Wednesday, October 8, 2008

Watoto wa Marekani














Ingawa kazi yangu kuu hapa Marekani ni kufundisha katika kiwango cha chuo kikuu, kufanya utafiti katika taaluma zangu, na kutoa mchango wa mawazo na uzoefu kwa walimwengu kwa ujumla, napenda sana kukutana na kuongea na watoto, kuwasilimulia hadithi za Afrika, na kuwaeleza kuhusu maisha ya Afrika na masuala mengine ya maisha kwa ujumla, katika nchi yao na duniani.





Nimeshaongea na watoto kwenye miji mbali mbali, katika mikoa ya Colorado, Minnesota, Pennyslvania, na Wisconsin. Watoto ni watoto. Kitu kimoja wanachopenda ni hadithi. Nami nimekuwa na fursa nyingi za kuwasimulia hadithi za Kiafrika. Kitu kimoja kinachofurahisha ni jinsi watoto walivyo na akili ya kufuatilia hadithi na kuzichambua. Hata watoto wanaodhaniwa kuwa hawana akili sana au hawana moyo wa kupenda masomo, wanaonyesha msisimko wanaposimuliwa hadithi. Hapa kuna taarifa kuhusu nilivyokutana na watoto wa shule ya LeTort, Pennsylvania. Soma hapa














Jambo hili limenifanya nikumbuke habari moja niliyosoma kuhusu mwanasayansi maarufu Einstein. Inasemekana aliulizwa na wazazi kuhusu mkakati bora wa kuwaandaa watoto kuwa wanasayansi makini. Wazazi walidhani kuwa angeshauri watoto wafundishwe sana masomo ya sayansi tangu utotoni. Lakini Einstein aliwajibu kuwa watoto wasimuliwe hadithi. Alipoulizwa nini kifanyike baada ya hizo hadithi, yeye alilisitiza kuwa watoto wasimuliwe hadithi zaidi.














Habari hii niliisoma nilipokuwa masomoni katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, katika kujisomea mwenyewe vitabu. Mwanzoni sikuelewa kwa nini Einstein alikuwa na mawazo hayo. Lakini baada ya miaka mingi, nilipojaribu kusoma zaidi mawazo ya Einstein, nilianza kufahamu alikuwa na maana gani. Yeye aliamini kabisa kuwa kitu cha maana kwa mtoto ni kumhamasisha awe mbunifu. Ubunifu--dhana ambayo Waingereza wanaita "imagination"--ndio msingi, kwa mujibu wa Einstein. Nilivyozidi kufuatilia habari za Einstein, nilikuja kuelewa kuwa yeye mwenyewe kama mwanasayansi alikuwa anatagemea sana ubunifu, sio tu majaribio katika maabara. Alikuwa na ubunifu wa hali ya juu; hata baadhi ya nadharia zake wataalam wenzake waliziona kuwa ni ndoto. Lakini miaka mingi baadaye, kutokana na kuwepo vifaa vya uchunguzi, nadharia zake zimethibitishwa kuwa kweli.

Watoto wa Marekani ni sawa na watoto wengine. Wana dukuduku, na wanapenda kujua mambo. Wana masuali mengi. Sehemu kadhaa nilipoenda kuongea na hao watoto, walimu wao walikuwa na wasi wasi kuwa labda watoto wataniuliza masuali ya kijinga. Lakini mimi niliwaambia walimu kuwa watoto wana haki ya kuuliza masuali, hata yawe ya aina gani.

Watoto wanaoonekana katika picha hizi hapa walikuwa wanafunzi kwenye shule za mji wa Faribault, Minnesota. Mwalimu wao alikuwa ameniomba awalete hao watoto ili niwape mawaidha na motisha. Hakufafanua zaidi, bali mimi nilichukulia hii kama fursa ya kuwaeleza hao watoto jinsi dunia ilivyo pana na yenye fursa nyingi kwao, jinsi dunia ilivyo na nchi nyingi, kila moja ikiwa na mazuri yake. Ilikuwa ni siku nzuri kwa watoto hao na kwangu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...