Thursday, March 7, 2013

Utalii wa Kiutamaduni Unakuza Uchumi Haraka



Hapa ni ndani ya kituo cha utamaduni cha jiji la Arusha
 Na Albano Midelo

UTALII wa kiutamaduni bado ni nadharia changa katika nchi za ulimwengu wa tatu ikiwemo Tanzania,kutokana na ukweli kuwa katika nchi hizo wamezoea kuona utalii wa asili wa kutembelea mbuga za wanyama.

Utalii wa kiutamaduni ni nadharia mpya hapa nchini ambapo serikali imeanza kuutambua utalii wa kiutamaduni na kuupa nguvu kubwa aina hiyo ya utalii miaka ya hivi karibuni,zamani vivutio vya utalii wa kiutamduni kama majengo ya kale,maeneo ya kihistoria na makumbusho hayakupewa mtazamo wa kiuchumi zaidi.

Maeneo hayo yalipewa mtazamo wa kielimu zaidi na kuundwa idara za mambo ya kale na idara ya makumbusho ambazo zote awali zilikuwa katika wizara ya elimu na utamaduni ambavyo viliwekwa kama vyanzo vya elimu zaidi kuliko vyanzo vya utalii kwa sababu wakati ule  watalaamu walifanya tafiti mbalimbali za mambo ya kale wakiwemo wakina Dk.Leakey


Hata hivyo baadaye kulikuwa na mabadiliko katika ulimwengu mzima hali iliyosukuma kuwepo kwa utalii wa kiutamduni na nchi zilianza kutoa kipaumbele katika utalii wa kiutamaduni ndiyo maana hapa nchini idara za mambo ya kale na makumbusho zilihamishwa kutoka wizara ya elimu na kuingia katika wizara ya utalii na maliasili.


 Utalii wa kiutamadini hivi sasa unakuwa na  hata mabadiliko ya utalii huo hayawezi kuonekana kwa haraka badala yake inatakiwa watalaamu kuwahamasisha wananchi kutambua fursa zilizopo katika aina hiyo ya utalii na kuzitumia ipasavyo fursa zilizopo ili kujiletea maendeleo wao binafsi na Taifa kwa ujumla wake.


Ni vigumu sana kutenganisha utalii asili na  utalii wa kiutamduni kutokana na aina hizo mbili za utalii kuwa na mahusiano ya karibu.Watalii wanapoingia nchini wote wanavutika na utalii wa aina zote mbili  .


Mtalii anapokwenda kutembelea utalii wa asili kama mbuga za wanyama pia anaweza kupita katika maeneo yenye utalii wa kiutamaduni na kwamba fursa ya utalii wa kiutamaduni ni kubwa kwa wananchi wa kawaida kuliko aina nyingine za utalii.


Mhadhili msaidizi kutoka idara ya utalii wa kiutamaduni chuo kikuu kishiriki cha Tumaini Frank Kimaro anabainisha kuwa  utalii wa kiutamaduni unazungumzia jamii husika na kwamba jamii hiyo inaweza kufaidika kutokana na utalii wa kiutamaduni ambao unapatikana katika eneo husika hadi kufikia hadi ngazi ya kitaifa.

“Unaweza kuona aina hii ya utalii ni tofauti na utalii wa asili ambao tunaangalia zaidi mbuga za wanyama na maeneo ambayo yametengwa na serikali ambapo wahusika wakubwa ni serikali yenyewe na siyo watu binafsi,katika utalii wa kiutamaduni wahusika wakuu ni  wananchi wenyewe”,anasisitiza  na kuongeza


“Wananchi katika utalii wa utamaduni wanaweza kunufaika kuanzia kiwango cha familia, mtaa, kitongoji,kijiji,wilaya,mkoa na kitaifa kwa hiyo utalii wa kiutamaduni unatoa fursa kubwa sana ya ukuaji wa uchumi kuanzia kwa mtu binafsi hadi kwa taifa”


Licha ya utalii wa utamaduni kuonekana kumlenga zaidi mwananchi wa kawaida ,lakini kipato anachopata mwananchi huyo kwa kucheza ngoma au kuuza bidhaa za jadi na kazi nyingine za mikono kipato chake kimekuwa cha chini na kuwakatisha tamaa wananchi.


Kimaro anasema kuwa vitu anavyovifanya mwananchi katika utalii wa kiutamaduni vina thamani kubwa kuliko mapato anayopata na kwamba katika hali ya kawaida vitu vya utamaduni vina thamani kubwa  na vikiachwa kupotea haviwezi kupatikana tena na kwamba hakuna kiwango cha malipo kamili kwa shughuli za utalii wa kiutamaduni.


Hata hivyo Kimaro anasema kuwa  utalii wa kiutamaduni unaweza kubadilisha kiwango cha maisha ya watu kutokana na kupata kipato kutokana  na kazi hiyo kuwa shughuli mbadala ambayo inawasaidia wao kuwaongezea kipato cha ziada katika mapato yao.


Anabainisha kuwa kabila la wamasai katika msimu wa utalii wa kiutamaduni wanapata mapato karibu shilingi 30,000 kwa siku kutokana na aina hiyo ya utalii jambo ambalo linaonesha kuwa ni kipato kikubwa ukilinganisha na vijana wengine mijini ambao wanaingiza kipato kidogo sana.


Bidhaa zinazotokana na utalii wa kiutamaduni kama samani zilizotengezewa kwa miti pamoja na sanamu za kuchonga zimekuwa zinauzwa na watu binafsi kwa watalii na wageni wengine kwa bei za juu sana kwa mfano kiti kinachotengezwa kwa kutumia miti ya mianzi kinauzwa kati ya shilingi 200,000 hadi 300,000,


kofia inayotengenezwa kwa ukindu inauzwa kati ya shilingi 3500 hadi 5000,mkanda unaotengenezwa kwa ngozi  yenye shanga unauzwa kati ya shilingi 5000 hadi 10,000,kigoda kilichotengenezwa kwa mti wa kawaida kinauzwa kati ya shilingi 10,000 hadi 15,000 wakati kinyago cha kuchongwa kinauzwa kuanzia shilingi 20,000 hadi 500,000 kutegemea na ukubwa wa kinyago hicho.


Hata hivyo amesema bei ya mtengenezaji ni ndogo ambapo muuzaji wa mwisho ndiyo anayepata faida kubwa kwa kuwa anauza kwa bei ya juu zaidi  na kwamba mnunuzi wa kati anakwenda kutafuta vitu hivyo sehemu ambazo mzalishaji anauza kwa bei nafuu ili na yeye aweze kuuza kwa bei ya juu  ili kufidia gharama za usafiri, uchukuzi, uhifadhi na malazi.


Nafasi ya utalii wa kiutamaduni ni kubwa katika kukuza uchumi wa nchi  kutokana na ukweli kuwa utalii unachangia uchumi wa Tanzania katika kiwango kikubwa  na kuchukua nafasi ya pili hivyo utalii endelevu una nafasi kubwa katika kuleta maendeleo endelevu.


Kulingana na mhadhili huyo utalii huo pia una nafasi kubwa ya kuchangia uchumi wa watu binafsi kwa sababu utalii unatengeneza ajira za moja kwa moja na ajira ambazo sio za moja kwa moja ambapo  watanzania wengi hivi sasa wamejiajiri katika shughuli za utalii wa kiutamduni ambao wamefungua maduka ambayo wanauza vitu vya kiutamaduni vyenye bei kubwa zaidi katika soko la utalii.


“Soko la vitu vya utamaduni wa kitalii vinatoa ajira kwa watu wengi wakiwemo mwenye duka,mtengenezaji na msambazaji hivyo kufungua fursa za ajira za moja kwa moja kwa wananchi ambapo watu wengine wananufaika na utalii wa utamaduni kutoka kwenye migongo ya watu walioajiriwa  moja kwa moja katika sekta hiyo’’,anasisitiza.


Anawataja watu wanaonufaika katika sekta ya utalii wa kiutamduni kutoka katika migongo ya watu wengine kuwa  ni pamoja na watu wenye hoteli,nyumba za kulala wageni,watu wanaouza maji na vyakula mbalimbali na kwamba  utalii huo unafungua milango ya ajira.


Uchunguzi umebaini kuwa katika ulimwengu hivi sasa kuna nchi nyingi ambazo zimekuza uchumi wake kwa haraka kupitia utalii wa kiutamaduni zikiwemo Australia,Ujerumani,Uingereza pamoja na nchi nyingine nyingi za ulaya ambazo kutokana na ukosefu wa mbuga za wanyama wengi kama zilivyo katika Afrika wameamua kuendeleza utalii wa kiutamaduni zaidi kuliko utalii wa asili na kupata maendeleo makubwa kupitia aina hiyo ya utalii.


Kutokana na hali hiyo watanzania na wadau wote wa utalii wanatakiwa sasa kubadilika kimawazo na kifkra kutoka   katika aina ya utalii wa asili ambao ni kuangalia wanyamapori na na kuingia katika utalii wa kiutamaduni ambao ni wa kipekee kwa kuwa  hutofautiana  kutoka eneo moja kwenda eneo jingine na watalii kupata vitu vipya hivyo kuvutika zaidi .



albano.midelo@gmail.com, 0766463129.

CHANZO: Blogu ya Maendeleo ni Vita



No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...