Monday, June 27, 2016

Masuali Kuhusu Uislam Kutoka Katika Blogu ya Kimbilia

Nimeshaandika mara kwa mara kuwa blogu yangu hii ni uwanja huru wa fikra, mawazo, na mitazamo. Ninakaribisha mijadala, na hoja za kuchangamsha bongo, wala sijali kama zinawatatiza watu. Ninasimamia uhuru wa watu kutoa mawazo.

Dini ni mada mojawapo ninayopenda kuona inajadiliwa. Wakati wengi wanaamini kuwa tujiepushe na mijadala ya dini, mimi ninasema kuwa mijadala ya dini ni muhimu. Kwa msingi huo, leo ninaleta mada ya dini kwa staili ya pekee.

Siku chache zilizopita, niliona makala juu ya u-Islam katika blogu ya Kimbilia. Ni makala inayoibua masuali mengi juu ya u-Islam. Inastahili kusomwa na kujadiliwa. Kati ya masuala yanayotokana na makala hii ni suala la haki na uhuru wa mtu kuwa na dini, kutokuwa na dini, au kubadili dini. Binafsi, ninatetea uhuru na haki hiyo, kama nilivyotamka katika blogu hii.  Tangazo la kimataifa la haki za binadamu linatambua haki hiyo.

Ningependa kujua kwa nini watu waliojitoa katika u-Islam, kama vile Wafa Sultan, mzaliwa wa Syria, na Ayaan Hirsi Ali, mzaliwa wa Somalia, wanasumbuliwa na kutishiwa maisha yao. Je, huu ni msimamo wa u-Islam, au ni upotoshaji? Ni haki kumwingilia mtu uhuru wake wa kuamini dini aitakayo, au uhuru wake wa kubadili dini au kuishi bila dini? Masuala hayo na mengine yanajitokeza katika blogu ya Kimbilia. Bora tuyatafakari na kuyajadili.

11 comments:

Anonymous said...

Jibu:

THERE SHALL BE no coercion in matters of faith. 2:256 (Asad). Uislamu haujakataza mtu kujitoa katika dini.

Anonymous said...

Kwahiyo kuingia na kutoka mtu halazimishwi.

Mbele said...

Ndugu Anonymous,

Shukrani kwa ujumbe wako. Binafsi, nilifahamu toka zamani kwamba mafundisho ya u-Islam yanapingana kuhusu suala hili. Kwa upande moja, kuna hiyo dhana uliyoleta, kwamba pasiwe na shuruti katika suala la imani, kwamba imani ni suala la hiyari ya kila mtu. Msimamo huo nimeusoma katika maandishi mbali mbali. Mfano mmoja ni huu hapa.

Msimamo unaozingatiwa ni tofauti. Kwa mujibu wa sharia, adhabu ya kuacha u-Islam ni kifo, kama inavyoelezwa katika makala hii.

Suala la hiari na uhuru wa mtu halizingatiwi. Mtu akijitoa katika u-Islam anapachikwa majina ya kihasama. Ingekuwa suala la hiari linazingatiwa, mtu wa namna hiyo angeachwa aendelee kuishi kwa amani na raha zake, sawa na watu wengine. Kadhalika, watu wasio wa-Islam wanapachikwa majina ya kihasama. Haizingatiwi kuwa dini ni hiari ya mtu.

Nimalizie kwa kusema kuwa hata kama mtu hauawi, kule kubambikizwa majina ya kihasama, kama vile "apostate" (kwa ki-Ingereza), "kafiri," na kadhalika ni mashambulizi ("aggression") ya kisaikolojia. Ni kuandaa mazingira ya kumhujumu. Ni kuhalalisha hujuma dhidi yake, na hata kumwua inachukuliwa kama tendo lenye thawabu.

Anonymous said...

1. Nani analichukulia tendo la kuuwa kuwa ni tendo la thawabu? Allah mwenyewe au nani? Thawabu anatoa Allah. Kama kuuwa ni thawabu kwanini Allah asiseme hivyo kwenye Quran?

2. Nani anampachika majina ya kihasama mtu aliejitoa Uislamu? Ni Allah katika Quran?

Unajua tatizo la watu wengine ni kuona Uislamu kuwa ni mawazo ya watu fulani. Uilamu unahitaji watu kusoma kama wanavyosoma elimu nyengine. Kwanini watu watoe judgement bila ya kusoma? Kwanini judgement zitokane na mawazo ya watu? Kama ilivyo kwenye siasa watu wanaotetea misimamo yao kuna watu wanawapinga, serikali zinawafunga na hata kuwaua. Lakini nani mwenye authority katika Uislamu kufanya hivyo? Wanaofanya wanafanya kwa maoni yao hakuna chombo kilichowapa authority ya kufanya hivyo.Sio Uislamu ng'o. Ni watu waliokosa elimu na wanaoendeshwa na maoni yao.

Mbele said...

Ndugu Anonymous

Sijui kama wewe ni mu-Islam au la, lakini napenda kwanza kukumbushia kwamba mafundisho ya u-Islam hayatoki katika Qur'an tu, bali pia katika hadith. Katika jawabu langu hapa juu, nimetaja makala mbili. Hiyo ya pili inasaidia kufafanua suala la kama kuua kumehalalishwa na kama kuna thawabu katika kuuwa huko. Makala hiyo inatuingiza katika Qur'an na pia katika hadith.

Makala hii inatupa angalau kianzio cha kulifahamu suala la uhusiano wa kuuwa na thawabu, kwa kuwa makala hii inatupa ufahamu wa namna Allah anavyohusika katika aina ya uuwaji unaoongelewa. Dhana hii ya kuhusika kwa Allah imo katika Qur'an, katika aya za mwisho mwisho kabla ya kufariki kwa Muhammad. Unaweza kufuatilia suala hili katika makala hii, ambayo inataja vyanzo mbali mbali vya kufuatiliwa pia.

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Japo umeuliza wka kiswahili, nitatoa baadhi ya aya ili wahusika waamue. Pia nisema kuwa Uislam hata Ukristo vilienezwa kwa nguvu na ahadi za uongo na kusadikiza, kwa ncha ya upanga (Uislam) na ndimi za moto (Kwa Uroma. Hata ukiangalia kwa mfano maana ya Uislam yaani kujisalimisha au surrender kwa kiingereza ni baada ya nini? Japo wanaotaka kuwaaminisha watu kuwa uislamu ni dini ya amani hupenda kutafsiri kuslim kama salaam wakati ni kujisalimisha. Leo sitasema mengi.

Quran (4:89) - "They wish that you should disbelieve as they disbelieve, and then you would be equal; therefore take not to yourselves friends of them, until they emigrate in the way of God; then, if they turn their backs, take them, and slay them wherever you find them; take not to yourselves any one of them as friend or helper."
"Kill the unbelievers wherever you find them." Koran 2:191 "Make war on the infidels living in your neighborhood." Koran 9:123 "When opportunity arises, kill the infidels wherever you catch them." Koran 9:5 "Any religion other than Islam is not acceptable." Koran 3:85 "The Jews and the Christians are perverts fight them."... Koran 9:30 "Maim and crucify the infidels if they criticize Islam" Koran 5:33 "Punish the unbelievers with garments of fire, hooked iron rods, boiling water melt their skin and bellies." Koran 22:19 "The unbelievers are stupid urge the Muslims to fight them." Koran 8:65 "Muslims must not take the infidels as friends." Koran 3:28 "Terrorize and behead those who believe in scriptures other than the Qur'an." Koran 8:12 "Muslims must muster all weapons to terrorize the infidels." Koran 8:60

Mbele said...

Ndugu Mhango

Shukrani kwa mchango wako. Nikizingatia kuwa inachukua muda kutafuta na kuandika taarifa kama hiyo uliyoleta, nimeona ni wajibu na uungwana kushukuru. Elimu ni kuelimishana, nawe ni mfano wa kuigwa kwa kuwa si mchoyo wa elimu.

Khalfan Abdallah Salim said...

Prof. Mbele, nini maoni yako kwa mtu msaliti kwa taifa lake? Unaionaje hukumu ya kifo kwa makosa mballimbali hapo Marekani na hata kwetu Tanzania kwa mtu muuaji na msaliti?

Kwanza kabla ya kujadili Uislam na adhabu za makosa, ni vyema ukajihakiki nafsi yako kuwa je unafikiri binadamu anastahili adhabu ya kuuawa? Nani mwenye mamlaka ya kuua? Unaonaje kuwa yule mwenye mamlaka ya uhai i.e Mungu ndiye huyohuyo anapoweka sheria yake kuwa kwa kosa fulani, mtu auwawe. Unaonaje kama ni kitu chako mwenyewe ulichokiuunda mathalani kitabu chako, baada ya kupitwa na wakati ukaamua kukichoma moto?

Maswali haya naona ni muhumu kufikiria.

Mhango,

Unaweza kunukuu vitabu vyote vya dini na ukakutana na mistari kama hiyo lakini haikufanyi kuwa mjuzi wa dini hiyo. Kila dini ina wajuzi wake wanaojua maana na muktadha wa aya husika na matumizi yake katika wakati ule na sasa. Kama msomi, inatarajiwa context iwe inazingatiwa wakati wa mjadala ili wasomaji wanufaike badala ya kupotoshwa na maana tu ya mstari au aya fulani ya Qur'an?

Khalfan Abdallah Salim said...

Prof. Mbele, nini maoni yako kwa mtu msaliti kwa taifa lake? Unaionaje hukumu ya kifo kwa makosa mballimbali hapo Marekani na hata kwetu Tanzania kwa mtu muuaji na msaliti?

Kwanza kabla ya kujadili Uislam na adhabu za makosa, ni vyema ukajihakiki nafsi yako kuwa je unafikiri binadamu anastahili adhabu ya kuuawa? Nani mwenye mamlaka ya kuua? Unaonaje kuwa yule mwenye mamlaka ya uhai i.e Mungu ndiye huyohuyo anapoweka sheria yake kuwa kwa kosa fulani, mtu auwawe. Unaonaje kama ni kitu chako mwenyewe ulichokiuunda mathalani kitabu chako, baada ya kupitwa na wakati ukaamua kukichoma moto au kuamrisha watoto wako wafanye hivyo?

Maswali haya naona ni muhumu kufikiria.

Mhango,

Unaweza kunukuu vitabu vyote vya dini na ukakutana na mistari kama hiyo lakini haikufanyi kuwa mjuzi wa dini hiyo. Kila dini ina wajuzi wake wanaojua maana na muktadha wa aya husika na matumizi yake katika wakati ule na sasa. Kama msomi, inatarajiwa context iwe inazingatiwa wakati wa mjadala ili wasomaji wanufaike badala ya kupotoshwa na maana tu ya mstari au aya fulani ya Qur'an.

Mbele said...

Ndugu Khalfan Abdallah Salim

Shukrani kwa masuali yako. Siwezi kusema nina majibu, bali nina mitazamo, na mitazamo hiyo siichukulii kama dogma, bali ni hatua niliyofikia katika safari ya kujielimisha. Elimu ni safari isiyo na mwisho, ni bahari isiyo na ukomo.

Mtazamo wangu kuhusu masuali yako ni kuwa ninapambanua mambo ya kidunia ("secular") na mambo ya imani za dini. Kwenye mambo ya kidunia, ninaafiki kuwa binadamu ana mamlaka ya kuhukumu. Mtu akiiba au akiua, na tukathibitisha kwa mujibu wa sheria zetu, ninaafiki kitendo cha wanadamu kumwadhibu mtu huyu.

Lakini kwenye mambo ya imani za dini, mtazamo wangu ni kuwa hayo ni mambo ya kumwachia Mungu. Siafiki dhana ya wanadamu kuadhibu au kutekeleza adhabu kwa masuala hayo. Anayefahamu yaliyomo katika nafsi ya mtu, anayefahamu imani ya mtu, ni Mungu pekee. Hata ninavyosoma Qur'an, ingawa bado sijafika mbali, ninaona tena na tena jinsi Qur'an inavyosisitiza kuwa Allah ndiye anayeona yaliyomo nafsini na moyoni mwa binadamu.

Kwa kuzingatia kuwa binadamu hana uwezo wa kuona yaliyomo katika nafsi au moyo wa binadamu mwenzake, ninapinga wazo la binadamu kumwadhibu binadamu mwenzake juu ya masuala ya imani ya dini.

Mimi ni m-Katoliki. Ninafahamu kuwa karne za zamani, Kanisa lilikuwa linawahukumu watu kwa masuala haya ya imani, na kuwaadhibu. Kwa mfano, Kanisa lilitekeleza adhabu ya kifo kwa watu wengi walioshtakiwa kwa kosa la "heresy."

Lakini, miaka ya baadaye na hadi leo, Kanisa halifanyi hivyo. Limetambua makosa na sasa linazingatia kuwa mwenye hukumu ya haki kabisa juu ya masuala ya imani ya dini ni Mungu pekee. Kwa hivyo, m-Katoliki wa leo nikiamua kuacha dini yangu na kusilimu, au nikiamua kujitoa katika dini kabisa na kuwa "atheist," hakuna tishio wala adhabu nitakayopata kutoka kanisani wala kutoka kwa waumini. Hawaruhusiwi kuniadhibu. Wanachotakiwa kufanya ni kuniombea kwa Mungu, aendelee kunibariki na kuongoza njia zangu.

Dunia ya leo si kama ya karne zile za mitume. Leo tuna upeo tofauti kuhusu masuala kama haki za binadamu. Mtazamo wangu ni kuwa sherti twende na wakati. Ninaogopa kuwa tutakuwa tunamkosea Mungu iwapo tunaacha kutumia ufahamu aliotujalia katika mazingira yetu na badala yake tunafuata akili ya watu wa karne za zamani.

Akili na fursa za zama zetu hizi tumepewa ili tuzitumie. Hata misahafu ni lazima tuisome na kuitafsiri kwa kutumia akili yetu ya leo. Huu ndio mtazamo wangu.

Khalfan Abdallah Salim said...

Prof. mtazamo wako juu ya tofauti ya mambo ya kidunia na kiimani unafahamika kwa kuwa si mgeni sana kwangu.

Je unafahamu kuwa Uislam hautofautishi matendo ya wanadamu kuwa ni ya kidunia na kiimani? Uislam unamtazama mwanadamu katika ujumla wake (in totality) na katika mambo yake yote. Mahusiano na Mungu, mahusiano na watu bali mpaka mahusiano na nafsi yake.

Ndio maana inasemwa kuwa Uislam ni mfumo kamili wa maisha na sio imani tu. Hata hivyo, Uislam unamambo ya msingi ambayo Mwenyezi Mungu kwa kupitia maandiko yake na ujumbe wa Mtume wake, hakutaka yabadilike abadan na yapo ambayo wanadamu wanaweza kufikiria namna nzuri ya kufuata mafundisho au sheria fulani katika eneo lao. Mathalan, katika sheria za Uislam, hatuwezi kujadili hukumu ya kuua muuaji aliyethibitishwa, kuwa asiuawe. Tunaweza kujadili namna (methods) ya kumuua ili kutii Sheria aliyoweka na Mungu na kwa mujibu wa zama zetu. Lakini hatuwezi kusema hilo ni la kidunia, wanadunia waamue wenyewe hata kutofuata Sheria ya Mungu, sio la kiimani.

Waislam na hata wakristo, wanaamini kuwa Mungu anamapenzi na wanadamu, anaujuzi zaidi kuliko mwanadamu, ndiye aliyeumba mwanadamu kwa kumpa uhai na akaweka sheria zisimamiwe na watu. Kama imethibitika kuwa Mungu ambaye mwanadamu ni wake, (waislam hawaamini kuwa wanavyuoni au Masheikh ndio watunga sheria, wao ni wafafanuzi wa Sheria n.k) kaweka sheria ya kuuawa kwa anayeua au anayetoka katika Uislam. Hakuna anayeweza kumhoji Mungu au Mtume wake kwa sababu wakati au zama zimebadilika au kuna haki za binadamu kwa kuwa mola ndiye mjuzi na mmiliki na mletaji wa zama. Anayajua yaliopita, yaliopo na yajayo! Hivi tumefikia kumfunza Mungu haki zetu? Yeye hazijui? Haki za binadamu zimefikia kuwa ni sawa kuingiliana waume kwa waume, watu kwa wanyama na pengine zitafika hadi mtu na mtoto wake waoane n.k kweli maarifa ya Mungu ni dhaifu ya maarifa yetu zama hizi chini ya mwamvuli wa haki za binadamu?

Prof. wakati Ukiristo umepitia katika majadiliano makali juu ya hukumu mbalimbali za biblia, hadi hii ya kuuawa au kutotoza riba kuondoshwa na viongozi wa kanisa. Hii ni kwa kuwa kwa mafundisho ya Ukristo, yamewapa mamlaka viongozi hao kwa kuwa na roho mtakatifu kuwa hawafanyi makosa na hivyo Papa anatunga sheria. Hili la mamlaka ya papa na kutofanya makosa, linaweza kujadiliwa msingi wake wakati mwingine. Katoa wapi papa mamlaka haya ya kufuta Sheria za biblia?

Uislam hauna upapa wa kutunga Sheria. Sheria zipo na aliyeziweka ni yeye au kwa amri yake. Nyingine zipo wazi na nyingine zinahitaji juhudi kuzifahamu. Hizi zinazohitaji juhudi kuzifahamu ndio mlango aliouacha Mola makusudi kwa hekima yake-watu watafakari na waamue kwa umoja wao. Hizi Sheria zake zilizowazi hazina wakati wa kuzibadilisha, yeye ametaka iwe hivyo, waislamu wanasalimu amri juu yake. Na hii ni maana moja wapo ya Muislam. Yale ambayo ameyaacha bila sheria ya wazi, tutajadiliana na kwenda na wakati. Uislam sio mgeni wa dhana ya kwenda na wakati katika fungu hili la pili la Sheria zinazotokana na juhudi ya wanazuoni ambao hawana mamlaka ya sheria za wazi alizoweka Mola.Kwa mfano, chini dola ya Ottoman empire, waliweka sheria kuwa faida katika bidhaa isizidi 100%. Lakini kwa kwenda na wakati, kwa kuzingatia laws of demand and supply, sheria hiyo haipo tena. Ili kwenda na wakati, Utawala wa Khalifa Omar, uliweka kodi mbalimbali ambazo hazijatajwa na Mungu wala Mtume wake kulingana na mazingira na hali ilivyo. Dola ya kiislam ya leo, inaweza kuondoa kodi hizo bila kuonekana wanavunja Sheria ya Mungu, kwa kuwa hazikutungwa na Mungu wala kufunzwa na Mtume, bali yalikuwa makubaliano ya waislam wa zama zile.

Nikomee hapa. Samahani kwa makala ndefu, lakini natumai ipo faida ndani yake.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...