
Labda kuna haja ya kufafanua kitu tunachokilalamikia, maana wa-Tanzania hao hao inaonekana wanasoma sana vitabu ambavyo vinatungwa papo kwa papo kuhusu masuala kama vile mapenzi.
Vitabu hivi vinaandikwa haraka na kuchapishwa haraka na ndio maana naviita vitabu vya chap chap. Ni vijitabu, kwani vina kurasa chache tu.
Mwaka jana nilipokuwa Tanzania nilinunua kitabu cha aina hiyo kiitwacho "Pata Mambo, Part 5 ," kilichoandikwa na Fuad Kitogo (Dar es Salaam: Elite Business). Ingawa hiki ni kijitabu cha kurasa 40 tu, kinashughulikia masuala mengi kama inavyooneka katika picha ya jarida hapo juu.
Hivi vitabu vya chap chap si vitabu vyenye kiwango cha kuridhisha kitaaluma, bali vinawavutia na labda kuwaridhisha wasomaji wa ki-Tanzania. Katika ukurasa wa kwanza kuna maelezo haya: "Kitabu hiki ni mwendelezo wa vitabu vya Pata Mambo kuanzia namba moja vinavyopendwa kusomwa nchi nzima."
Kuwepo kwa vitabu hivi na kupendwa kwake ni changamoto kwetu sisi tunaodai kuwa utamaduni wa kusoma vitabu umefifia Tanzania. Labda uvivu tunaoulalamikia uko kwenye kusoma vitabu vikubwa vinavyotumia muda na fikra zaidi katika kuvisoma, tofauti na hivi vya chap chap ambavyo ni rahisi kuvisoma na kuvimaliza.