

Baada ya nusu saa hivi, ilianza shughuli ya kupeperusha bendera. Watu walielekezwa zilipowekwa bendera ili wachukue bendera ya nchi yao na kujiunga katika maandamano wakiwa wamebeba bendera. Nilikwenda nikaikuta bendera ya Tanzania, nikaibeba katika maandamano.
Tuliendelea kuongea na watu wa mataifa mbali mbali hapo kwenye meza yetu, tukapata pia fursa ya kuzunguka kwenye meza za wengine, na kupiga picha. Kwa namna ya pekee ninakumbuka tulivyozungumza na mama mmoja Mmarekani, kuhusu tofauti za tamaduni akatueleza yaliyomkuta Japani. Mila na desturi alizozizoea Marekani ziliwashangaza wenyeji. Nasi tulimweleza yanayotokea pale wa-Afrika wanapokuwa na wa-Marekani, kama nilivyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.



Baada ya kurejea kutoka kwenye tamasha, nimeangalia mtandaoni, nikaona taarifa za mama huyu kama vile hii hapa. Ninawazia kumwalika darasani kwangu nitakapofundisha tena kozi yangu.
Muda wote wa tamasha kulikuwa na vikundi vya burudani jukwaani na pia vyakula vya nchi mbali mbali. Ninaleta hapa baadhi ya picha za tamasha.