Tuesday, July 28, 2015

Kitabu Umechapisha, Kazi ni Kukiuza

Pamoja na kuandika vitabu, ninajitahidi kujielimisha kuhusu masuala yanayohusiana na uchapishaji, utangazaji, na uuzaji wa vitabu. Kwa bahati nzuri, kuna vitabu vingi na vingine vinaendelea kuchapishwa, na pia makala nyingi kuhusu masuala hayo.

Napenda kuongelea suala la kukiuza kitabu. Niliwahi kuongelea suala hili katika blogu hii. Nimeliongelea pia katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Ni suali linalonigusa na kunifikirisha daima, nami napenda kuwashirikisha waandishi wengine katika kulitafakari.

Usemi kwamba chema chajiuza, kibaya chajitembeza unaweza kuwa na mantiki nzuri kuhusiana na vitabu. Wateja wakiridhishwa au kufurahishwa na kitabu, hawakosi kuwaambia wengine. Aina hii ya utangazaji, ambayo kwa ki-Ingereza huitwa "word of mouth," ni muhimu sana.

Mimi mwenyewe nimeshuhudia hivyo kutokana na kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Tangu nilipokichapisha kitabu hiki, mwaka 2005, wasomaji wamekuwa wakiwaambia wengine. Kwa lugha ya mitaani, wanakipigia debe.

Waandishi wengi hawajui kuwa baada ya kuchapisha kitabu, wana jukumu la kukitangaza na kukiuza. Wengi wanamtegemea mchapishaji afanye kazi hiyo. Hakuna shaka kwamba mchapishaji hujitahidi kukitangaza kitabu. Anawajibika kufanya hivyo, kwani anatafuta fedha za kugharamia uchapishaji, kuwalipa wafanyakazi wake, na kujipatia faida.

Lakini, waandishi tunapaswa kuona mbali zaidi. Kwanza, tusijiziuke. Mchapishaji hawezi kufanya kila kitu, hata kama angependa. Gharama za kukitangaza kitabu ni kipingamizi kwa mchapishaji, hasa yule ambaye si tajiri.

Pili, dunia inabadilika muda wote, nasi tunawajibika kujifunza mambo mapya muda wote. Leo hii kuna tekinolojia zinazomwezesha mwandishi kujichapishia kitabu chake. Katika mazingira haya, mwandishi anawajibika kubeba jukumu la kutangaza na kuuza kitabu. Si busara kutegemea "word of mouth" pekee.

Haikuwa rahisi kwangu kuanza kuvitangaza vitabu vyangu. Kutokana na malezi, mila na desturi, nilijiuliza italeta picha gani katika jamii iwapo ningekuwa natangaza na kuuza vitabu vyangu. Nilielezea wasi wasi huo katika blogu hii, na jinsi nilivyojikomboa.

Leo sioni tatizo kutangaza vitabu vyangu. Nimejifunza na ninaendelea kujifunza umuhimu na mbinu za kufanya hivyo, kwa kusoma vitabu na makala mbali mbali. Ndio maana mara kwa mara naandika katika blogu hii kuhusu matamasha ya vitabu ninayoshiriki. Kusoma kumenileta katika upeo huu mpya. Elimu ni mkombozi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...