama haya ya uvunjaji wa amani
yasipodhibitiwa na kukomeshwa haraka yanaweza kuumba chuki ambayo
inaweza kuibua mlipuko mkubwa na machungu kwa wananchi na matokeo yake
yakawa mabaya kwa Taifa zima. Hekima na busara inatufundisha kuwa
tusipoziba ufa tutajenga ukuta.

Ni vyema wenye dhamana ya kuongoza wakakumbuka kuwa wanawajibu mbele
ya Mungu aliyewaweka au kuwaruhusu kuingia madarakani na siku moja
watatoa hesabu mbele zake.

Mwisho, natoa wito kwa watanzania wenzangu tuulinde umoja, amani na
utengamano wa taifa letu, tuikimbie dhambi ya ubaguzi kwa kuwa
tukiiruhusu itatuangamiza sote. Tuliombee taifa letu na kukiwa na
mbegu ya chuki tuimalize kwa njia ya majadiliano na vikao vya pamoja
vinavyohusisha viongozi wa dini zote na serikali pia.

Imetolewa leo 28/05/2012
Na Dk. Barnabas Mtokambali
Askofu Mkuu wa TAG

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...