Saturday, May 5, 2012

The Snows of Kilimanjaro

Wiki hii, nimesoma tena "The Snows of Kilimanjaro," hadithi maarufu ya Ernest Hemingway mwandishi m-Marekani aliyezaliwa mwaka 1899 akajiua kwa risasi mwaka 1960. Baada ya kusoma hadithi kwa makini, nimeangalia tena DVD iliyotokana na hadithi hii, ambamo waigizaji wakuu ni Gregory Peck na Ava Gardner.

Nimefuatilia maandishi na maisha ya Hemingway kwa muda mrefu. Hakuna siku inayopita bila mimi kusoma, kuwazia, au kuongelea habari za Hemingway. Ni mwandishi ambaye amenigusa kwa namna mbali mbali, kuanzia kipaji cha uandishi hadi falsafa yake kuhusu mambo mengi. Nimeunda hata kozi kuhusu mwandishi huyu, kama nilivyoelezea hapa na hapa.

"The Snows of Kilimanjaro" ni hadithi mojawapo maarufu kuliko zote katika lugha ya ki-Ingereza. Inamhusu mwandishi aitwaye Harry, ambaye tunamwona mbugani karibu na Kilimanjaro, akiwa anauguza kidonda mguuni, kilichotokana na kuchomwa mwiba wakati akiwinda. Ni kidonda kibaya, ambacho kinaonekana kutishia maisha ya Harry. Tunamwona mke wake Harry akifanya kila awezalo kumuuguza Harry, papo hapo akitegemea kuwa itakuja ndege ya kumchukua na kumpeleka hospitalini.

Katika hali hiyo ya kunyemelewa na kifo, Harry anakumbuka maisha yake na safari zake Ulaya na sehemu mbali mbali zingine. Anajutia jinsi alivyochelewa au kushindwa kuandika kuhusu mambo mengi aliyoyashuhudia na kuyafanya maishani, na sasa anafahamu kuwa hataweza kuandika tena. Jambo hilo linamwongezea msongo wa mawazo. Yeyote anayefahamu habari za Hemingway ataona kuwa Hemingway mwenyewe, katika miaka ya mwisho ya maisha yake, alisongwa na mawazo ya aina hiyo hiyo, kwa kutambua kuwa kipaji chake cha kuandika vizuri kilikuwa kinadidimia.

Katika hadithi ya "The Snows of Kilimanjaro" hatusikii sana habari za Kilimanjaro, ingawa tunajua fika kuwa wahusika wako mbugani karibu na mlima huo. Hemingway alianza hadithi yake kwa utangulizi ambao umekuwa maarufu sana:

Kilimanjaro is a snow-covered mountain 19,710 feet high, and is said to be the highest mountain in Africa. Its western summit is called the Masai "Ngaje Ngai," the House of God. Close to the western summit there is the dried and frozen carcass of a leopard. No one has explained what the leopard was seeking at that altitude.

Ajabu ya chui huyu na masuali anayozua, ni kama kielelezo cha masuali tata yanayojitokeza katika hadithi nzima, kuhusu maana ya maisha, mahusiano baina ya wanadamu, kama vile baina ya wanawake na wanaume, athari za utajiri wa fedha katika maisha, na kadhalika. Pamoja na yote mengine, Hemingway alikuwa mwanafalsafa aliyetafakari sana suala la uandishi na changamoto zake. Hadithi zake nyingi, kama vile Green Hills of Africa na A Moveable Feast, zinafafanua suala hili.

Waliotengeneza filamu hawakufuata kila kipengele au mtiririko kamili wa alichoandika Hemingway. Wameichukulia hadithi ya Hemingway kama kianzio au kichocheo cha ubunifu wao. Pamoja na kwamba wamefanya mabadiliko ya hapa na pale, filamu hiyo inatuwezesha kuona kwa vitendo yale tunayosoma katika hadithi, na pia inatuwezesha kuona taswira za sehemu mbali mbali zinazotajwa katika hadithi.

Kwa upande wetu wa-Tanzania, tungekuwa taifa makini katika kuvithamini vitabu, tungetumia vilivyo maandishi ya watu kama Hemingway kuitangaza nchi yetu. Lakini, jamii yetu ina umaskini wa fikra. Haivithamini vitabu, na matokeo yake ni kama wahenga walivyosema, kwamba kuku wa maskini hatagi. Watakuja wengine, wageni, kuzitumia fursa hizi, na kwa kweli wako ambao wanazitumia.

1 comment:

darkheart2011 said...

You has a great blog. I'm very interesting to stopping here and leaves you a comment. Good work.

Lets keep writing and share your information to us.

Nb: Dont forget to leave your comment back for us.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...