Wednesday, July 1, 2015

Vitabu Nilivyojipatia Wiki Hii

Kama ilivyo kawaida yangu, napenda kuongelea vitabu nimeongeza katika maktaba yangu. Wiki hii, ambayo bado haijaisha, nimejipatia vitabu vinne. Cha kwanza ni Jake Riley: Irreparably Damaged, kilichotungwa na Rebecca Fjelland Davis. Nilikinunua tarehe 28 mwezi huu, katika tamasha la vitabu, Deep Valley Book Festival, mjini Mankato kutoka kwa mwandishi, ambaye tumefahamiana miaka kadhaa. Kufuatana na maelezo, hii ni hadithi ya kubuniwa.

Katika tamasha hilo, nilinunua pia kitabu kiitwacho No Behind, kilichotungwa na Louise Parker Kelly. Tuliongea kidogo, na mwandishi, akaniambia kuwa ni mwalimu na kuwa kitabu chake ni hadithi ya kubuniwa, kuhusu maisha na harakati za mtoto wa shule eneo la Washington D.C.

Kitabu kingine ambacho nilikipata jana ni Noontide Toll. Ni mkusanyo wa hadithi fupi za Romesh Gunesekera, mwandishi mahiri sana wa Sri Lanka. Sikumbuki kama nilikinunua kitabu hiki. Huenda wachapishaji wameniletea kwa kuwa nimewahi kuagiza vitabu vingine vya Gunesekera kwa kufundishia. Gunesekera ni mmoja wa waandishi wanaonivutia sana kwa uwezo wao wa kutumia ki-Ingereza.

Kitabu kingine, Lucy: the Beginnings of Humankind, nilikinunua jana katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf. Waandishi wake ni Donald Johanson na Maitland Edey. Nilivutiwa na jina la Lucy kwenye uso wa kitabu, nikahisi kuwa kitabu kinamhusu binadamu wa kwanza, ambaye masalia yake yalivumbuliwa Ethiopia. Nilipokisogelea, niliona kuwa ni hivyo.

Kutokana na maelezo kwenye jalada la mbele, kitabu hiki kinasimulia namna uvumbuzi huu ulivyotokea na maelezo kuhusu binadamu huyu wa kwanza. Kwa mujibu wa uchambuzi katika gazeti la The New York Times Book Review, dhamira ya kitabu hiki ni "One of the most compelling scientific investigations ever undertaken." Ni wazi kuwa kitabu hiki ni hazina isiyo kifani. 

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...