Monday, January 30, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Highly Paid Expert"

Leo nilikwenda Minneapolis na wakati wa kurudi, nilipita Mall of America, kuangalia vitabu katika duka la Barnes & Noble. Nilitaka hasa kuona kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Niliangalia scheme vinapowekwa vitabu vya fasihi, nikakuta kitabu kipya juu ya Ernest Hemingway, Everybody Behaves Badly: The Backstory to 'The Sun Also Rises.' kilichoandikwa na Lesley M.M. Blume. Kwa kuwa nimezama sana katika uandishi wa Hemingway, maisha na falsafa yake, na kwa kuwa nimeshasoma The Sun Also Rises, nilitamani kukinunua kitabu hiki, ambacho, kwa maelezo niliyoyaona, kinazungumzia yaliyo nyuma ya pazia.

Sikuwa na hela za kutosha, kwa hivyo nikaamua kuangalia vitabu vingine. Nilitumia muda zaidi katika sehemu ya "Business/Management." Huwa ninapenda sana kununua na kusoma vitabu vya taaluma hii, kwani vinanifundisha mengi kuhusu mambo ya ujasiriamali na biashara. Taaluma hii inanisaidia katika kuendesha shughuli za kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants.

Hatimaye, nilikiona kitabu kilichonivutia kwa namna ya pekee, The Highly Paid Expert, kilichoandikwa na Debbie Allen.  Kwa mujibu maelezo nyuma ya kitabu, huyu mwandishi ni mtaalam maarufu katika mambo ya biashara na ujasiriamali. Niliangalia ndani, nikaona mada anazoongelea ni za kuelimisha kabisa, kama vile matumizi ya tekinolojia za mawasiliano na mitandao.

Niliona anatoa ushauri wa kusisimua. Kwa mfano, anasema kuwa ni lazima mtu unayetaka mafanikio katika shughuli zako, uwasaidie wengine kufanikiwa. Unavyowasaidia wengine wafanikiwe, unajijengea mtandao wenye manufaa kwako pia. Ubinafsi na uchoyo wa maarifa haukuletei mafanikio. Kitabu hiki kinavutia kwa jinsi mwandishi anavyothibitisha mawazo yake, ambayo kijuu juu yanaonekana kama ya mtu anayeota ndoto.

Kwa bahati niliweza kuimudu gharama ya kitabu hiki, nikakinunua na kuondoka zangu, kwani nilikuwa sina hela iliyosalia. Sijutii kununua vitabu. Vitabu vinavyoelimisha ni mtaji, kwani hakuna mtaji muhimu zaidi ya elimu. Kwa wajasiriamali, wafanya biashara, watoa huduma, na kwa kila mtu, elimu ni tegemeo na nguzo muhimu. Ulazima wa kununua vitabu ni sawa na ilivyo lazima kwa mkulima kununua pembejeo.

Thursday, January 26, 2017

Ukabila wa Tanzania

Kuna dhana kuwa hakuna ukabila Tanzania, kwa maana ya ubaguzi au uhasama miongoni mwa makabila. Kwa ujumla dhana hiyo ni ukweli, hasa tukifananisha na baadhi ya nchi zingine. 
Lakini, ni wazi kuwa wa-Tanzania wengi wameamua kubuni namna ya kuifanya nchi yetu ifurahie matunda ya ukabila. Kwa kuwa ubaguzi na uhasama wa makabila umeshindikana, wamegundua kuwa ubaguzi na uhasama unawezekana kwa njia ya vyama vya siasa.
Mimi ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa ninaangalia mambo wanayofanya wa-Tanzania wenye vyama, na ninaona jinsi yanavyofanana na yale yanayotokea katika nchi zenye ukabila.
Kwa mfano, katika nchi moja jirani, ukabila ulivyokolea, wahusika walikuwa wanaitana majina ya kudhalilisha, hasa ya wadudu au wanyama. Hiyo ilikuwa ni sehemu ya itikadi ya uhasama. 
Hali hiyo tayari imeshamiri Tanzania. Watu hawaitwi binadamu, bali nyumbu, fisi, na kadhalika. Kule Rwanda, kabla ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994, katika propaganda dhidi ya wale waliokusudiwa kuuawa walipewa majina kama "inyenzi" (kwa ki-Ingereza, "cockroaches").
Wa-Tanzania wenye vyama wanatupeleka huko huko. Maandalizi ya kiitikadi yameshakamilika. Vitendo vya kuhujumiana, vitisho, na hata mauaji vimekuwa vikifanyika, hasa wakati wa kampeni za uchaguzi, na kuna kila dalili kuwa vitendo hivi vitashamiri. 
Mwalimu Nyerere kabla hajaaga dunia, alihofia hali iliyokuwa ikijitokeza Tanzania, akauliza iwapo wa-Tanzania tumechoshwa na amani. Ni wazi kuwa wa-Tanzania tuliziba masikio.
Wenye vyama wanazidi kuvuruga amani, sio tu kwa vitendo wanavyofanyiana, bali pia kwa hofu wanayoijenga mioyoni mwa sisi tusio na vyama, ambao ni watu wa amani. Ni ujinga kujidai kuwa sisi ni nchi ya amani, wakati mioyoni hakuna amani, bali hofu.
Enzi za Mwalimu Nyerere, kulikuwa na viongozi, ambao walitambua na kuzingatia umuhimu wa kudumisha mazingira ya amani nchini. Leo, wale wanaotegemewa kuwa viongozi ndio vinara na wahamasishaji wa uvunjifu wa amani. Ni kama ilivyokuwa Rwanda, kuelekea mwaka 1994.
Kwa kuwa hatujabahatika kuwa na ukabila kama wenzetu wa nchi zingine, wa-Tanzania wengi wameona tunahitaji nasi kufaidi matunda ya ukabila kwa kutumia vyama vya siasa. Mungu isamehe Tanzania.

Sunday, January 22, 2017

Maandamano Makubwa Dhidi ya Rais Trump

Jana hapa Marekani yamefanyika maandamano makubwa dhidi ya rais Donald Trump, ambaye aliapishwa juzi. Maandamano haya yaliyoandaliwa na kukusudiwa kwa wanawake, yanasemekana kuwa makubwa kuliko yote yaliyowahi kufanyika katika historia ya Marekani kwa siku moja. Maandamano haya yamefana sana, kwa mahudhurio na hotuba mbali mbali, na yametoa ujumbe wa wazi kuwa serikali ya Rais Trump isitegemee kuwa itatekeleza ajenda yake bila vipingamizi.

Marekani ni nchi inayoheshimu uhuru wa watu kujieleza. Katiba inalinda uhuru huo. Ndio maana maandamano ya kumpinga Rais Trump yalifanyika nchi nzima bila kipingamizi. Polisi walikuwepo kwa ajili ya kulinda amani, si kuzuia maandamano, wala kuwakamata wahutubiaji waliokuwa wanamrarua Rais Trump. Polisi wana wajibu wa kuhakikisha kuwa waandamanaji wanayo mazingira muafaka na fursa kamili ya kutekeleza haki yao ya kuandamana na kuelezea mawazo yao.

Ninajua kuna wengine walioshiriki maandamano ya jana ambao si wa-Marekani. Kuna wakimbizi na wahamiaji kutoka nchi mbali mbali ambao walishiriki. Hapa Marekani, huhitaji kuwa raia ili kushiriki maandamano. Mimi sikushiriki, kwa sababu zangu binafsi.

Kwa kuwa mimi si raia wa Marekani, na sijawahi kuwazia kuwa raia, sioni kama nina haki au sababu ya kujihusisha na siasa za ndani za Marekani. Sipigi kura wakati wa uchaguzi wa viongozi. Kwa nini nijihusishe na maamuzi ya hao viongozi? Kama maamuzi yataiathiri nchi yangu, hapo nitaona nina wajibu wa kuisemea nchi yangu. Ninatambua wajibu wangu wa kuitetea nchi yangu popote nilipo.

Ingekuwa maandamano yanahusu masuala ya Tanzania ningeshiriki, kwa sababu Tanzania ni nchi yangu. Serikali ya Tanzania ikifanya mambo yasiyokubalika, halafu wa-Tanzania au marafiki wa Tanzania wakaandaa maandamano ya kupinga au kulaani, ni haki yangu kushiriki. Kule Uingereza, mwaka 2015, wa-Tanzania waliandamana kupinga mwenendo wa uchaguzi Zanzibar. Maandamano kama yale ni haki yangu kushiriki.

Huu utamaduni wa Marekani na nchi kama Uingereza unaendana na tangazo la kimataifa la haki za binadamu. Baada ya maandamano haya ya kihistoria ya jana dhidi yake, Rais Trump ametuma ujumbe: "Peaceful protests are a hallmark of our democracy. Even if I don't always agree, I recognize the rights of people to express their views." Tafsiri kwa ki-Swahili ni, "Maandamano ya upinzani ya amani ni kielelezo thabiti cha demokrasia yetu. Hata kama mara nyingine sikubaliani na wahusika, ninatambua haki ya watu kuelezea mawazo yao."

Thursday, January 19, 2017

Nimejipatia Vitabu Vingine vya Bure

Jana niliandika katika blogu hii kuhusu vitabu nilivyovipata jana hiyo hiyo. Nilisema kuwa nilivipata hapa chuoni St. Olaf. Leo nilipita tena hapo, nikaviona vitabu vingi vya soshiolojia, na vichache vya taaluma zingine.

Nilichukua vitatu. Kimoja ni Who Speaks for Islam?: What a Billon Muslims Really Think, kilichoandikwa na John L. Esposito na Dalia Mogahed. Ni matokeo ya utafiti uliofanywa miongoni mwa wa-Islam kutoka nchi nyingi, ili kubaini mitazamo yao juu ya masuala kadhaa, kama vile mahusiano baina ya nchi za ki-Islamu na mataifa ya Magharibi, wanawake katika jamii za ki-Islam, na jihad.

Kitabu kingine ni Student Learning Abroad: What Our Students Are Learning, What They're Not And What We Can Do About It. kilichohaririwa na Michael Vande Berg, R. Michael Paige, and Kris Hemming Lou. Nimekisikia kitabu hiki kwa miaka miwili au mitatu, na nilitaka kukinunua. Imekuwa kama muujiza kuwa nimeiona nakala, nikajuchukulia. Kutokana na nilivyofahamu, kitabu hiki ni muhimu sana kwa watu kama mimi ambao tunajishughulisha na programu za kupeleka wanafunzi nchi za nje.

Katika vyuo vingi vya Marekani kuna programu za kupeleka wanafunzi nchi za nje kwa masomo ambayo huweza kuwa ya muda mfupi, kama mwezi moja, muda mrefu kiasi, kama miezi sita, na pia muda mrefu zaidi, kama mwaka moja. Fikra zilizopo ni kuwa fursa hizo huwapa wanafunzi upeo mpana wa ulimwengu na tamaduni tofauti, na kwa hivyo huwaandaa kuweza kuumudu ulimwengu ambao una mwingiliano mkubwa wa tamaduni.

Kitabu hiki chenye insha nyingi kinajadili mtazamo huo ili kuona kama una mashiko au la. Kwangu mimi ambaye daima nimeamini kuwa programu za kupeleka wanafunzi nchi za nje zina manufaa sana, kitabu hiki ninahisi kitanifungua macho nione mambo ambayo sikuyafahamu.

Kitabu cha tatu nilichojipatia ni riwaya, On the Hills of God, iliyotungwa na Ibrahim Fawal. Huyu ni m-Marekani mwenye asili ya Palestina, mzaliwa wa Ramallah. Sikuwa ninamfahamu, ila nimeona maelezo juu yake katika kitabu hiki. Ni msomi anayefundisha masomo ya filamu na fasihi. Hii ni riwaya ya kwanza ya mwandishi huyu, na inaanzia na tukio la kuporwa kwa ardhi ya wa-Palestina kulikofanywa na wa-Zionisti mwaka 1947, Kutokana na upekee wa suala la harakati za wa-Palestina, nitafanya juu chini niisome riwaya hii.

Wednesday, January 18, 2017

Vitabu Nilivyojipatia Leo

Leo, baada ya wiki nyingi kidogo, nimeona nirejee tena kwenye mada ambayo nimekuwa nikiiandikia tena na tena katika blogu hii. Ni juu ya vitabu ninavyojipatia, iwe ni kwa kununua, au kwa namna nyingine.

Leo asubuhi, kama kawaida, nilienda chuoni St. Olaf kufundisha. Nilipoingia katika jengo la maktaba, ambamo pia ni makao ya idara yangu ya ki-Ingereza, nilipita kwenye meza ambapo huwekwa vitabu na makabrasha kwa ajili ya yeyote anayehitaji. Niliona meza imejaa vitabu kuliko siku nyingine yoyote iliyopita, nikaamua kuviangalia.

Niliona kuwa vyote vilikuwa vitabu vya taaluma, hasa masuala ya wanawake na jinsia. Niliamua kujichukulia vitatu, baada ya kuangalia ndani na kuona maelezo ya vitabu hivi. Kitabu kimojawapo ni Sex & Power, kilichotungwa na Susan Estrich. Niliona maelezo kuwa mwandishi alikuwa profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha Harvard na baadaye profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha California ya Kusini. Ameandika vitabu kadhaa na makala mbali mbali. Alikuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais wa Harvard Law Review. Huenda msomaji wa taarifa hii utakumbuka kuwa hiki ni cheo ambacho Barack Obama aliwahi kushika. Kutokana na mada ya kitabu, na orodha ya sura zake niliona kuwa kitabu hiki kitanielimisha sana kuhusu nafasi ya wanawake katika jamii.

Kitabu cha pili kilichonivutia kwa namna ya pekee ni Globalization: The Making of World Society, ambacho kimetungwa na Frank J. Lechner. Kama tunavyofahamu, mada ya utandawazi inavuma sana miongoni mwa wanataaluma, wanasiasa, na jamii kwa ujumla. Hata hivi, mitazamo kuhusu nini maana ya utandawazi, chimbuko lake, faida na hasara zake, ni masuala ambayo yanajadiliwa na yamegubikwa na utata.

Mimi mwenyewe, kwa miaka kadhaa, nimetafakari suala la utandawazi, nikilihusisha na tofauti za tamaduni. Nimewahi hata kuendesha warsha kadhaa, nchini Tanzania, katika miji ya Arusha, Dar es Salaam, na Tanga. Kwa hivi, nilipokiona kitabu cha Globalization: The Making of World Society, nilikuwa na hamu ya kukisoma. Hiki kitaongeza idadi ya vitabu vyangu kuhusu utandawazi.

Kitabu cha tatu, Behind the Veil in Arabia: Women in Oman, kilichoandikwa na Unni Wikan, kilinivutia pengine zaidi ya hivi vingine. Nilipoona jina la kitabu hiki, nilikumbuka mara majina ya vitabu vingine, kama vile Beyond the Veil, cha Fatima Mernissi wa Morocco. Suala la wanawake katika nchi za ki-Arabu limeshika nafasi ya pekee kichwani mwangu kutokana na kozi niliyoanzisha na ninaifundisha, "Muslim Women Writers."

Simaanishi, na mtu asidhani, kwamba wa-Arabu wote ni wa-Islam, bali kuna suala la jinsi utamaduni unavyoingiliana na dini kiasi kwamba pamoja na tofauti za dini, kuna mambo kama mila, desturi, na lugha, ambayo yanawaungamisha wa-Arabu.

Katika kufundisha kozi ya "Muslim Women Writers" imedhihirika kuwa vazi kama hijab ni suala la utamaduni zaidi kuliko dini. Qur'an inasema wanawake wajisitiri na wainamishe macho, lakini haisemi wavae nini. Hili ni suala la kila utamaduni, na ndio maana mavazi ya wanawake wa ki-Islam katika tamaduni mbali mbali yanahitilafiana.

Maktaba yangu imetajirika leo kwa kuongezewa vitabu hivi muhimu. Ni raha iliyoje kujipatia hazina kubwa namna hii bila gharama yoyote kwa upande wangu.

Monday, January 16, 2017

Erica Huggins Ahutubia Chuoni St. Olaf

Leo mwanaharakati Erica Huggins amehutubia chuoni St. Olaf. Alialikwa kuhutubia kama sehemu ya maadhimisho ya siku ya Martin Luther King Jr. Erica Huggins alikuwa mwanaharakati maarufu katika Black Panther Party, na ameendelea kuwa mwelimishaji wa jamii, kama inavyoelezwa katika tovuti yake.

Ameelezea historia yake katika Black Panther Party, jinsi mume wake alivyouawa na idara ya upelelezi ya FBI, na jinsi yeye mwenyewe alivyofungwa kwa miaka miwili. Humo kifungoni alitumia muda wake kujichunguza nafsi na akili yake na masuala ya maisha na ulimwengu kwa umakini na utulivu mkubwa. Anaendelea na jadi hiyo, ambayo huitwa "meditation," kila siku.

Amesema kuwa mifumo yote ya kihasama na ukandamizaji, fikra zote za kihasama na kikandamizaji ni mambo yaliyoundwa na wanadamu. Kwa hivyo, wanadamu wana uwezo wa kuleta mabadiliko kwa kuunda mifumo na fikra zenye kujenga maelewano, upendo, na maendeleo ya binadamu. Alisema kuwa tunapaswa kuviheshimu viumbe vyote, sio binadamu tu. Hapo nilimkumbuka Shaaban Robert, ambaye naye alihimiza moyo wa kuvijali viumbe vyote.

Nimeguswa sana na hotuba yake, nikalazimika kutafakari hali ya Tanzania na ulimwengu, jinsi tunavyotumia nguvu nyingi katika kujenga uhasama, kushambuliana, na kubezana. Erica Huggins amebainisha kuwa tunaweza kuleta mapinduzi katika nafsi zetu, katika jamii zetu, na ulimwenguni.  

Saturday, January 14, 2017

Kitabu cha Uchambuzi wa "Hamlet"

Mwandishi maarufu Ernest Hemingway alisema, "There is no friend as loyal as a book," yaani hakuna rafiki wa kweli kama kitabu. Vyovyote unavyotaka kuitafsiri kauli hii ya Hemingway, ukweli ni kuwa kusoma kitabu kizuri ni mithili ya kuongea na rafiki wa kweli.

Baada ya kusoma Hamlet, kama nilivyoelezea katika blogu hii, nimeamua kusoma kitabu cha insha juu ya Hamlet, kinachoitwa Hamlet, ambacho kimehaririwa na Susanne L. Wofford. Ni kitabu cha insha ambazo zinaongelea nadharia za fasihi, na zinaichambua Hamlet kwa kutumia hizo nadharia tofauti.

Nadharia hizo ni "Feminist Criticism," "Psychoanalytic Criticism," "Deconstruction," "Marxist Criticism," na "The New Historicism." Lakini, pamoja na maelezo ya kina ya nadharia hizo, na uchambuzi mbali mbali wa Hamlet, kitabu hiki kina pia tamthilia yote ya Hamlet, toleo la The Riverside Shakespeare. Pia kitabu hiki kina maelezo ya maisha ya Shakespeare na mazingira ya kihistoria alimokulia, na historia ya uchambuzi wa tamthilia hiyo.

Ingawa nina vitabu vingine vya nadharia za fasihi, sio tu hizi zilizomo katika kitabu hiki, bali pia zingine, kama vile "Post-colonial criticism," "Structuralism," na "Post-structuralism," ninafurahia sana kusoma kitabu hiki. Kwa upande moja, ni muhimu kutambua kwamba hata kama unadhani unalifahamu jambo fulani katika taaluma, ni vizuri kuendelea kusoma mitazamo mbali mbali juu ya jambo hilo, au maelezo tofauti, kwani hata kama mtazamo ni ule ule, kila mwandishi ana namna yake ya kuuelezea.

Kwa hivyo, tukichukulia nadharia kama "Feminist Criticism" inavyoelezwa katika kitabu hiki, tunaona kuwa kuna misisitizo au mielekeo tofauti baina ya wachambuzi wa Marekani, Uingereza, na Ufaransa. Jambo hilo nilianza kulifahamu miaka ya 1980-86 nilipokuwa ninasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, hasa katika idara ya "Comparative Literature."

Ningetamani kuwa na ufahamu mkubwa wa ki-Swahili kiasi cha kuweza kuelezea kila kitu bila kutumia maneno ya ki-Ingereza. Dosari hii si jambo la kujivunia, nami sijasita kutamka hivyo katika blogu hii. Hata hivyo, ninavyofaidi kusoma vitabu vya ki-Ingereza, ninawasikitikia wale ambao hawajui lugha hii ambayo ndio lugha muhimu kuliko zote katika mawasiliano duniani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...