Saturday, July 25, 2015

Rais Obama na Dada Yake Auma Obama

Ujio wa Rais Obama nchini Kenya juzi umezua mambo mengi, ikiwemo furaha isiyo kifani miongoni mwa watu wa Kenya, Afrika Mashariki, na kwingineko. Kitendo cha Rais Obama kukutana na ndugu zake katika chakula cha jioni ni jambo la kukumbukwa. Kwa namna ya pekee, wengi tuliguswa na namna Rais Obama na dada yake Auma Obama walivyokutana.

Nilivyomwona dada huyu, nilikumbuka kuwa niliwahi kumtaja katika blogu hii baada ya kununua kitabu chake, And Then Life Happens: A Memoir. Niliingia mtandaoni nikaona mahojiano aliyofanyiwa na mtangazaji wa CNN. Halafu nilikitafuta kitabu chake katika maktaba yangu nikakipitia, kwa kuwa nilikuwa sijakisoma, bali nilikuwa nimekipitia juu juu tu.

Hakuna ubishi kwamba Auma Obama ni mama mwenye fikra za kusisimua na uwezo mkubwa wa kujieleza. Hilo linajitokeza wazi katika mahojiano yake. Masimulizi ya maisha yake, yaliyomo katika kitabu chake, yana mambo yanayoweza kuwahamasisha watoto wetu, hasa wasichana, wawe wanajiamini na kuwa watafuta elimu na maendeleo, wakijua kuwa wao wana uwezo sawa na mtu mwingine yeyote.

Kitu kingine kilichonivutia juu ya Auma Obama ni kwamba anakimudu sana ki-Jerumani, lugha ambayo alianza kujifunza alipokuwa Kenya na baadaye alipokuwa masomoni Ujerumani, ambako aliishi na kufanya kazi kwa miaka mingi. Kitabu chake alikiandika kwa lugha hiyo. Ninukuu maelezo yake kuhusu jambo hilo:

This book was originally written in German. Some may wonder why, when English is actually a language I grew up with, next to my native tongue, Luo. But the fact that I studied and worked in Germany made it seem natural to tell my story in the language in which I had spent my formative adult years. The writing came more easily to me, and in many ways my main audience was a German one.

Natafsiri kwa ki-Swahili kama ifuatavyo:

Kitabu hiki kiliandikwa awali kwa ki-Jerumani. Baadhi ya watu huenda watashangaa kwa nini, wakati ki-Ingereza ni lugha niliyokua nayo, sambamba na lugha mama yangu ya ki-Jaluo. Lakini ukweli kwamba nilisoma na kufanya kazi Ujerumani ilisababisha iwe rahisi kwangu kujieleza katika lugha ambayo ilinilea miaka ya kukua kwangu katika utu uzima. Uandishi huo ulikuja kirahisi kwangu, na kwa vyovyote, hadhira yangu kuu ilikuwa ni ya wa-Jerumani.

Kwa kuhitimisha, ninapenda kusema jinsi ninavyoguswa na ukweli kwamba mtu na dada yake, yaani Rais Obama na Auma Obama, wote wana vipaji vinavyofanana. Mbali ya kuwa ni waandishi, wote wanajituma katika kutumikia jamii. Katika mahojiano yake, Auma Obama anaongelea shughuli za taasisi yake iitwayo Sauti Kuu ambayo inashughulika na malezi ya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...