Tuesday, December 9, 2014

Uhuru wa Tanganyika na Ukoloni Mamboleo

Siku hii ya leo, ambayo ni ya kumbukumbu ya siku ambapo Tanganyika ilijipatia Uhuru, nilitaka kuandika makala, "Uhuru wa Tanganyika na Ukoloni Mamboleo." Nilianzza kuandika, lakini nilijikuta naandika insha ndefu, sio makala fupi ambayo nadhani inatakiwa katika blogu. Kutokana na jambo hilo, nimeifuta ile makala na badala yake nimeandika kwa ufupi mambo yafuatavyo.

Uhuru tulipata tarehe 9 Desemba, 1961. Nilikuwa mwanafunzi wa darasa la tatu, na ninakumbuka msisimko, hata kule kijijini kwangu. Waalimu wetu, Charles Kinunda, John Pantaleon Mbonde, na Alois Turuka, walikuwa chanzo kikubwa cha ufahamu wetu wa mambo yaliyokuwa yanatokea.

Kati ya kumbukumbu ambazo haziwezi kutoweka akilini mwangu ni picha ya askari Alexander Nyirenda akiweka mwenge wa Uhuru juu ya Mlima Kilimanjaro. Sambamba na tukio hili la kihistoria ni hotuba ya Mwalimu Julius Nyerere, ambamo alisema:

Sisi tunataka kuwasha mwenge, na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, ili umulike hata nje ya mipaka yetu, ulete tumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo mahali palipo na chuki, na heshima palipojaa dharau.

Mwalimu Nyerere, alifanya kila juhudi kuliongoza na kulielimisha hili Taifa huru, akisema kuwa tunaingia katika mapambano na maadui watatu: ujinga, umaskini na maradhi. Miaka ilivyopita, alifafanua vizuri malengo mengine ya Taifa hili: kujenga jamii ya usawa kwa wote, isiyo na matabaka; jamii yenye kutoa fursa sawa kwa wote, katika nyanja mbali mbali, kama vile uchumi, elimu, na afya; kuhakikisha kila mtu anatimiza wajibu wa kufanya kazi, chini ya kauli mbiu ya "Uhuru na Kazi," kujenga Taifa linalojitambua, kujiheshimu, na kujitegemea, Taifa huru lisilofungamana na upande wowote katika mazingira yale ya "Cold War," Taifa lenye kukaribisha urafiki na nchi yoyote kwa msingi wa kuheshimiana, Taifa ambalo halitamruhusu rafiki kutuchanguia marafiki au maadui, na tuwe mstari wa mbele kuunga mkono harakati za ukombozi Afrika na sehemu zingine duniani.

Hayo ndio yalikuwa malengo muhimu, ambayo Mwalimu Nyerere aliyaelezea katika hotuba zake, makala na vitabu mbali mbali. Alikuwa akienda na wakati, akizingatia mahitaji ya Taifa yalivyokuwa yanajitokeza. Kwa msingi huu, baada ya "Azimio la Arusha," aliendelea kuandika maandishi mengine, kama vile "Mwongozo," "Siasa ni Kilimo," "Elimu ya Kujitegemea," na "Binadamu na Maendeleo."

Hayo yote, tangu enzi za harakati za Uhuru hadi miaka ya mwisho mwisho ya sabini na kitu, yalifanyika chini ya uongozi wa chama cha TANU. Mtazamo na mwelekeo wa TANU ulikuwa wa kuongoza mapinduzi, kufuatana na mazingira ya kihistoria: kwanza ilikuwa kuwaunganisha wa-Tanganyika na kuwaongoza katika kupigania Uhuru, halafu, kuongoza harakati za kujenga ujamaa na kujitegemea.

Mwalimu Nyerere alifahamu fika kwamba Uhuru haukuwa mwisho wa safari. Kulikuwa na haja ya kupambana na urithi wa ukoloni, yaani ukoloni mamboleo na kuleta uhuru wa kweli, unaodhihirishwa na hali ya kujitegemea chini ya uongozi bora.

Miaka ilivyopita, baada ya chama kipya cha CCM kushika hatamu, hali ilikuwa hiyo kwa kipindi cha mwanzo. Lakini, pole pole, mwelekeo huu wa kuwa daima katika harakati za mapinduzi, ulianza kubadilika. Chini ya sera za CCM, kama vile "Azimio la Zanzibar," nchi imeendelea kuzama zaidi na zaidi katika mfumo wa matabaka na ukoloni mamboleo. Kwa lugha rahisi, CCM ni mhujumu wa Mapinduzi.

Ndoto na mategemeo ya Uhuru yametekwa nyara. Pamoja na kwamba tunasherehekea Uhuru tuliojipatia mwaka 1961, tutambue, kama TANU ilivyotambua, kuwa ule haukuwa mwisho wa safari. Enzi za TANU, tulitegemea kuwa tutajenga nchi ambayo iko chini ya mamlaka ya wakulima na wafanyakazi. Lakini, kama nilivyosema hapa juu, tunazidi kuzama katika ukoloni mamboleo. Wakulima na wafanyakazi, pamoja na washiriki wao, bado wana jukumu la kuendeleza harakati za kutafuta Uhuru wa kweli.

2 comments:

Dennis Dotto said...

Very well said ndugu Joseph Mbele. Katu asilani hujakosea kabisa. Nimeona ulivyojitahidi kuyaelezea kwa ustadi mkubwa, na kwa muhtasari (succinctly), maono ya Mwalimu Nyerere bila kupoteza uzito wake hata kidogo, kitu ambacho huwashinda waandishi wetu wengi.

Hata hivyo, binafsi nimependa zaidi ulivyolihitimisha andiko lako kwa kusema " Wakulima na wafanyakazi, pamoja na washiriki wao, bado wana jukumu la kuendeleza harakati za kuutafuta Uhuru wa kweli." Ninakubaliana na hiyo dhana kwa asimilia mia. Hii ni kwa vile ninatambua na kuona dhahiri kabisa kuwa, kwetu sisi Watanzania, kwa sasa hivi huo Uhuru tuliousherekea wiki hii hatunao. Tulionao ni 'Uhuru wa bandia.' Kwa maneno mengine, tumebadili rangi yetu ya wakoloni; kutoka katika makucha ya wakoloni weupe, kwenda kwenye makucha ya wakoloni weusi!

Ama kwa hakika, ni jukumu letu sasa kuanza tena harakati za kujikomboa kutoka katika aina hii ya ukoloni pia. Asante sana Mwalimu, nimelipenda sana hili andiko lako.

Mbele said...

Ndugu Dennis Dotto,

Nakushukuru kwa kutembelea hiki kiblogu changu, kusoma hii makala yangu, na kuweka maoni yako.

Kama nilivyosema, nawe umeliona hilo, nimeandika kwa kifupi. Nina mengi ya kusema kuhusu suala hili, kiasi kwamba ningeweza kuandika kitabu.

Nakutakia kila la heri
kwa msimu huu wa Krismasi, Mwaka Mpya, na daima.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...